16/04/2013

Samson: Apoteza Maisha lakini Aokoa Roho (Waamuzi 16:28)

Samson: Apoteza Maisha lakini Aokoa Roho  (Waamuzi 16:28)

 

Mimi ni Samson.

Kabla sijakusimulia kisa cha maisha yangu niruhusu kwanza nijitambulishe. Mimi naitwa Samson. Habari zangu mmezisoma katika kitabu cha Waamuzi sura ya 13 mpaka 16. Baba na mama yangu waliniita Samson, (kwa lugha yangu ya mama, kiebrania, walitamka jina langu, shemesh, kwa kiswahili chake, jua) wakimaanisha “mtu mwenye nguvu.”  Jina langu lilikuwa la pekee. Hata kuzaliwa kwangu hakukuwa kwa kawaida. Ukimwondoa Yohana na Yesu mnaowakumbuka, hakuna aliyezaliwa namna yangu kama mimi. Malaika aliwaambia wazazi wangu: “mnaenda kupata mtoto—mtoto mwenye kazi maalumu maishani. Kusudi la maisha yake ni kukomboa Israel toka mikono ya Wafilisti”. Utume wangu ulikuwa wazi, njia yangu ya maisha ilikuwa imetandikwa wazi mbele yangu. Kisha malaika wa Bwana akaendelea kusema, “Jambo pekee mnalopaswa kujua mnapaswa kumlea kama mnadhiri wa Mungu,  jambo la pekee analopaswa kukumbuka, anapaswa kuishi kwa kuzingatia vigezo na masharti ya mtu aliyetengwa na Mungu kwa kazi maalumu.”  
Nani kama Samsoni?!
Nikaanza kukua. Miaka ilipokua ikiipita na misimu ikizunguka ndivyo na umri na nguvu zangu zilivyozidi kuongezeka. Na nikaja kuwa na nguvu kweli, kweli. Hakuna ambaye hakunifahamu. Kila mmoja alilijua jina la Samson. Kila mmoja alilitamka jina langu kwa heshima. Na wasingeweza kunidharau. Nilikuwa na nguvu. Hakuna mwanamume chini ya jua aliyewahi kuwa na nguvu kunizidi. Nini? Mnadhani ninazidisha maneno kunogesha radha ya hadithi? Hebu  niwapatie ushahidi na muamue wenyewe kama madai yangu ni ya kweli au uongo.

Nilipokwenda Timna

Mapema nilipokua ningali kijana mbichi nilijaribu kupiga mbizi katika bahari ya mahaba. Ikatokea nikavutwa na mwanamke mmoja wa ovyo. Mwanamke huyo hakutoka katika jamii ya watu wangu. Na haikuwa shida, mbona wengi walioa au kuolewa na wapagani. Enzi hizo ilikuwa “ruhsa” kujifanyia lolote roho yako itapenda. Hapakuwepo mfalme katika Israeli (Wa 17:6; 21:25), Yoshua aliyeingiza Israeli alikuwa amekufa siku nyingi na Sauli mfalme wa kwanza wa taifa letu alikua hajaja. Na mimi, roho yangu ilimpenda mwanamke mfilisti aliyeishi Timna. Hakuwa muumini. Macho yangu yalipogongana na yake, nilivutwa naye, au niseme mrembo aliniwasha tamaa. Nilijua ninamtaka. Nikawaambia wazazi wangu, “Mnipatie huyo, maana ananipendeza sana” (14:3,7). Kawaida, wazazi wangu hawakupendezwa na uamuzi wangu wa kumuoa asiyeamini, lakini nilikuwa mtoto kichwa-ngumu na mwishowe wazazi wangu wakakubaliana nami.

Ili kukamilisha maandalizi ya arusi ilibidi niende Timna. Safari ilikuwa ya hatari; miamba na vichaka vimetanda njiani. Njia inanyoka-inapinda, inainuka- inashuka kufuatisha vilima vya Kaanani. Kulikuwa na maficho ya kutosha kwa majangiri. Lakini hilo halikusumbua mawazo yangu, zaidi nilikuwa nikifikiria utakuwaje usiku wa kwanza wa arusi na honeymoon. Ghafla macho yangu yakakutana na kitu kibaya kuliko jambazi—nikaona wingu la dhahabu likirukia toka nyuma yangu kuja karibu na mabega yangu. Alikuwa simba. Akifoka na kujirusha hewani kunifikia. Ungekuwa wewe ungefanya nini? Duaa? Lilia mama yako? Unajua nilichofanya? Bila kusita, nilipoona simba ananirukia aniue, nikamuwahi na kuanza kumpangua na kumpasua. Ungeweza kusikia mifupa ikivunjika, nyama ikichanika, na punde, simba alikuwa pembeni mwa barabara....akiwa vipande viwili. Mimi mwenyewe nilibaki mdomo wazi nikishangaa kazi ya mikono yangu. Na ule mzoga ulipokoma kuhangaika na kuacha kutetemeka, sikukaa nifikiri kwa nini simba anivamie, ametumwa na Mungu kunizuia nisiendelee mbele na safari yangu? Nilipotazama mzoni nilijua mimi ni mwanamume mwenye nguvu kupita wote.

Mimi na Kahaba wa Gaza

Bado huna hakika kuwa mimi ni mwanamume mwenye nguvu aliyewahi kuishi? Unahitaji ushahidi zaidi? Nitakupatia hadithi nyingine. Siku moja niliamua kwenda Gaza, mji wa kifilisti pembezoni mwa bahari (Wa 16:1-3). Nilikuwa natafuta kisura wa kujifurahisha naye. Nikajibadili kimwonekano nisijulikane na kujichanganya na watu waliojaa mtaani. Nilipokuwa nimejipumzisha kwenye kona fulani, nilimwona mwanamke wa usiku. Nilipendezwa kumtazama, nikalipa fedha na kulala naye. Katikati ya usiku nilipomaliza, nikajiandaa kuondoka. Lakini nikaona watu wa Gaza walikwisha nishtukia na kunigundua.  Na waliamini wamenipata. Niko ndani ya mji wao. Gaza kama miji mingine ya kifilisti ulikuwa umezungushiwa kuta ndefu, hata huwezi kurusha jiwe juu yake, pana kuruhusu gari linalokokotwa na farasi lipite. Kuta zao za mawe zilikuwa imara vya kutosha kumzuilia adui nje. Lango la mji lilitengenezwa na mti mgumu, unene wake futi 6, likining’nizwa na mawabu za shaba, kwenye fremu ya mlango wa futi 10 mpaka 15. Kama hiyo haitoshi geti la mji wao liliongezewa boriti za shaba juu yake kulifanya imara zaidi siku walipohisi hatari. Lango lilikuwa zito kweli kweli. Hakuna ambaye angeweza kutoka mjini mlango unapofungwa. Na wafilisti walijua nimepatikana.
Nilipoziona nyuso zao na kusikia wanavyonong’onezana nilihisi wanasema, “Tumempata, hatimaye Samsoni ni wetu”. Nilipogeuka na kuona kango zito limefungwa namna ile mpango wao ulikuwa wazi kwangu. Walitaka kuninasa kama panya kwenye mtego. Sijui ungefanyaje ungekuwa katika hali hiyo. Kujaribu kujificha labda? Toboa ukuta? Hiyo haikuwa staili yangu. Huyo sio Samson. Sikutetemeka katika hofu. Nilitembea wima, kifua mbele katikati ya mji mpaka nikafika langoni mwa mji. Nikatazama huku na huko kuona kama kuna yoyote yupo jirani ashuhudie mimi ni nani. Nilitema mate mikononi, nikainama chini, nikakamata boriti lililokuwa likikazia mrango ufunge. Nashukuru bori hilo liliwekwa pale chini. Nikapata pa kushikia. Kisha nikaanza kuvuta.....zaidi na zaidi. Nilipovuta nikaanza kusikia joto joto la Roho wa Mungu limeanza kusambaa mwili mzima. Nilipozidi kuvuta zaidi na zaidi joto la kiungu likazidi kukolea. Nikaanza kuona nyufa, kusikia mbao zikilalamika (kakak..kaka..) na mwishoni lango lilinyofoka na nikalimwaga chini. Mtu wa kawaida baada ya shughuli iliyofanyika angeuacha mlango hapo na kuondoka zake. Lakini niliona sitakuwa nimewapatia wafilisti wasiotahiliwa somo la kutosha. Kwa hiyo nikalinyanyua geti mabegani mwangu na mpaka umbali wa maili 28 juu ya kilele cha kilima na kuliacha hapo. Wangehitaji timu ya majeshi kuurudisha mlango getini. Isingefaa nikimbie mji wao salama. Nilitaka wasumbuke. Mimi ni mwanamume mwenye nguvu aliyewahi kuishi. Hakuna swali. Hakuna upinzani.

Niliporudi tena Timna

Aha! Mnakumbuka niliwaambia kuhusu safari yangu ya Timna kwa ajili ya maandalizi ya arusi yangu? Kweli taratibu za uchumba zilikwisha, uchumba wetu ulikubarika na wazazi wa pande mbili. Lakini mambo yalikuwa bado hayako sawa. Arusi inakaribia. Ikanibidi nisafiri tena. Nyumbani mpaka Timna si karibu. Nilipokuwa safarini, tumbo langu likinikata kwa njaa. Hatimaye, nikafika sehemu ya barabara nilipomrarua mfalme wa pori. Nikaamua kutazama uharibifu nilioufanya, nikachungulia mzoga. Haa kuna asali! Nilichokiona mimi ni chakula kutuliza njaa yangu. Bila kujali kama kuna nyuki au kwamba Mungu alinikataza nisiguse maiti, nikatuma mkono ndani ya mzoga na kujizolea asali. Nikasubiri nione kama Mungu atatuma malaika mwenye upanga anikate shingo kwa kuwa nimevunja kiapo kwa kugusa mzoga, sikuona. Nisubiri nione ardhi ikifunguka kwa tetemeko na kunimeza, kimya. Labda wazazi wangu hawakuwa sahii waliponiambia Mungu hataki mimi nishike kitu najisi kama: mbona sijadhurika? Nikawagawia wazazi wangu bila kuwaambia nimeitoa wapi, nami nikaanza kuila asali huku ikitapakaa mdomoni na kinitiririka mikononi. Nakwambia, hakuna siku asali ilikuwa tamu kama siku ile!
Niliendelea mbele mpaka nikafika Timna, maandalizi ya arusi yakaisha na arusi ya kufana ikafanyika. Arusini wafilisti walikuwa wananishangaa-shangaa wakinichungulia bila kuamini macho yao. Wakijiuliza, hivi Samson ni mwanamume wa kawaida au wa kimiujiza. Unajua nilivyokua nikijisikia. Nikataka kuwaonesha kuwa mimi ni mwanamume.Nikaagiza bia ya Kifilisti. Kwani bia moja inashida gani? Mwanaume, nikainywa na chupa kuiweka chini. Na hapo nikajua nimevunja kiapo cha pili kama mnadhiri wa Mungu. Nikasubiri nione hasira ya Mungu ikiniwakia na radi toka mbinguni ikiniangukia. Dhambi yangu ina matokeo gani? Sikuwahi kufikiria swali hili kwa mda mrefu namna hii. Sikua naogopa, lakini nilitamani kujua Mungu atanifanya nini? Na unajua alinifanyaje? Hakuna! Hakuna lolote! Nikaanza kufikiri hii habari ya dhambi inaua ni maongezi tu. Mbona nimevunja viapo vyangu viwili na hakuna kilichonitokea. 
Maisha yakaendelea. Lakini si na mwanamke niliyemuoa. Ndoa ile haikuendelea. Hiyo nayo ni hadithi ndefu. Lakini niliwatia adabu wafilisti kwa kunivunjia ndoa yangu.  Niliwaua wafilisti wengi tu. Nani mwanamume kama mimi?

 

Nilipompata Delila

Na maisha yakaendele, nikiwa sina mwanamke wa kudumu. Ndipo siku moja nikadhani nimepata jibu la maombi yangu. Nilikutana na mwanamke wa moyo ndoto zangu. Alikuwa na nywele ndefu, ngozi nyeupe, na macho yake yangekumaliza. Kila nguo inamkaa! Huyu ndiye mwanamke! Jina lake aliitwa.....Delila. Alikua ameumbika; alikuwa na kila kitu cha kumfurahisha mwanamume. Huwezi kuhitaji mwingine. Isipokuwa kwa kitu kimoja.....alikuwa mzuri lakini....alikuwa akitaka kitu chake lazima akipate. Anaweza kukiomba kwa kurudia rudia mpaka akipate. Na sasa alitaka kujua siri za nguvu zangu. Alikuwa anaweza kusema, “Samson kama unanipenda niambie asili ya nguvu zako.” Alisema huku akilegeza macho yake, na akizilaza nywele zake mara huku mara huku. Na akanimaliza.
Samsoni akiwa amesalitiwa
Mara kadhaa alinibembeleza nimwambie, na mara zote nilimwambia kidogo tu na sikumwambia ukweli wote. Lakini Delilah hakukata tamaa. Hata hivyo, unajua, alikuwa ameahidiwa na maafisa wa usalama wa taifa furushi la hela kama ataipata siri. Pesa nyingi kama jumla ya mishahara ya mfanyakazi kwa maisha yake yote. Akijua hilo ndivyo alivyozidi kunisihi akisema, “Wasemaje nakupenda; na moyo wako hauko pamoja nami? “ (16:13). Mwishowe nikamwambia Delila nadhiri moja ambayo sikuwa nimeivunja. Nilimwambia kuwa sijawahi kukata nywele zangu. Nilivyomwangalia machoni, nilijua ninaweza kumuamini. Usiku ule, niliishia usingizini na kichwa changu mapajani mwake. Nilimtumainia maisha yangu, lakini alinisaliti. Nilipokua nimelala, kumbe akamleta mtu kunikata nywele zangu. Mimi sina habari. Kisha akaniita, “Samsoni, Wafilisti wanakujia!” (16:20). Nikaamka mwanamume kama nilivyozoea kuamka. Nikasema mbona hawa Wafilisti hawaelewi somo, hebu niwaoneshe mara nyingine tena kuwa mimi ni mwanamume mwenye nguvu aliyewahi kuwepo. Nikajaribu kujinyoosha, lakini sipati nguvu. Uchovu niliolala nao upo pale pale. Wafilisti wakaja, wakanikamata, na kuninyang’anya nguvu zangu na uanaume wangu.

 

Majuto Kitanzini

Samsoni Kitanzini
Ndugu zangu hebu niwaambie: mimi sikuwa hivi. Wameninyoa nywele zangu zote, siwezi kutamba tena. Wamening’oa macho yangu, siwezi kuona tena. Wamenifunga, siko huru tena .

 

Nimeingiaje kwenye shimo hili?

Laiti kama ningewasikiliza wazazi wangu nisingekuwa hapa. Nakumbuka wazazi wangu walivyokua wakiniambia na nilivyokua nikiwajibu:
  •  “Samsoni, usisahau, ukashika chochote kilicho kichafu. Samsoni usikaribie huko. Hutakiwi kugusa mizoga.”  “Najua mama, najua." Niliwajibu, "Umekwisha niambia mara mia kidogo.”
  •  “Samson, usiende huko. Huko ndiko vinyaji vyote vinapatikana. Vinywaji vyote vilivyochachushwa. Kileo chochote kisipite mdomoni mwako. Wewe ni Mndadhiri. Usikariebie huko.”
  • Baba yangu aliniambia, “Samson, kumbuka, usikate nywele zako.” “Ninajua, baba. Hiyo ni ishara kwamba mimi ni mnadhiri na kila mmoja anitambue kuwa mimi si wa kawaida.”
Ninakiri tatizo langu halikuwa kwamba sikuambiwa. Laiti kama ningewasikiliza wazazi wangu nisingekuwa hapa.

Nimeingiaje kwenye shimo hili?

Sasa ninajua tamaa ya mwili inaweza kuwa imetulia, lakini haifi kamwe. Makaa ya moto yanaweza kuwa yamebakia chini ya majivu ukadhani yamezima, lakini yakipulizwa na upepo, yanaweza kuwasha msitu mzima. Na matokeo yake mtu anaweza kuunguzwa. Na ndiyo yaliyonipata.
Nilipokua na kahaba, nilijifikiria, “Nikijiridhisha naye mara hii ya mwisho, itakua basi.” Lakini unajua dhambi moja inaita nyingine. Nilikua ninapanda pengu ambayo ilikua izae matunda yake baadaye. Nilianza kumkubalie Delila kunishika-shika. Sikuyakimbia majaribu; nilibakia ndani ya mipaka yake. Unaweza kudhani nimezidisha, lakini nadhani ingekua bora kama Wafilisti wangenifanya kipofu nikiwa bado mdogo. Ingenisaidia nisijiingize kwenye mapenzi haramu. Delila inamaanisha “mtu aliye dhaifu” au “mtu aliye na shauku.” Nilikua mwanamume mwenye nguvu kupita wote, na sikudhohofishwa na maaskari au majeshi, lakini na mwanamke. Mimi, Samsoni mwenye nguvu sikuweza kujiponya toka mikononi mwa Delila, “mtu aliye dhaifu.”

Siulizi tena nimeingiaje kwenye shimo hili.

Samsoni awaua Wafilisti
Ninajua ni makosa yangu. Sio kosa la Delila, japo kwa muda mrefu nilimlaumu sana. Sio kosa la Delila, wala vaa yake, wala macho yake au mabembelezi yake. Kosa ni langu: ningewasikiliza wazazi wangu nisingekua hapa. Kweli, hapa nilipo, sina nywele na sina macho. Lakini namshukuru Mungu. Siwezi kunywa sumu. Baada ya kutolewa macho, sasa naweza kuona. Na sasa kwa mara ya kwanza nimeweza kutubu na kuabudu na kuhutubu. Japo wafilisti bado wamenifunga mwili wangu kwa minyororo, lakini Mungu ashukuriwe, roho yangu iko huru. Wafilisti wamenifunga kama mbwa kibandani na kumtukana Mungu wangu. Lakini, ninaomba Mungu adhihirishe nguvu zake kupitia udhaifu wangu, aoneshe wema wake kupitia ubaya wangu. Ninamshukuru niko hapa ili nikuambie uhitaji kua hapa, na kama upo hapa tayari usife moyo Mungu hutoa nafasi ya pili tutazame makosa yetu ili tuyajutia na kuyaacha.
(Hubiri lililotolewa na Pr Enos Mwakalindile 13 April, 2013 Donge SDA church, Tanga) 

11/04/2013

NAMNA YA KUMSAIDIA MTOTO KUJENGA HAMU YA KUJISOMEA



uTANGULIZI

Kumsaidia mtoto kupenda kusoma ni zawadi kubwa unaweza kumpatia mwanao maishani. Watoto waliozoweshwa kusoma nyumbani (sio kufanya homework ya shule tuu) wameonekana kuwa na mafanikio makubwa kimasomo shuleni kuliko wale ambao hawasomi. Mtoto anaweza kunufaika kwa yafuatayo anapopenda kujisomea vitabu mbalimbali, magazeti, n.k.:

  • ·        anajiongezea maarifa,  
  • ·        anakuza fikra au mawazo yake
  • ·        anapanua upeo wake wa kuona na kuyanyambulisha mambo.
  • ·        zaidi anajiongezea kujiamini.


ZIFUATAZO NI mbinu CHACHE UNAWEZA KUTUMIA:  


1.     Waruhusu watoto waone mfano kwako. Hebu wakuone ukisoma biblia, kitabu, gazeti, novels, n.k..

2.     Ongea nao kuhusu vitabu ambavyo umekuwa ukisoma. Wasimulie jinsi ulivyonufaika navyo.

3.     Soma na watoto wako kila siku na muda maalum ambapo televishen imezimwa na mambo mengine yamesitishwa.  Kabla hawajalala wasomee kitabu. nenda nao chumbani na ingia kitandani nao au kaa kwenye kiti uwasomee somo fulani au hadithi.
     Waruhusu pia kuuliza maswali na wewe pia upate nafasi ya kuuliza maswali. Kwa kuongelea yale tusomayo pamoja inasisitizia kwenye bongo zetu yale tusomayo. Na zaidi inafanya mda ule kuwa wenye mvuto. Mwanao akiuliza swali la udadisi unaweza lingine ukampa nafasi ya kulifuatilia zaidi na atakapopata fumbuzi la swali lake atazidi kutambua umuhimu wa kujisomea.                                                                     Ibada za kila siku ni za msingi sana kwa watoto lakini pia kusoma nao aina nyingine za vitabu kutawanufaisha zaidi watoto wetu.

4.     Tayarisha notes fupifupi uwapatie wazisome, mfano hadithi za biblia, jinsi na umuhimu wa kutunza afya zetu, habari za watu maarufu, waliofanikiwa maishani, siasa, historia, n.k..

5.     Tafuta kufahamu nini mtoto anapenda, kama ni kupika mtafutie vitabu vya mapishi, kama ni wanyama basi vitabu vinavyohusu wanyama, kama michezo basi gazeti au vitabu kuhusu michezo mbalimbali n.k. mweleze jinsi hivyo vitabu vitakavyo mpatia ufahamu au ujuzi zaidi wa hicho kitu anachokipenda.

6.     Mfundishe tofauti za usomaji. Kusoma kutafuta kujua jambo fulani, kusoma kuelewa zaidi jambo fulani, na kusoma kwa kujiburudisha. Kuna habari nyingi na za kila aina, upatikanaji wake ni rahisi zaidi na popote mfano tovuti (internet) kwa computer au hata kwa simu n.k..  Hivyo basi ni muhimu kumfundisha mwanao namna ya kuchuja habari zenye manufaa kwake na habari zisizo na manufaa kwake, zenye kujenga na zenye kuharibu. 

7.     Mpongeze mwanao kwa kusoma. Kama kunajambo zuri amefanya na unatamani kumpatia zawadi, kwenda kwenye duka la vitabu na kumpatia nafasi ya kutafuta kitabu anachopenda, hii inaweza kuwa zawadi nzuri.


MWISHO

Kumbuka kwamba muda huu ni wa pekee kwako na wanao kujenga mahusiano. Baada ya siku ya maangaiko na shughuli nyingi hatimaye watoto wanapata nafasi ya utulivu na wewe.  Kwa hiyo fanya muda huu uwe wa kufurahisha na kuburudisha.

Imeandaliwa na:  Aika Mwakalindile


08/04/2013

Mtambue, Jitambue, Watambue: Namna Yesu Anavyolitazama Kanisa (Mathayo 16:13-19)


(Hubiri nililolitoa sabato ya tarehe 6 Aprili, 2013, kanisa la SDA Magomeni-Tanga)

 

0. Utangulizi

“Unalionaje Kanisa lako?” Swali hili moja lakini laweza kuamsha majibu mengi. Watu wana mitazamo tofauti tofauti juu ya kanisa. Kwa macho ya mwingine kanisa ni kama “kimbilio la wanyonge,” huku kwa mwingine ni kama “nyumba iliyohamwa siku nyingi.” Kwa mwingine kanisa ni kama “mgodi wenye utajiri wa milele,” huku kwa mwingine  ni kama “shimo la mapokeo ya zamani.”  Kwa huyu KKKT ndilo kanisa, na kwa yule SDA ndilo kanisa. Kanisa linaweza kuonekana vizuri kwa macho ya mmoja na kwa mwingine likaoneka vibaya. Uzuri wa kitu upo katika macho ya mwonaji.

Lakini uzuri wa macho wa kitu sio lazima ufanane na ubora wake katika uhalisia wake. Ndio maana mwanamke niliyemwona mrembo jana leo ninamwona wa kawaida tu. Na kanisa nililoliona limejaa ngano jana, leo naliona limesheheni magugu. Macho yetu yanacheza-cheza, na hisia zetu huhamisha hamisha mitazamo yetu kama mawingu ya angani yanavyosukumwa sukumwa na upepo. Kama mtu anakuuliza unalitazamaje kanisa bora umwambie ukweli. Mwambie siwezi kukupatia kielelezo kinachofanana na kanisa uso kwa uso, isipokuwa picha yake niliyoichora mimi akilini mwangu. 

Tena mwambie asipoteze muda wake na muda wako na swali lake.  Mwambie, yupo wa kumuuliza, yaani Mungu. Mungu ndiye mwenye kanisa na analitazama ndani na nje, juu na chini. Mungu pekee analitazama kanisa katika uzuri wake na ubaya wake—hakuna kinachoweza kutoroka macho ya Mungu; maana, macho yake  yanawaka kama tochi. Ni Mungu pekee ndiye anayelitambua kanisa katika uhalisia wake.

Na hapo natamani kujua: hivi Mungu analitazamaje kanisa? Japo swali hili nauliza leo, lakini jibu lake lilitolewa zamani kama injili ya Mathayo ilivyoandikwa zamani. Katika injili ya Mathayo 16 Yesu anauliza mitazamo ya watu kwanza kumhusu Yeye. “Watu hunena Mwana wa Adamu kuwa nani?” (fungu 13). Hivi watu wananionaje? Kwa kuuliza swali hili, Yesu hakuwa anatafuta utambulisho wake, kana kwamba hajifahamu. Hapa Yesu alitaka kujua maono yao juu yake, ili awapatie maoni yake juu yao. 

Na Yesu akapewa majibu. Majibu yao yalikuwa tofauti-tofauti kulingana na maoni yao yalivyokuwa yametofautiana. Kulikuwa na hao waliosema Yesu ni Yohana Mbatizaji; wengine walisema Yesu ni Eliya; Yesu ni Yeremia; Yesu ni mmojawapo wa manabii. Bila shaka Yesu alihuzunishwa na majibu yao. Kwa sababu Yesu alikuwa zaidi ya Yohana Mbatizaji, Eliya, Yeremia, au nabii. Yesu aliona jinsi watu walivyochagua kumchora mawazoni mwao kama walivyopenda na si kumtazama kama alivyojitambulisha kwao. 

Ndipo Yesu akawageukia wanafunzi wake na kutaka kujua wanamtambuaje. Tusubiri tuone. Je, wanafunzi watafumbia macho uungu wa Yesu na kuyakazia tu kwa ubinadamu wake? Je, wanafunzi waliokuwa na nafasi ya kumtambua Yesu kwa miaka mitatu hivi watamwona tu kama mmoja wa wacha Mungu wa zamani? Yesu alikuwa ana hamu kujua wanafunzi wake wamechagua kumtambuaje. 

Bahati nzuri Petro akatoa jibu lililotuliza moyo wa Yesu. Petro akamwambia Yesu: “Wewe ndiwe Kristo (Masihi-Mkombozi aliyetumwa na Mungu) na Mwana wa Mungu aliye hai?” (Haleluya!). Na Yesu akampongeza haraka akimwambia, una bahati, huo sio mtazamo wa kibinadamu. Ninajua macho ya watu yanavyotazama; kwa vyoyote, “mwili na damu havikufunulia hili, bali baba yangu aliye mbinguni”(fungu la 18). 

Katika mazungumzo yaliyofuata; Yesu ni kama anasema, “kwa kuwa pamoja na ubinadamu wangu umekubali kuniona kama Masihi na Mwana wa Mungu, nami sasa nitakueleza ninavyokutazama wewe na wote wanaonikiri kama wewe. Niacheni sasa niwaambie ninyi ni nani.” Na hebu tuone Yesu anawatambuaje waumini wake?

1. Kanisa ni Kama Jengo lililosimama Mwambani

Kwanza kabisa ninamsikia Yesu anawatambua waumini wake kama  Jengo lililosimama Mwambani (angalia nami fungu la 18a): Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu. Ni mara mbili tu katika shuhuda za Injili zote nne[1] Yesu amekaririwa akitambua wafuasi wake kama kanisa (na kanisa likiwa na maana rahisi ya jamii ya watu wa Mungu). Na hii ni mara yake ya kwanza kufanya hivyo. 

Na ili tulielewe vizuri kanisa kama linavyoonekana mbele ya Yesu ni vizuri tutafute kuelewa ana maana gani anaposema, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu”? Yesu analilinganishaje kanisa kama Jengo juu ya mwamba? Na Petro anahusikaje hapo? Kuna uhusiano gani kati ya jamii ya waumini na  Petro na jengo na mwamba? Kwani Petro na jengo na mwamba vinawakilishaje kanisa? 

Tuanze na Petro. Hebu turudie kumsikia Yesu akimpongeza Petro kwa kumkiri ilivyo sahihi. Yesu anapompongeza anamwita kwa jina gani? Nasikia Yesu anamwita Petro kwa jina lake la zamani (jina alilopewa na wazazi wake)-Simoni Baryona. Na Yesu anapotaka kumhusisha na kanisa anatumia jina alilompatia kama mfuasi wake-Petro (Yoh 1:42). Simoni Baryona, kama yeye, hana uhusiano wowote na hicho ambacho Yesu anakwenda kukizingumzia kulihusu kanisa lake. Yesu anapomwita kwa jina Simoni mwana wa Yona, anaharakisha kumkumbusha kuwa yeye ni Petro. Petro ni jina la kiyunani (lunga ya waandishi wa Agano Jipya)  lenye kumaanisha “mwamba/ jiwe kubwa”. Lakini Petro na Yesu walizoelea kuzungumza lugha yao ya asili ya kiaramaki. Na jina la Petro kwa kiaramaki ni Kefa, likiwa na maana ile ile ya “mwamba”. Bila shaka kauli ya Yesu kwa Petro katika kiaramaki ilisikika hivi: “Wewe ndiwe Kefa (mwamba) na juu ya kefa (mwamba) hili nitalijenga kanisa langu”. 

Kwa kauli hii, ni wazi kwamba Simon Baryona ni mwamba na juu yake Kanisa litajengwa. Lakini kauli hii inanifanya nisugue kichwa na kuuliza hivi, Simon Baryona kweli ni mwamba? Mbona muda mchache baadaye Yesu alimwita Simon Baryona “shetani”(Mathayo 16:23)? Inawezekanaje kanisa lisimame juu ya mwamba wa namna hii? Simon Baryona ni mwamba? Mbona wakati huo Yesu alimwambia Simon Shetani amewataka ninyi apate kuwapepeta kama vile ngano, lakini nimekuombea wewe ili imani yako isitindike [isipungue]?” (Luka 22:31,32). Inawezekanaje Simon kama kweli ni mwamba ahofiwe kurushwa-rushwa kama kijiwe kwenge ungo? Simoni Baryona ni mwamba? Mbona baadaye mwamba ulisogea dhoruba ya mateso ulipoipiga huko Gethsemani na katika nyua za Kuhani Mkuu? Ni mwamba gani unaoweza kusogea? Simon Baryona ni mwamba? Kanisa linawezaje kuwa imara kama litajengwa juu ya “kefa” hili na mwamba huu? Bwana unamwona sawa sawa Simon Baryona? Simon mwana wa Yona ana umwamba gani hata aweze kutoa usalama kwa kanisa litakalojengwa juu yake? 

“Tulia” namsikia Yesu akiniambia. Ni kweli Simon mwana wa Yona ni kama wana wengine waliozaliwa na wanadamu. Lakini hapa ninamwona kama nilivyompatia jina Mwamba alipochagua kuwa mfuasi wangu. Sasa hivi na hapa hapa Petro ameishi sawa sawa na jina lake. Ninyi ni mashahidi: wengi wamechagua kuyumbishwa na upepo wa maoni ya watu kunihusu mimi. Wengi wameniona kama Yohana Mbatizaji, Eliya, Yeremia, na kama nabii tuu. Lakini Petro amekataa kuyumbishwa na maoni ya wengi. Hapa Petro ameonesha ukefa au upetro au umbwamba. Petro ni muumini wa kwanza kunikiri mimi kama Mwana wa Mungu. Imani ya Petro kwangu kwangu ni msingi imara na salama ambao juu yake nitalijenga kanisa langu. Umwamba wa Mwamba (Petro) ni imani yake kwa mwana wa Adamu kama Mkombozi na Mwana wa Mungu.

Na hebu tuulize historia, Je Yesu alijenga kanisa lake juu ya mwamba wa imani ya Petro? Ni kweli:

  • Katika mathayo 16:16 tunamkuta Petro kama mwanafunzi wa kwanza kumkiri Yesu mbele ya wanafunzi wenzake kama Mkombozi aliyetumwa na Mwana wa Mungu kabla wanafunzi wengine hawajafanya hivyo.
  • Katika Matendo sura ya 2, tunamkuta tena Petro kama mhubiri wa kwanza kumkiri Yesu mbele ya wayahudi wenzake kama Masihi na Mwana wa Mungu kabla wahubiri wengine hawajafanya hivyo.
  • Na katika Matendo sura ya 10 tunamkuta Petro kama mhubri wa kwanza kumkiri Yesu mbele ya wamataifa kama Masihi na Mwana wa Mungu kabla wahubiri wengine hawajafanya hivyo.

Kwa kifupi historia takatifu inashuhudia kuwa kanisa limesimama juu ya imani aliyokiri Petro. Na imani hiyo ni imani kama historia ya Ukristo inavyodhihirisha. Miaka 2000 imekuja na kuondoka, mataifa yamekuja na kuondoka, lakini kanisa limeendelea kuwepo likikiri kwamba Yesu ni Mkombozi na Bwana. Na mpaka leo wakristo wapo na wataendelea kuwapo wanapoendelea kushiriki ungamo la Petro: Yesu ni Mkombozi wa Ulimwengu na Mwana wa Mungu.

Haikuwa rahisi mara zote kwa Petro kumkiri Yesu kama alivyo mbele ya watu waliokataa kumtambua Yesu. Petro alipigwa viboko, tupwa gerezani, na mwishoni kusulubiwa kama Bwana wake. Haijawa rahisi kwa waumini wa Kristo kushikilia imani yao huku wakikabiliwa na  vitisho na upanga na njaa na dhiki na adha na dhihaka. Lakini ni imani yao ndiyo iliyowafanya waendele kuwepo. Ni imani yao imara kama ilivyo ya Ki-Petro ndio iliyowafanya wasalie kama jengo lililojengwa mwambani. 

Na hakuna msingi imara mwingine tuliopewa kusimamia isipokuwa imani yetu kwa Yesu. Hatuwezi kubakia kama wafuasi wa Yesu kama tutasita kumtangaza Yesu kama Kristo na Mwana wa Mungu. Inawezekana kwa kumtangaza hivyo tutaonekana hatuvumilii dini za wengine au tunavuruga amani na utengamano katika jamii. Inawezekana kwa kumkiri Yesu tukaonekana wajinga wasiokwenda na wakati; kwa kuwa, wasomi na watu maarufu hawamwoni mwana wa Mariam kama Mwana wa Mungu, hawamwoni mwalimu wa Galilaya kama Mkombozi wa dunia yote. Inawezekana wengi wakataka kumwona  Yesu kama wanavyotaka kumwona; yaani, nabii tu, mwalimu tu, mponyaji tu, mshauri tu. Lakini sisi hatuwezi kukubaliana na mitazamo yao isiyotulia kama mchanga wa baharini na tukabakia wakristo shupavu. Inahitajika imani kali kumtangaza Yesu kama Mwokozi na Bwana ukiwapo nyumbani na kazini na mjini; na hiyo ndiyo imani  imara kama jengo mwambani. Bila kujali kisomo chao, makabila yao, au madhehebu yao, hakika waumini wasio na haya kumtangaza Yesu alivyo, ndio Kanisa litakalosalia kuwepo mpaka mwisho wa wakati.
Kanisa la Mungu ni Jengo linalosimama juu ya mwamba wa imani. Ndivyo linavyosimama mbele ya macho ya Yesu.

2. Kanisa ni kama Jeshi lililoko uwanja wa vita

Yesu aliposema atalijenga kanisa lake mwambani hakutaka tufikiri litakuwa salama mbali na hatari na ushindani. Maana, Yesu analitambua pia kanisa lake kama Jeshi lililo katika uwanja wa vita (angalia  Math 16:18b). Yesu anasema, “milango ya kuzimu haitalishinda [kanisa langu].” Kanisa ni kama Jeshi lililoko vitani likipambana. 

Lakini linashindana na nani? Yesu ameweka wazi, Kanisa linashindana na “milango ya kuzimu”. Na kuzimu haiwakilishi kitu kingine isipokuwa mauti na kifo (uf 1:18). Mahali pengine tunasoma kwamba dhambi huzaa mauti (Yakobo 1:15). Na kama dhambi huzaa mauti, basi kanisa linapambana na dhambi kama mzazi na mauti kama mtoto. Adui wa kanisa sio wewe sio mimi na wala si wao; adui wa kanisa sio wapagani, adui wa kanisa sio viongozi wake wala washiriki wake; isipokuwa tu kama ni vibaraka wa dhambi na mauti.

Kanisa liko vitani, na Yesu anataka tulitazame hivyo. Kanisa halijatulia na haliwezi kutulia. Mpaka limeondolewa uwanjani mwa vita, mbali na dhambi na kifo, kanisa haliwezi kutulia. Wale wanaolilia utulivu na amani watusubiri malangoni mwa Yerusalemu. Huko ndiko hakuna maombolezo wala kilio wala maumivu (ufu 21:4). Wale wanaolalamikia magugu yamezidi kanisani, au uovu umezidi kulinukisha kanisa, au siasa zimezidi kulichafua kanisa waliacha kanisa la Mungu. Wanyamaze wakisubiri siku ya hukumu ifike; siku ambayo wema na wabaya watatenganishwa milele na vita dhidi ya wema na uovu itamalizwa milele. Kabla ya hapo kila mmoja sharti aelewe Kanisa ni Jeshi lililoko vitani na hivyo ndivyo Yesu anavyoliona.

Wewe na mimi tuko vitani. Inawezekana tumemkimbia Yesu, tumemkana hadharani au sirini, hilo lisitukatishe tamaa. Tukumbuke  tuko vitani. Tunaweza kutetereka na kujeruhiwa, si neno, kwa  hatutaitupilia mbali imani yetu. Mapambano yanaweza kuwa makali na majeraha yakatuliza usiku na mchana, lakini hatutaachilia imani yetu kwa Yesu. Vidole vya wanaotushtumu na kutushtaki vinaweza kutusonda na kutukumbusha tulivyomkana Yesu, lakini hatutakata tamaa kutumaini wema wake kutusamehe na uweza wake kutusimamisha tena. Kama tutabakia uwanjani mwa vita na silaha ya imani yetu kwake ikisalia mikononi, hakika tutasonga mbele kwa ushindi hadi ushindi. 

Yesu amekwisha sema, “milango ya kuzimu” haitatushinda. Haleluya! Ijumaa adui anaweza kudhuru miili yetu, Ijumaa adui anaweza kukimbiza marafiki zetu mbali nasi, Ijumaa adui anaweza kutupiga mapigo, akanyanganya nguo zetu na heshima yetu. Lakini, bado ijumaa tunaweza kukabidhi roho zetu kwake Yeye awezaye kuzitunza. Kama jiwe la adui lilishindwa kumzuilia Yesu kaburini jumapili ile ya ufufuo, kadhalika hata sisi “milango ya kuzimu haitatushinda.”  

Kanisa ni imara kama Jengo mwambani na hodari kama Askari vitani. Na ninafurahi kuwa ndivyo Yesu anavyowatazama waumini wake.

3. Kanisa kama mlinzi wa malango ya Ufalme

Mwishoni, katika aya yetu Yesu anamalizia kulitambulisha kanisa kama Mlinzi wa malango ya ufalme (angalia nami fungu la 19): “Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni”. Kefa nitakupa  wewe funguo [ni wewe ukisimama pamoja na waumini wote watakao nikiri mimi}. Wewe ni mshika funguo, mlinzi katika malango ya ufalme. Unaweza kufunga na kufungua, kuruhusu na kuzuia, wewe ni mlinzi. 

Lakini Petro na wote wenye imani kama yeye ni walinzi wa namna gani mlangoni pa ufalme? Petro anaweza kufungulia au kuzuilia nini mlangoni mwa ufalme? Kabla hatujalielewa hilo: unakumbuka maneno ya Yesu kwa walimu wa dini katika Luka 11:52? Yesu alisema, “Ole wenu, enyi wana-sheria, kwa kuwa mmeuondoa ufunguo wa maarifa; wenyewe hamkuingia, na wale waliokuwa wakiingia mmewazuia.” Mahali pengine Yesu anawalaumu Mafarisayo (washika dini) kwa kosa hilo hilo (Math 23:13). Mara zote hizo funguo zinasimama badala ya maarifa na ujuzi waliopewa. Wana-sheria na Mafarisayo walikuwa na ujuzi wa maandiko ambao ungeweza kuwanufaisha wao na wengine. Lakini hawakutumia maarifa hayo ipasavyo.

Na kwa Petro na waumini wote, ujuzi na maarifa ya ufalme umetolewa.
Petro na waumini tumefunuliwa na Baba wa mbinguni kumwona Yesu kama Masihi na Mwana wa Mungu. Ufunuo huo ni ufunguo langoni mwa ufalme. Injili ya Yesu yaweza kuwafungulia malango ya ufalme wote wanaoipokea na kuwafungia malango hayo hayo wanapoikataa. Petro na sisi tumepewa funguo nyeti.

Na hivi Petro alizitumiaje funguo zake? Petro alizitumia funguo hizo mara nyingi:

  • Mara ya kwanza ni siku ya Pentekoste alipowaonesha wayahudi  kuwa Yesu ni Masihi na Mwana wa Mungu aliye hai. Akawaambia, “Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi” (Mdo 2:38). Na siku ile maelfu walifunguliwa malango ya ufalme.
  • Mara nyingine Petro alimfungulia malango ya ufalme, Kornelio na nyumba yake na wote wakaingia (Mdo 10).
  • Mara nyingine Petro  akiwa na Yohana alimfungulia kiwete malango ya ufalme naye akanyanyuka akiingia hekaluni akirukaruka kwa furaha.
  • Mara nyingine Petro na Yohana wakawafungulia wasamaria nao wakapokea Roho Mtakatifu.
  • Lakini mara nyingine Petro alimfungia Anania na Safira na hawakuingia katika ufalme.

Funguo alizopewa Petro ndizo tulizopewa. Tumepewa kuwafungulia watu wamjue Yesu kama Mkombozi nao wafunguliwe. Na kama kila mmoja wetu aliyepewa funguo hizi atazitumia wangapi wangepokea msamaha wa dhambi, wangapi wangefunguliwa na utumwa wa dhambi, wangapi wangepokea uponyaji. Wengi wamesimama langoni mwa ufalme wakisubiria mtu awafungulie. Watu hao wapo magerezani na hospitalini na kazini na manyumbani na kwenye facebook na kwenye youtube na kwenye simu. Wafungulie, waingie. Zitumie funguo zako za ufalme.

0. Mwisho

Sihitaji kuuliza tena unalionaje kanisa. Kristo mwenye kanisa amekwisha kulitambulisha kanisa lake. Yesu ametuambia kuwa kanisa lake ni kama Jengo mwambani, askari vitani, na mlinzi mlangoni. Yesu anakwambia unabakia salama unaponiamini, unapata ushindi unaponiamini, na uwasaidie wengine waniamini. 

Na Mungu akubariki unapomtambua Yesu kama alivyo, akubariki unapojitambua kama anavyokutambua, na akubari unaposaidia wengine wamtambue. Mtambue, jitambue, watambue.


[1] Ni katika Mathayo sura ya 16 na 18 tu Yesu amekaririwa akizungumzia wafuasi wake kama kanisa.