08/04/2013

Mtambue, Jitambue, Watambue: Namna Yesu Anavyolitazama Kanisa (Mathayo 16:13-19)


(Hubiri nililolitoa sabato ya tarehe 6 Aprili, 2013, kanisa la SDA Magomeni-Tanga)

 

0. Utangulizi

“Unalionaje Kanisa lako?” Swali hili moja lakini laweza kuamsha majibu mengi. Watu wana mitazamo tofauti tofauti juu ya kanisa. Kwa macho ya mwingine kanisa ni kama “kimbilio la wanyonge,” huku kwa mwingine ni kama “nyumba iliyohamwa siku nyingi.” Kwa mwingine kanisa ni kama “mgodi wenye utajiri wa milele,” huku kwa mwingine  ni kama “shimo la mapokeo ya zamani.”  Kwa huyu KKKT ndilo kanisa, na kwa yule SDA ndilo kanisa. Kanisa linaweza kuonekana vizuri kwa macho ya mmoja na kwa mwingine likaoneka vibaya. Uzuri wa kitu upo katika macho ya mwonaji.

Lakini uzuri wa macho wa kitu sio lazima ufanane na ubora wake katika uhalisia wake. Ndio maana mwanamke niliyemwona mrembo jana leo ninamwona wa kawaida tu. Na kanisa nililoliona limejaa ngano jana, leo naliona limesheheni magugu. Macho yetu yanacheza-cheza, na hisia zetu huhamisha hamisha mitazamo yetu kama mawingu ya angani yanavyosukumwa sukumwa na upepo. Kama mtu anakuuliza unalitazamaje kanisa bora umwambie ukweli. Mwambie siwezi kukupatia kielelezo kinachofanana na kanisa uso kwa uso, isipokuwa picha yake niliyoichora mimi akilini mwangu. 

Tena mwambie asipoteze muda wake na muda wako na swali lake.  Mwambie, yupo wa kumuuliza, yaani Mungu. Mungu ndiye mwenye kanisa na analitazama ndani na nje, juu na chini. Mungu pekee analitazama kanisa katika uzuri wake na ubaya wake—hakuna kinachoweza kutoroka macho ya Mungu; maana, macho yake  yanawaka kama tochi. Ni Mungu pekee ndiye anayelitambua kanisa katika uhalisia wake.

Na hapo natamani kujua: hivi Mungu analitazamaje kanisa? Japo swali hili nauliza leo, lakini jibu lake lilitolewa zamani kama injili ya Mathayo ilivyoandikwa zamani. Katika injili ya Mathayo 16 Yesu anauliza mitazamo ya watu kwanza kumhusu Yeye. “Watu hunena Mwana wa Adamu kuwa nani?” (fungu 13). Hivi watu wananionaje? Kwa kuuliza swali hili, Yesu hakuwa anatafuta utambulisho wake, kana kwamba hajifahamu. Hapa Yesu alitaka kujua maono yao juu yake, ili awapatie maoni yake juu yao. 

Na Yesu akapewa majibu. Majibu yao yalikuwa tofauti-tofauti kulingana na maoni yao yalivyokuwa yametofautiana. Kulikuwa na hao waliosema Yesu ni Yohana Mbatizaji; wengine walisema Yesu ni Eliya; Yesu ni Yeremia; Yesu ni mmojawapo wa manabii. Bila shaka Yesu alihuzunishwa na majibu yao. Kwa sababu Yesu alikuwa zaidi ya Yohana Mbatizaji, Eliya, Yeremia, au nabii. Yesu aliona jinsi watu walivyochagua kumchora mawazoni mwao kama walivyopenda na si kumtazama kama alivyojitambulisha kwao. 

Ndipo Yesu akawageukia wanafunzi wake na kutaka kujua wanamtambuaje. Tusubiri tuone. Je, wanafunzi watafumbia macho uungu wa Yesu na kuyakazia tu kwa ubinadamu wake? Je, wanafunzi waliokuwa na nafasi ya kumtambua Yesu kwa miaka mitatu hivi watamwona tu kama mmoja wa wacha Mungu wa zamani? Yesu alikuwa ana hamu kujua wanafunzi wake wamechagua kumtambuaje. 

Bahati nzuri Petro akatoa jibu lililotuliza moyo wa Yesu. Petro akamwambia Yesu: “Wewe ndiwe Kristo (Masihi-Mkombozi aliyetumwa na Mungu) na Mwana wa Mungu aliye hai?” (Haleluya!). Na Yesu akampongeza haraka akimwambia, una bahati, huo sio mtazamo wa kibinadamu. Ninajua macho ya watu yanavyotazama; kwa vyoyote, “mwili na damu havikufunulia hili, bali baba yangu aliye mbinguni”(fungu la 18). 

Katika mazungumzo yaliyofuata; Yesu ni kama anasema, “kwa kuwa pamoja na ubinadamu wangu umekubali kuniona kama Masihi na Mwana wa Mungu, nami sasa nitakueleza ninavyokutazama wewe na wote wanaonikiri kama wewe. Niacheni sasa niwaambie ninyi ni nani.” Na hebu tuone Yesu anawatambuaje waumini wake?

1. Kanisa ni Kama Jengo lililosimama Mwambani

Kwanza kabisa ninamsikia Yesu anawatambua waumini wake kama  Jengo lililosimama Mwambani (angalia nami fungu la 18a): Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu. Ni mara mbili tu katika shuhuda za Injili zote nne[1] Yesu amekaririwa akitambua wafuasi wake kama kanisa (na kanisa likiwa na maana rahisi ya jamii ya watu wa Mungu). Na hii ni mara yake ya kwanza kufanya hivyo. 

Na ili tulielewe vizuri kanisa kama linavyoonekana mbele ya Yesu ni vizuri tutafute kuelewa ana maana gani anaposema, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu”? Yesu analilinganishaje kanisa kama Jengo juu ya mwamba? Na Petro anahusikaje hapo? Kuna uhusiano gani kati ya jamii ya waumini na  Petro na jengo na mwamba? Kwani Petro na jengo na mwamba vinawakilishaje kanisa? 

Tuanze na Petro. Hebu turudie kumsikia Yesu akimpongeza Petro kwa kumkiri ilivyo sahihi. Yesu anapompongeza anamwita kwa jina gani? Nasikia Yesu anamwita Petro kwa jina lake la zamani (jina alilopewa na wazazi wake)-Simoni Baryona. Na Yesu anapotaka kumhusisha na kanisa anatumia jina alilompatia kama mfuasi wake-Petro (Yoh 1:42). Simoni Baryona, kama yeye, hana uhusiano wowote na hicho ambacho Yesu anakwenda kukizingumzia kulihusu kanisa lake. Yesu anapomwita kwa jina Simoni mwana wa Yona, anaharakisha kumkumbusha kuwa yeye ni Petro. Petro ni jina la kiyunani (lunga ya waandishi wa Agano Jipya)  lenye kumaanisha “mwamba/ jiwe kubwa”. Lakini Petro na Yesu walizoelea kuzungumza lugha yao ya asili ya kiaramaki. Na jina la Petro kwa kiaramaki ni Kefa, likiwa na maana ile ile ya “mwamba”. Bila shaka kauli ya Yesu kwa Petro katika kiaramaki ilisikika hivi: “Wewe ndiwe Kefa (mwamba) na juu ya kefa (mwamba) hili nitalijenga kanisa langu”. 

Kwa kauli hii, ni wazi kwamba Simon Baryona ni mwamba na juu yake Kanisa litajengwa. Lakini kauli hii inanifanya nisugue kichwa na kuuliza hivi, Simon Baryona kweli ni mwamba? Mbona muda mchache baadaye Yesu alimwita Simon Baryona “shetani”(Mathayo 16:23)? Inawezekanaje kanisa lisimame juu ya mwamba wa namna hii? Simon Baryona ni mwamba? Mbona wakati huo Yesu alimwambia Simon Shetani amewataka ninyi apate kuwapepeta kama vile ngano, lakini nimekuombea wewe ili imani yako isitindike [isipungue]?” (Luka 22:31,32). Inawezekanaje Simon kama kweli ni mwamba ahofiwe kurushwa-rushwa kama kijiwe kwenge ungo? Simoni Baryona ni mwamba? Mbona baadaye mwamba ulisogea dhoruba ya mateso ulipoipiga huko Gethsemani na katika nyua za Kuhani Mkuu? Ni mwamba gani unaoweza kusogea? Simon Baryona ni mwamba? Kanisa linawezaje kuwa imara kama litajengwa juu ya “kefa” hili na mwamba huu? Bwana unamwona sawa sawa Simon Baryona? Simon mwana wa Yona ana umwamba gani hata aweze kutoa usalama kwa kanisa litakalojengwa juu yake? 

“Tulia” namsikia Yesu akiniambia. Ni kweli Simon mwana wa Yona ni kama wana wengine waliozaliwa na wanadamu. Lakini hapa ninamwona kama nilivyompatia jina Mwamba alipochagua kuwa mfuasi wangu. Sasa hivi na hapa hapa Petro ameishi sawa sawa na jina lake. Ninyi ni mashahidi: wengi wamechagua kuyumbishwa na upepo wa maoni ya watu kunihusu mimi. Wengi wameniona kama Yohana Mbatizaji, Eliya, Yeremia, na kama nabii tuu. Lakini Petro amekataa kuyumbishwa na maoni ya wengi. Hapa Petro ameonesha ukefa au upetro au umbwamba. Petro ni muumini wa kwanza kunikiri mimi kama Mwana wa Mungu. Imani ya Petro kwangu kwangu ni msingi imara na salama ambao juu yake nitalijenga kanisa langu. Umwamba wa Mwamba (Petro) ni imani yake kwa mwana wa Adamu kama Mkombozi na Mwana wa Mungu.

Na hebu tuulize historia, Je Yesu alijenga kanisa lake juu ya mwamba wa imani ya Petro? Ni kweli:

  • Katika mathayo 16:16 tunamkuta Petro kama mwanafunzi wa kwanza kumkiri Yesu mbele ya wanafunzi wenzake kama Mkombozi aliyetumwa na Mwana wa Mungu kabla wanafunzi wengine hawajafanya hivyo.
  • Katika Matendo sura ya 2, tunamkuta tena Petro kama mhubiri wa kwanza kumkiri Yesu mbele ya wayahudi wenzake kama Masihi na Mwana wa Mungu kabla wahubiri wengine hawajafanya hivyo.
  • Na katika Matendo sura ya 10 tunamkuta Petro kama mhubri wa kwanza kumkiri Yesu mbele ya wamataifa kama Masihi na Mwana wa Mungu kabla wahubiri wengine hawajafanya hivyo.

Kwa kifupi historia takatifu inashuhudia kuwa kanisa limesimama juu ya imani aliyokiri Petro. Na imani hiyo ni imani kama historia ya Ukristo inavyodhihirisha. Miaka 2000 imekuja na kuondoka, mataifa yamekuja na kuondoka, lakini kanisa limeendelea kuwepo likikiri kwamba Yesu ni Mkombozi na Bwana. Na mpaka leo wakristo wapo na wataendelea kuwapo wanapoendelea kushiriki ungamo la Petro: Yesu ni Mkombozi wa Ulimwengu na Mwana wa Mungu.

Haikuwa rahisi mara zote kwa Petro kumkiri Yesu kama alivyo mbele ya watu waliokataa kumtambua Yesu. Petro alipigwa viboko, tupwa gerezani, na mwishoni kusulubiwa kama Bwana wake. Haijawa rahisi kwa waumini wa Kristo kushikilia imani yao huku wakikabiliwa na  vitisho na upanga na njaa na dhiki na adha na dhihaka. Lakini ni imani yao ndiyo iliyowafanya waendele kuwepo. Ni imani yao imara kama ilivyo ya Ki-Petro ndio iliyowafanya wasalie kama jengo lililojengwa mwambani. 

Na hakuna msingi imara mwingine tuliopewa kusimamia isipokuwa imani yetu kwa Yesu. Hatuwezi kubakia kama wafuasi wa Yesu kama tutasita kumtangaza Yesu kama Kristo na Mwana wa Mungu. Inawezekana kwa kumtangaza hivyo tutaonekana hatuvumilii dini za wengine au tunavuruga amani na utengamano katika jamii. Inawezekana kwa kumkiri Yesu tukaonekana wajinga wasiokwenda na wakati; kwa kuwa, wasomi na watu maarufu hawamwoni mwana wa Mariam kama Mwana wa Mungu, hawamwoni mwalimu wa Galilaya kama Mkombozi wa dunia yote. Inawezekana wengi wakataka kumwona  Yesu kama wanavyotaka kumwona; yaani, nabii tu, mwalimu tu, mponyaji tu, mshauri tu. Lakini sisi hatuwezi kukubaliana na mitazamo yao isiyotulia kama mchanga wa baharini na tukabakia wakristo shupavu. Inahitajika imani kali kumtangaza Yesu kama Mwokozi na Bwana ukiwapo nyumbani na kazini na mjini; na hiyo ndiyo imani  imara kama jengo mwambani. Bila kujali kisomo chao, makabila yao, au madhehebu yao, hakika waumini wasio na haya kumtangaza Yesu alivyo, ndio Kanisa litakalosalia kuwepo mpaka mwisho wa wakati.
Kanisa la Mungu ni Jengo linalosimama juu ya mwamba wa imani. Ndivyo linavyosimama mbele ya macho ya Yesu.

2. Kanisa ni kama Jeshi lililoko uwanja wa vita

Yesu aliposema atalijenga kanisa lake mwambani hakutaka tufikiri litakuwa salama mbali na hatari na ushindani. Maana, Yesu analitambua pia kanisa lake kama Jeshi lililo katika uwanja wa vita (angalia  Math 16:18b). Yesu anasema, “milango ya kuzimu haitalishinda [kanisa langu].” Kanisa ni kama Jeshi lililoko vitani likipambana. 

Lakini linashindana na nani? Yesu ameweka wazi, Kanisa linashindana na “milango ya kuzimu”. Na kuzimu haiwakilishi kitu kingine isipokuwa mauti na kifo (uf 1:18). Mahali pengine tunasoma kwamba dhambi huzaa mauti (Yakobo 1:15). Na kama dhambi huzaa mauti, basi kanisa linapambana na dhambi kama mzazi na mauti kama mtoto. Adui wa kanisa sio wewe sio mimi na wala si wao; adui wa kanisa sio wapagani, adui wa kanisa sio viongozi wake wala washiriki wake; isipokuwa tu kama ni vibaraka wa dhambi na mauti.

Kanisa liko vitani, na Yesu anataka tulitazame hivyo. Kanisa halijatulia na haliwezi kutulia. Mpaka limeondolewa uwanjani mwa vita, mbali na dhambi na kifo, kanisa haliwezi kutulia. Wale wanaolilia utulivu na amani watusubiri malangoni mwa Yerusalemu. Huko ndiko hakuna maombolezo wala kilio wala maumivu (ufu 21:4). Wale wanaolalamikia magugu yamezidi kanisani, au uovu umezidi kulinukisha kanisa, au siasa zimezidi kulichafua kanisa waliacha kanisa la Mungu. Wanyamaze wakisubiri siku ya hukumu ifike; siku ambayo wema na wabaya watatenganishwa milele na vita dhidi ya wema na uovu itamalizwa milele. Kabla ya hapo kila mmoja sharti aelewe Kanisa ni Jeshi lililoko vitani na hivyo ndivyo Yesu anavyoliona.

Wewe na mimi tuko vitani. Inawezekana tumemkimbia Yesu, tumemkana hadharani au sirini, hilo lisitukatishe tamaa. Tukumbuke  tuko vitani. Tunaweza kutetereka na kujeruhiwa, si neno, kwa  hatutaitupilia mbali imani yetu. Mapambano yanaweza kuwa makali na majeraha yakatuliza usiku na mchana, lakini hatutaachilia imani yetu kwa Yesu. Vidole vya wanaotushtumu na kutushtaki vinaweza kutusonda na kutukumbusha tulivyomkana Yesu, lakini hatutakata tamaa kutumaini wema wake kutusamehe na uweza wake kutusimamisha tena. Kama tutabakia uwanjani mwa vita na silaha ya imani yetu kwake ikisalia mikononi, hakika tutasonga mbele kwa ushindi hadi ushindi. 

Yesu amekwisha sema, “milango ya kuzimu” haitatushinda. Haleluya! Ijumaa adui anaweza kudhuru miili yetu, Ijumaa adui anaweza kukimbiza marafiki zetu mbali nasi, Ijumaa adui anaweza kutupiga mapigo, akanyanganya nguo zetu na heshima yetu. Lakini, bado ijumaa tunaweza kukabidhi roho zetu kwake Yeye awezaye kuzitunza. Kama jiwe la adui lilishindwa kumzuilia Yesu kaburini jumapili ile ya ufufuo, kadhalika hata sisi “milango ya kuzimu haitatushinda.”  

Kanisa ni imara kama Jengo mwambani na hodari kama Askari vitani. Na ninafurahi kuwa ndivyo Yesu anavyowatazama waumini wake.

3. Kanisa kama mlinzi wa malango ya Ufalme

Mwishoni, katika aya yetu Yesu anamalizia kulitambulisha kanisa kama Mlinzi wa malango ya ufalme (angalia nami fungu la 19): “Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni”. Kefa nitakupa  wewe funguo [ni wewe ukisimama pamoja na waumini wote watakao nikiri mimi}. Wewe ni mshika funguo, mlinzi katika malango ya ufalme. Unaweza kufunga na kufungua, kuruhusu na kuzuia, wewe ni mlinzi. 

Lakini Petro na wote wenye imani kama yeye ni walinzi wa namna gani mlangoni pa ufalme? Petro anaweza kufungulia au kuzuilia nini mlangoni mwa ufalme? Kabla hatujalielewa hilo: unakumbuka maneno ya Yesu kwa walimu wa dini katika Luka 11:52? Yesu alisema, “Ole wenu, enyi wana-sheria, kwa kuwa mmeuondoa ufunguo wa maarifa; wenyewe hamkuingia, na wale waliokuwa wakiingia mmewazuia.” Mahali pengine Yesu anawalaumu Mafarisayo (washika dini) kwa kosa hilo hilo (Math 23:13). Mara zote hizo funguo zinasimama badala ya maarifa na ujuzi waliopewa. Wana-sheria na Mafarisayo walikuwa na ujuzi wa maandiko ambao ungeweza kuwanufaisha wao na wengine. Lakini hawakutumia maarifa hayo ipasavyo.

Na kwa Petro na waumini wote, ujuzi na maarifa ya ufalme umetolewa.
Petro na waumini tumefunuliwa na Baba wa mbinguni kumwona Yesu kama Masihi na Mwana wa Mungu. Ufunuo huo ni ufunguo langoni mwa ufalme. Injili ya Yesu yaweza kuwafungulia malango ya ufalme wote wanaoipokea na kuwafungia malango hayo hayo wanapoikataa. Petro na sisi tumepewa funguo nyeti.

Na hivi Petro alizitumiaje funguo zake? Petro alizitumia funguo hizo mara nyingi:

  • Mara ya kwanza ni siku ya Pentekoste alipowaonesha wayahudi  kuwa Yesu ni Masihi na Mwana wa Mungu aliye hai. Akawaambia, “Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi” (Mdo 2:38). Na siku ile maelfu walifunguliwa malango ya ufalme.
  • Mara nyingine Petro alimfungulia malango ya ufalme, Kornelio na nyumba yake na wote wakaingia (Mdo 10).
  • Mara nyingine Petro  akiwa na Yohana alimfungulia kiwete malango ya ufalme naye akanyanyuka akiingia hekaluni akirukaruka kwa furaha.
  • Mara nyingine Petro na Yohana wakawafungulia wasamaria nao wakapokea Roho Mtakatifu.
  • Lakini mara nyingine Petro alimfungia Anania na Safira na hawakuingia katika ufalme.

Funguo alizopewa Petro ndizo tulizopewa. Tumepewa kuwafungulia watu wamjue Yesu kama Mkombozi nao wafunguliwe. Na kama kila mmoja wetu aliyepewa funguo hizi atazitumia wangapi wangepokea msamaha wa dhambi, wangapi wangefunguliwa na utumwa wa dhambi, wangapi wangepokea uponyaji. Wengi wamesimama langoni mwa ufalme wakisubiria mtu awafungulie. Watu hao wapo magerezani na hospitalini na kazini na manyumbani na kwenye facebook na kwenye youtube na kwenye simu. Wafungulie, waingie. Zitumie funguo zako za ufalme.

0. Mwisho

Sihitaji kuuliza tena unalionaje kanisa. Kristo mwenye kanisa amekwisha kulitambulisha kanisa lake. Yesu ametuambia kuwa kanisa lake ni kama Jengo mwambani, askari vitani, na mlinzi mlangoni. Yesu anakwambia unabakia salama unaponiamini, unapata ushindi unaponiamini, na uwasaidie wengine waniamini. 

Na Mungu akubariki unapomtambua Yesu kama alivyo, akubariki unapojitambua kama anavyokutambua, na akubari unaposaidia wengine wamtambue. Mtambue, jitambue, watambue.


[1] Ni katika Mathayo sura ya 16 na 18 tu Yesu amekaririwa akizungumzia wafuasi wake kama kanisa.

Hakuna maoni: