14/05/2013

Uponyaji Bethzatha: “Je, Wataka Kupona?” (Yoh 5:1-14)


Utangulizi

 Kama unatamani maisha bora zaidi ya uliyonayo sasa, usiondoke hapa; maana, unaweza kupata maisha mapya sasa. Lakini kabla ya yote unahitajika  kujibu swali rahisi lakini la muhimu. Swali ni hili, “Je, Wataka Kupona? Huwezi kukwepa kujibu swali hili kama unahitaji kupona. Mganga pekee anayeweza kukuponya haanzi kukutibu kabla hajakusikia utamjibuje. Na ndivyo Yesu Mkombozi alivyomuuliza mgonjwa mmoja swali hilo la msingi tunaposoma katika Injili ya Yohana 5:1-14:

1 Baada ya hayo kulikuwa na sikukuu ya Wayahudi, naye Yesu akaenda Yerusalemu.
 2 Huko Yerusalemu, karibu na mlango uitwao Mlango wa Kondoo, kulikuwa na bwawa la maji liitwalo kwa Kiebrania Bethzatha, ambalo lilikuwa nabaraza tano zenye matao.
 3 Humo barazani mlikuwa na wagonjwa wengi wamekaa: vipofu, viwete na waliopooza.*fa*
 4 missing 4maana mara kwa mara malaika alishuka majini nyakati fulani na kuyatibua. Mtu yeyote aliyekuwa wa kwanza kuingia majini baada yamaji kutibuliwa, alipona ugonjwa wowote aliokuwa nao.
 5 Basi, hapo palikuwa na mtu mmoja aliyekuwa mgonjwa kwa muda wa miaka thelathini na minane.
 6 Naye alipomwona huyo mtu amelala hapo, akatambua kwamba alikuwa amekaa hapo kwa muda mrefu, akamwuliza, "Je, wataka kupona?"
 7 Naye akajibu, "Mheshimiwa, mimi sina mtu wa kunipeleka majini wakati yanapotibuliwa. Kila nikijaribu kuingia, mtu mwingine hunitangulia."
 8 Yesu akamwambia, "Inuka, chukua mkeka wako utembee."
 9 Mara huyo mtu akapona, akachukua mkeka wake, akatembea. Jambo hili lilifanyika siku ya Sabato.
 10 Kwa hiyo baadhi ya Wayahudi wakamwambia huyo mtu aliyeponywa, "Leo ni Sabato, si halali kubeba mkeka wako."
 11 Lakini yeye akawaambia, "Yule mtu aliyeniponya ndiye aliyeniambia: `Chukua mkeka wako, tembea."`
 12 Nao wakamwuliza, "Huyo mtu aliyekwambia: `Chukua mkeka wako, tembea,` ni nani?"
 13 Lakini yeye hakumjua huyo mtu aliyemponya, maana Yesu alikuwa amekwisha ondoka mahali hapo, kwani palikuwa na umati mkubwa wa watu.
14 Basi, baadaye Yesu alimkuta huyo aliyeponywa Hekaluni, akamwambia, "Sasa umepona; usitende dhambi tena, usije ukapatwa na jambo bayazaidi."

Bethzatha



Swali “Je, Wataka Kupona? Limeulizwa katika kisa hiki. Kabla hatujaelewa swali hili, nakualika tutembelee eneo la tukio, na kufuatilia kwa karibu yaliyotokea katika hadithi hii. Kisa chenyewe kimetokea kandokando ya bwawa lililoitwa Bethzatha. Bethzatha ni jina lilitoholewa na Yohana kutoka kiebrania kwenda kwa kigiriki na limebakia hivyo hivyo katika biblia zetu za kiswahili—Bethzatha. Yohana  kama mwanahistoria makini hakumuacha msomaji wake akisie mwonekano wa bwawa lenyewe. Anatuambia kuwa bwawa lilikuwa limezungukwa na matao (mabaraza) matano. Kwa muda mrefu wasomi wasioamini walidhani hadithi hii ni ya kutunga, wakisema eti hakuna mahali kihistoria palipojulikana kama Bethzatha. Mpaka mwaka 1940 wafukuaji wa mambo ya kale (wajulikanao kama wana akiolojia)  walipofanikiwa kupata jiwe la kale lenye jina Bethzatha. Hivyo, hii si hadithi tu yenye fundisho. Hadithi ni ya hakika kama Bethzatha yenyewe ilivyo mahali halisia.

Yohana akitusimulia kisa kwa nia ya kutuminisha zaidi uhakika wa kihistoria wa hadithi yake anaendelea kutuambia Yesu alipitia lango gani akiingia Yerusalemu. Anasema Yesu aliingia Bethzatha kupitia lango lililojulikana kama “Lango la Kondoo” (leo watalii wanaozuru mji wa Yerusalemu ya zamani wanaambiwa panaitwa “Lango la mtakatifu Stefano.”).  Hili ni lango lililotumika kupitishia kondoo ndani ya mji wa Yerusalemu tayari kwa mauzo kwa mahujaji. Yesu kama hujaji aliingia mjini kwa kupitia lango hili, kaskazini-mashariki mwa mji. Karibu na soko hili Yesu akakutana na Bethzatha yenyewe. Ukubwa wa Bethzatha ni futi 150 kwa 300; kubwa la kutosha kupokea watu kwa mamia. Wenyeji wa Yerusalemu wanapaita mahali hapa Bethzatha, huenda wakimaanisha "Nyumba ya Neema." Nyumba hii ni bwawa la maji yanayoaminiwa kuponya maradhi. Na utaonai eneo limefurika wagonjwa waliotafuta neema ya kufunguliwa (kumbuka watu walivyojaza kwa babu). Anapokuja hapa Yesu anakutana na hospitali isiyo na kuta, kliniki ya iliyojaa vipofu, na viwete, na walioopoza wakiwa wamejazana! (Fikiria harufu ya kondoo upande huu na ya wagojwa upande huu, jiulize kwa nini Yesu aingie Yerusalemu kupitia lango hili!)

Inaonekana hakuna anayefahamu mpaka sasa nani aliyeingia hapa katika “Nyumba ya Neema.” Wagonjwa wa Bethzatha hawajui kuwa mahujaji aliyetokea Galilaya ni Bingwa wa magojwa! Yesu anawatazama kwa huruma.  Apande juu ya dari na atangaze kuwa saa ya neema imefika? Apaze sauti yake kuwaambia amefika awasaidie? Kwamba sasa anakwenda kuifunga hospitali hii na kuwarudisha wote nyumbani? Hapana. Huo sio mpango-kazi wa Yesu. Huwa Yesu hatangazi kazi zake, ila kazi zake zinamtangaza. Yesu akiwatazama wagonjwa, macho yake yakawa yakikimbia-kimbia kumpata mgonjwa aliyechoka kupita wote.

Katika wagonjwa wote, Yesu akaamua kumkaribia mgonjwa mmoja tu. Mgonjwa hajamwita Yesu na wala hamfahamu, lakini huyu ndiye anayetaka kumponya. Mgonjwa hajawahi kuita ama kuimba “usinipite
Mwokozi, unapodhulu wengine” lakini huyu ndiye Yesu anataka kumfikia. Kweli Bwana humrehemu amurehemuye na kumbariki ambarikiye, bila kujali imani ya mpokeaji. Mgonjwa huyu hana imani atapona tena. Mwanzoni aliamini atapona, lakini si sasa. Mwanzoni ndugu na jamaa zake waliamini, hata wakasaidia kumleta yalipo maji ya uzima. Lakini sasa hawaamini tena atapona, ndio maana wamemwacha mwenyewe. Kwa miaka 38 ameteseka na sasa yupo hapa mwenyewe pembezoni mwa maji ya uponyaji akisubiria uponyaji. Hana shamba, hana nyumba. Mali yake ni mkeka wake anaoulalia. Mikono yake imekakamaa kwa kutembea chini akijibuluta kama omba-omba. Ugonjwa wa kupooza miguu umewasababishia baadhi ya wagonjwa kujikojolea bila wao kuwa na habari. Inawezekana Yesu anapomkaribia mgonjwa ana harufu ya mkojo, mgonjwa amechoka!

Yesu anapomfikia, anainama kuanza kuongea naye. Hapo nyuma ni Nikodemu kiongozi wa Kiyahudi na afisa mwingine wa kirumi ndio walioanza kumsemesha Yesu. Lakini alipoongea na mwanamke msamaria aliyetengwa na sasa mgonjwa mchovu ni Yesu ndiye anayeanza kuongea. Yesu anajali masikini zaidi ya watu wote! Yes akamuuliza mgonjwa,"Je, Wataka Kupona?" Utadhani mgeni huyu anayesimama mbele ya mgonjwa haoneshi kumjali mgonjwa; atamuulizaje mgonjwa, "Je, Wataka Kupona?" Kwani yeye hajui mgonjwa yupo Bethzatha?

Je, Wataka Kupona?

Je, Uko Tayari Kukaribiana na Changamoto za Mtu Mwenye Afya?

Kwa haraka haraka utadhani kumuuliza mgonjwa kama anataka kupona ni kufanyia mzaha zahama yake, lakini ukilitazama swali lenyewe kwa ukaribu haionekani hivyo. Mara nyingine wagonjwa hawataki kupona. Mgonjwa anapopona anakuwa amemaliza seti moja ya matatizo lakini na kuibua mengine. Kuna changamoto za maisha zinazowafikia walio na afya tu! Kwa upande wa mgonjwa huyu, kwa miaka 38 hajawahi kugombana na viongozi wa dini, lakini leo atakapotoka miguuni pa Yesu atakabiliana na changamoto ya kutofautiana na viongozi wake wa dini. Atakapoponywa na kuamuliwa kujitwika mkeka wake na aende atakuwa anakwenda kinyume na walimu wake wa dini walivyomfundisha. Kumbuka kuwa kati ya mambo 39 wayahudi waliyokatazwa kutoyafanya siku ya sabato kwa kuwa kwa kuyafanya ni kutenda kazi mojawapo ni kubeba kitanda siku ya sabato. Mgonjwa yupo tayari kukutana na changamoto ya kutofautiana na viongozi wake? Atakuwa tayari kuwajibika kwa matendo yake kama mtu mzima, au ataishia kusema, “msinilaumu mimi, si kosa langu. Muulizeni aliyeniponya”? 

Cha ajabu ndicho mzee huyu alichokifanya (fungu 10). Alipotakiwa kuwajibika kwa matendo yake inawezekana akafika mahali akasema moyoni mwake, kuliko vita hii maisha yalikuwa bora pale kwenye mkeka wangu. Yesu akatafuta kumwokoa mgonjwa huyu na majuto ya kuingia kwenye maisha ya kujitegemea. Kwa lugha nyingine alikuwa anamuuliza, uko tayari kulipa gharama ya kuwa mtu mzima? Unahiari kukabiliana na changamoto za Mtu mwenye afya?

Je, Uko Tayari Kupoteza Fursa za Kubakia “Kwenye Mkeka”?

Lakini Yesu ana nia nyingine anapouliza mgonjwa wa Bethzatha swali hili. Kabla hajamponya, Yesu anamtaka ajihoji kama yupo tayari kupoteza fursa alizokuwa akizifaidi kama mgonjwa. Kumbuka wagonjwa kama huyu katika Yerusalemu ya karne ya kwanza walikuwa omba-omba. Omba-omba walijikimu maisha kwa fadhila za mahujaji waliokuja kuabudu Yerusalemu. Na mahujaji waliamini watapata thawabu kubwa
kwa kuwasaidia masikini wanapotembelea mji mtakatifu. Mgonjwa alifaidi fursa zote hizi akiwa kwenye mkeka wake. Rafiki, Kuna fursa za kubakia kwenye mkeka, na kabla ya kuponywa unahitajika kuhihari kupoteza faida hizo:
  • Ukiwa kitandani, shida ya kuamuka asubuhi kwenda shule haipo tena, Tuition huendi tena, homework hutakiwi kufanya tena; isipokuwa, unaletewa juisi, chips zinakaangwa, kuku wanapoteza maisha kwa ajili yako, unakaa ukiangalia TV muda wote. Lakini ukipona fursa zote hizi umezikosa. Je, wataka kupona?
  • Ukiwa mlevi, unajisikia kuchangamka, aibu hupotea, huna mawazo ya kukusumbua: hufikirii Mungu amenikataza nini, hukifikirii nitailisha nini familia yangu. Lakini ukipona fursa zote hizi umezikosa. Je, wataka kupona?
  • Ukiwa tapeli na fisadi, unajisikia mwerevu, unakula bila jasho, una muda wa kutosha kwa starehe zako. Lakini ukipona fursa zote hizi umezikosa. Je, wataka kupona?
  • Ukiwa kwenye ndoa haramu, bado kuna heshima unayopata (nimeoa, nimeolewa) na  matunzo unayofaidi. Lakini ukipona, fursa zote hizi umezikosa. Je, wataka kupona?
  • Ukiwa mwenye hasira, umezoea kumkasirikia mwenzi wako wa zamani, wazazi wako au Mungu wako, kuna utamu fulani unausikia unapokasirika. Lakini ukipona utamu umeukosa. Je, wataka kupona?
  • Yesu anapouliza, Je, unataka kupona? Kweli anahitaji kujua kama uko tayari kupoteza fursa zote unazozifaidi sasa uwapo kwenye mkeka wako.

Yesu amesimama pale pale na swali lile lile. Je unataka kupona? Utamjibuje? Utajibu: “labda baadaye?”, “Ndiyo”, au “Hapana”?

"Ninataka kupona" 

Bahati nzuri mgonjwa wa Bethzatha alitaka kupona. Japo hakutoa jibu la moja kwa moja lakini alionesha anataka kupona. Akaanza kumsimulia Yesu jinsi alivyohangaika kupata uponyaji bila mafanikio. Aliamini kama kila mmoja mitaani alivyoamini kwamba maji katika bwawa hili yakitibuliwa wa kwanza kuingia anapona. Imani yake ndiyo iliyomleta hapo, japo imani hiyo bado haijazaa matunda. Anamweleza kuwa amekosa mtu wa kumudumbukiza haraka maji yatibuliwapo. Utadhani anajaribu kumshawishi Yesu amsaidie kumtumbukiza siku maji yakivurugwa eti na malaika.Shida yake alikosa njia sahii ya uponyaji. Yesu akamsikiliza akimuhurumia. Bila kutafuta kumsahihisha kuwa imani yake kwa maji haya ni potovu na yeye hana muda na hadithi za mitaani, Yesu akaamua sasa kumponya.

"Simama, jitwike mkeka wako, uende" 

Yesu akitambua mgonjwa hamtambui yeye ni nani, akaamua kutoa amri ya kimamlaka: “Simama, jitwike mkeka wako, uende.”

“Simama, jitwike mkeka wako”

Ukinukuu maneno haya moja kwa moja toka kigiriki, lugha aliyoitumia Yohana utaona maana iliyokusudiwa: Simama (kitendo cha mara moja[aorist imperative]), jitwike mkeka wako (kitendo cha mara moja[aorist imperative]). Yesu anatamka kwa kishindo na anataka kitendo cha mara moja. Mara moja aamuke na aachane na mazingira ya ugonjwa wake. Hilo ni tendo la mara moja na upesi. Yesu hamwachii mgonjwa asema, “asante sasa nimeweza kusimama, ila kkilago changu nitakiacha hapa, ikitokea shida tena niikute nafasi yangu pembezoni mwa maji ya uponyaji.” Hapana, Yesu anamtaka mgonjwa aachane na maisha yake ya kale,. Aachane na aliyokuwa anayafanya. Anamtaka asimame na kujitwika godolo lake.

Kama mgonjwa wa Bethzatha ukitaka kupona, “simama, jitwike godolo lako uende”:
  • Ukitaka kuachana na ugonjwa uliokulaza miaka yote, nyanyuka tupa shuka na blanketi ondoka kitandani, simama jitwike godolo lako
  • Ukitaka kupona kutoka uvivu na kutojituma, simama jitwike mkeka wako
  • Ukitaka kupona kutoka kulazimika kufanya kazi na Sabato, achana na kazi hiyo, simama jitwike mkeka wako na uende.
  • Ukitaka kupona unywaji, kamwage chupa iliyosalia kabatini, achana na wanywaji wenzako, usizubaye  katika mazingira ya unywaji, simama jitwike godolo lako
  • Ukitaka kupona na hasira dhidi ya mpenzi wako, achana na mawazo yanayoamsha hasira yako, acha kujihurumia, acha kivitazama vidonda au makovu uliyosababishiwa, simama jitwike mkeka wako.
  • Ukitaka kupona kutoka mapenzi haramu, futa namba yake ya simu, usimpigie, usimtembelee, usiongee naye, simama jitwike mkeka wako.

Rafiki usisite kusimama na kujitwika gogoro lako. Kama kwa kusimama na kujitwika mkeka wako unaogopa utapoteza fursa ya kuwa pembezoni mwa bwawa la maji uliyoyaamini, tupilia mbali hofu yako, maana maji uliyoyaamini na kuyasubiria hayaja kukusaidia na ukiendelea kubakia hapo utakufa tu.
Mpendwa, najua mazoea yanatabu. Tunajisikia salama tukibakia kwenye mtindo wa maisha tuliyoyazoea. Lakini ndugu kama mazoea hayo hayatupi usalama, ni bora kuchukua uamuzi mgumu: achana na mazoea hatarishi. Tumeona Yesu akikutana baadaye na mgonjwa aliyepona na kumtahadharisha asirudie mtindo wake wa maisha ya dhambi yasije yakampata makubwa zaidi ya yaliyompata! Kama jicho lako, au mkono wako au miguu yako inakukosesha achanana viungo vyako, vingo’oe na vitupilie mbali, ni bora uingie uzimani ukiwa mpungufu kuliko kuingia Jehanamu ukiwa na viungo na mazoea yako hatarishi

 “...uende”

Tumesema ukiyasoma maneno aliyotumia Yesu katika lugha ya mwandishi utaona maana iliyokusudiwa ikibaki wazi: Simama na Jitwike [aorist imperative] ilikuwa ni amri ya mara kwa kitendo cha mara moja. Lakini sasa tunaposoma agizo la mwisho katika lungha hiyo hiyo ya awali (kiyunani) tunakuta Yesu anamtaka mgonjwa afanye kitendo cha mara kwa mara. Yesu anapomuagiza mgonjwa Uende, Yesu anamwambia mgonjwa adumu kutembea. Mgonjwa asiache kutembea, aendelee kutembea.

Mgonjwa wa kupooza aliyeponywa baada ya kusimama na mkeka kichwani angeweza kusema, “ndio nimesimama na godolo nimebeba, lakini miguu bado inauma, sikuzoea kutembea, hebu nisimame kidogo.” Hilo Yesu hakulitaka mgonjwa alifanye ndio maana akamwabia, “dumu kutembea”. Ushauri ambao Yesu anampatia ni ushauri ambao daktari yeyote wa mifupa angempatia mgonjwa wa Bethzatha. Mgonjwa wa mifupa ni lazima atembee mara kwa mara! Mgonjwa wa Bethzatha ni lazima adumu kutembea. Haitoshi asimame na kilago chake kichwani. Haitoshi apige hatua moja au mbili na kutegemea atabakia mzima. Ndio maana Yesu anamwambia dumu kutembea.  Na alichomwambia mgonjwa yule ndicho anatuambia sote: dumuni kutembea katika maisha mapya!
  • Haitoshi kuacha kulaghai na kutapeli kwa mwaka mzima, lakini ukibanwa sana unaongeza uongo kidogo ili ujikwamue, dumu kutembea katika mazoea mapya
  • Haitoshi kuacha kuvuta au kunywa kilabuni, lakini nyumbani unatumia chupa moja au mbili, dumu kutembea katika mazoea mapya.
  • Haitoshi kuacha kumsalimia mpenzi wako haramu kwa wiki moja, lakini wiki ya pili unasema hebu nimsalimie kidogo, dumu kutembea katika mazoea mapya
  • Haitoshi kuacha kukasirika ukiwa ndani katika nyumba ya sala, lakini tukitoka ibaadani huwezi kumsalimia, tembea sasa katika mazoea mapya.
  • Haitoshi kuanza kwenda katika nyumba ya ibaada kwa wiki mara moja au mbili lakini wiki zingine huuendi, dumu kutembea katika mazoea mapya

Rafiki huo ndio ukweli. Tukidumu kutembea katika uzima mpya tuliopokea, tutabakia uzimani, na hakuna hatari kwamba tutarudi kifoni.

Mwisho

Kwa hiyo swali ambalo Yesu alilomuuliza mgonjwa wa Bethzatha ndilo analomuuliza mtu yeyote anayetaka mabadiliko.  Je, wataka kupona? Hili ni swali linalostahili kujibiwa sasa kama wahitaji kupona sasa. Swali hilo linalenga nini katika maisha yako? Unahitaji kupona kutoka shida gani? Kama Yesu hakuwa na haja ya kukusaidia, unadhani angeuliza, unataka kupona?

Ombi pamoja nami ombi hili:

Bwana Yesu, hapa unasimama karibu yetu. Unajua mahali ulipotukuta. Tupo penye mkeka wetu, wapweke katikati ya watu. Unajua kushindwa kwetu maishani. Kama ni kushindwa kusamehe, kushindwa kupenda, au kushindwa kuachana na mazoea yanayotuharibu, Bwana wewe watujua. Sasa Bwana, umetuuliza leo kama tunataka kupona. Tusaidie tutake kusaidiwa. Tusaidie tuseme “Ndiyo, Bwana, Ndiyo, Bwana”. Hapa hapa Bwana kuna mtu anaomba, “nataka nipone, niko tayari kuponywa”. Bwana sikia maombi yetu. Sema nasi kwa sauti yenye nguvu na ya uponyaji, gusa akili zetu na mioyo yetu, mpaka tusikie maneno yako, “inuka, chukua mkeka wako uende” Tuachanishe Bwana na maisha yetu yaliyopita, na tembea nasi katika upya wa maisha. Ameni

Hakuna maoni: