Yesu: Mkuu wa Nuru
Habari
Rafiki! Karibu kwenye mahojiano maalumu kati ya Yesu na Nikodemu. Awali ya
yote, hebu nikuombe ufunge macho. Sijasema tuombe. Umefunga? Unaona nini?... Giza?
Kadhalika
ukifungua tu injili ya Yohana utaona giza! Nalo giza ni nene na pana kiasi cha
kuikosesha dunia uhai. Katika msimu huu “haki[ja]fanyika chochote
kilichofanyika”. Dunia haina sura wala maumbile
isipokuwa utupu mweusi. Lakini Mungu hapendi giza litawale dunia.

Ni
bahati iliyoje kupokea nuru na kufanyika mtoto wa Mungu! Tofauti na mtoto wa
mtaani, mtoto wa nyumbani mwa Baba ana uhakika wa maisha, ana Yesu aliye nuru
na uzima. Na Yesu mwenyewe anaahidi wote wanaomwamini hawatatembea gizani kamwe
(8:12).
Nikodemu: Mtu wa Giza?
Baadaye
kidogo, katika sura ya tatu, Yohana anaripoti juu ya mtu aliyetembea gizani,
wakati wa usiku (2:2) kuja kukutana na Yesu aliye nuru ya ulimwengu. Japo
anatembea gizani Yohana anatufahamisha mtu huyu ni nani.
Yohana
anamtaja kwa jina la Nikodemu. Japo hatumfahamu kabisa, jina lake linaweza
kutufunulia tabia yake. Kwanza, japo ni myahudi lakini ana jina la kigiriki.
Tunajua kuwa katika karne hii ya kwanza kigiriki ni lugha ya kimataifa
inayotawala shughuli za kibiashara na kielimu. (Unajua tena hapa Palestina
wasomi na watu wanaoenda na wakati hujipa majina ya kigiriki). Huenda Nikodemu
ni myahudi “aliyefunguka”. Swali ni kama Nikodemu atakuwa tayari kufunguka
anapokutana na Yesu usiku huu.
Lakini
jina la Nikodemu linatuashiria kitu kingine kuhusiana na tabia ya mtembezi huyu
wa usiku. Jina lake katika ulimi wa kigiriki, Nikodemos, humaanisha, mshindi.
Kama Nikodemu ni mshindi nataka kujua
kama ni jasiri au mwoga. Huku kumwendea Yesu gizani ni dalili ya ujasiri au
uwoga?

Sasa
kama wazee wa Yerusalemu hawamwoni
mwalimu wa Galilaya kama masihi, iweje Nikodemu aende kinyume na maoni ya
wenzake? Hata kama ishara za Yesu hapa majuzi
ziliwafurahisha watu wengi wa mitaani hapa Yerusalemu, lakini maajabu
hayo yalikuwa bugdha na udhia kwa
viongozi wa jamii na serikali. Nikodemu atamwendeaje mtu aliyejichukulia
madaraka mkononi ya kufukuza wafanya biashara hekaluni hata kuwakoseshea
makuhani mapato (2:13-21)? Akimwendea Yesu makuhani-watawala watamwonaje?
Kufanya hivyo inahitajika kuwa na moyo wa simba.
Ingawa
Nikodemu hana ujasiri wa kumpongeza
mchana mvunjifu wa mfumo uliopo; moyoni anaona Yesu anastahili pongezi
na tena kusikilizwa kwa ukaribu. Ndipo Nikodemos, anashinda hofu ya kutengwa na
wenzake na kuchagua kumwendea Yesu. Potelea pote. Lakini anajaribu kuwa
mwangalifu—angalia muda gani anamwendea.
Ni
muda sasa umepita tangu jua lianguke magharibi. Nikodemu anaangalia huku na huku, anajifunika
weusi wa giza, na anashika njia, anapita mitaa miembamba ya Yerusalemu,
anakwenda, anakwenda. Anapita lango la mji, anakwenda, anakwenda aliko Yesu-Taa
. Hebu tumfuate nyuma yake ili tukamsikie Nikodemu, mgeni wa usiku, ana nini na
Yesu?
Giza na Nuru uso kwa uso
Sasa
Yesu amejipumzisha katika bustani moja, iliyoko pembezoni mwa kuta za
Yerusalemu na Nikodemu anaingia. Faragha ya Yesu na wanafunzi wake imeingiliwa.
Lakini, kwa upendo mgeni anapishwa kiti akae, tena haraka. Ni sawa mgeni apishwe haraka, kulingana na tamaduni zao. Si hata mwonekano
wake unafanana na hadhi aliyonayo—kilemba
kichwani, kazu ndefu, ndevu mpaka
kifuani! Wanafunzi wanamwachia nafasi akae.
Waangalie
wanafunzi wanavyoangaliana wanapompisha mgeni akae, wasikie wakiulizana: “iweje kiongozi wa
Yerusalemu amtafute mwalimu wetu usiku huu— wakati ambapo Yerusalemu haiko
tayari kumuamini masihi tokea Galilaya? Amekuja kwa lipi?” Hebu tubaki pamoja
na wanafunzi pembeni, tusikie Nikodemu anataka nini.
Nikodemu amgeukia Yesu: Sehemu ya I; Hongera mwalimu (fungu 2)
Akiwa
ameketi chini anatamtazama mwenyeji wake Yesu, mgeni Nikodemu anajaribu
kumfungulia zawadi mwenyeji wake. Anafungua kinywa chake na kumwagia Yesu
salamu za hongera. Msikie anavyoanza, "Rabi, tunajua kwamba wewe ni mwalimu
uliyetumwa na Mungu, maana hakuna mtu awezaye kufanya ishara unazozifanya Mungu
asipokuwa pamoja naye." (Yoh 3:2).
Kwa
macho ya paka, Yesu anamtazama Nikodemu machoni akimmwagia pongezi. Upesi, Yesu
anang’amua hitaji la mgeni wake. Analijua bila kuambiwa na wambeya au
wanahabari. Na ni siri iliyo wazi kwamba Yesu “aliwajua wote; ... [kwani] alijua yaliyomo ndani ya mwanadamu”
(2: 24-25). Hata moyo wa Nikodemu uko wazi mbele za Yesu kama kitabu
kilichofunguliwa.
Lakini
kwa kutokujua kuwa amesimama mbele ya Mjua Yote, Nikodemu amefanya kosa la ujuaji. Umemsikia amesemaje? Amesema
“tunajua.” “Mimi pamoja na wenzangu wa Yerusalemu tumeona mambo yako, na tunajua
wewe ni mwalimu wa viwango, rabi mwenye mhuri wa Mungu”. Nikodemu alidhania
amekuja kuitazama taa ya Galilaya, asijue kumbe ni Jua linalotazama watu.
Yesu amgeukia Nikodemu: Sehemu ya I; “Zaliwa Upya” (fungu 3)
Yesu
anamtazama Nikodemu na yuko tayari kumjibu. Kwa sifa zilizomwagwa, ningekuwa
mimi kwa lugha ya mama ningesema, ndaga
fijo. Lakini Yesu hadakii pongezi na uchombezi wa Nikodemu kwa ahsante. Kwa
Yesu sifa alizopewa ni kama mauwa yaliyonyauka na mapambo ya kukanyagwa.
Mwambie
Nikodemu ameanza vibaya na asirudie tena. Asijaribu tena kumpandisha mwalimu wa
Galilaya daraja mpaka usawa wa kimo chake kwa maneno yake matamu. Akifanya
hivyo asidhani anamtendea Yesu fadhila. Japo
Yesu atokea Galilaya ya wamataifa na yeye atokea Yerusalemu, ajue kwamba Yesu
ni wa viwango vya juu tayari, zaidi ya Yerusalemu
zaidi ya hekalu.
Yesu
hawezi kumshukuru Nikodemu kwa kumtambua kama mwalimu mwenye kazi
zinazoonekana. Kwani Yesu ni zaidi ya mwalimu mwenye muhuri wa Mungu au mtenda
miujiza ya kushangaza. Mwambie Nikodemu kuwa, Yesu ni Mungu-Mwalimu
aliyeshuka toka juu kumfunua Mungu kwa wanadamu (Angalia Yoh 1:18; 3:13).
Yesu ni mng’ao wa utukufu wa Mungu na chapa ya nafsi yake (Ebr 1:3). Yesu ni
“Nuru ya ulimwengu”! (8:12). Hivyo ndivyo Yesu alivyo; na anapendeza akisalia
hivyo. Haitaji make-up au sifa-bandia ili apendeze!
Kama
vile hajasikia hongera alizopewa, Yesu anamjibu Nikodemu akisema, “Amini, amini, nakuambia, Mtu
asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa mbinguni.” (3:3)
Nikodemu
elewa anayeongea nawe sasa ni mfalme na sasa anaonge habari za ufalme wake.
Nakwambia, “hakuna mtu aliyepaa mbinguni, ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni,
yaani, Mwana wa Adamu” (3:13)[1].
Mwana wa Adamu ameupokea tayari ufalme toka kwa Mzee wa siku (kumbuka
alichokiona Danieli katika njozi za usiku. Daniel 7:13-14) na sasa ameshuka nao
mpaka hapa chini. Yeyote amwaminiye mwana ana uzima ana ufalme (Yoh 3:36; Kol
3:4). Tazama ishara anazotenda Yesu, humwoni hapa mtu mwenye mfano wa
mwanadamu, mfalme kweli kweli, tena aliye juu ya hekalu lote, na mamlaka zote,
na maumbile yote. Lakini pasipo kuzaliwa
mara ya pili, huwezi kuuona ufalme huu wa
mbinguni.”
Maneno
ya Yesu yanamwangukia Nikodemu kama radi
machoni na kumwacha kichwa-chini asijue aendeleze vipi mazungumzo. Anabaki
akitikisa kichwa na kujiuliza, “nimesikia sawa? Mimi Nikodemu nizaliwe anothen
ndio niuone ufalme wa mbinguni?”
Nikodemu amgeukia Yesu: Sehemu ya II; Inawezekanaje? (fungu 4)
Yesu
amemwambia Nikodemu “zaliwa anothen, ( ἄνωθεν ) ndipo
utauona ufalme” Ametumia neno la kigiriki anothen—neno lenye maana ya tena
au toka juu. Inaelekea Yesu ana maana zote mbili
anapomwambia anapaswa azaliwe anothen, yaani tena na tokea juu.
Lakini
Nikodemu akitikisa kichwa na kubabaika akili kwa mwangaza wa ukweli, akaona
aiache maana ya anothen kama
“kuzaliwa toka juu” na kudakia maana ya anothen
kama “kuzaliwa mara ya pili” kama kinga yake ya usoni nuru isimchome. Msikie anavyohoji,
“Awezaje mtu kuzaliwa akiwa mzee? Aweza
kuingia tumboni mwa mamaye mara ya pili akazaliwa?” (3:4).
Pole
Nikodemu, lakini huna sababu ya kutapa-tapa. Kwa nini ubabaike unapoambiwa uzaliwe
anothen? Ninaposema zaliwa anothen
yaani mara ya pili kwa vyovyote si maanishi urudi tumboni mwa mama yako. Kama
ningemaanisha hivyo mbona ingekuwa kazi bure. Maana siku zote zao na mbegu
hufanana na mtoto-nyoka na mama nyoka hufanana? Nikodemu hatakama ungeingia na
kutoka tumboni mwa mamayo mara saba ungebakia na asili hiyo hiyo kama ya
mamayo. Ninaposema zaliwa anothen sisemi rudi tumboni mwa mama yako urudi upya.
“Mwalimu
katika Israeli” kumbuka kuwa walimu hutumia lugha za ishara kuelezea uhalisia
wa kitu, na hapa ndicho ninachokifanya. Mbona wewe na wayahudi wenzako hutumia
lugha ya kuzaliwa anothen kuashiria kuwa wasio wayahudi wamebadilishwa kuwa wayahudi? Ni lipi gumu
hapa lisiloeleweka? (Angalia 3:12)
Hapana
hakuna gumu lolote isipokuwa mchezo wa mende. Hapa Nikodemu unakimbilia uvungu
wa zuria kuepa nuru inayokumumlika; unatafuta kujificha kwenye malumbano ya
hoja kuogopa kutazamana na ukweli unaomtazama. Hapa
unahoji uhalali wangu kukutaka wewe mzee wa kiyahudi ubadilike upya kama
mwongofu mpya wa uyahudi. Unadhani wasio wayahudi wana haja kuzaliwa anothen, lakini si wewe. Hauko tayari
ukweli huu ukutazame.
Yesu amgeukia Nikodemu: Sehemu ya II; Zaliwa kwa Roho (fungu 5-6)
Na
ukweli hauko tayari kumwachia Nikodemu ajifiche kwenye malumbano ya hoja, leo
amepatikana. Umebaki pale pale ukimmulika. Yesu, aliye kweli na uzima (1 Yoh
5:20), anamkazia macho Nikodemu na
kumwambia, “Mtu asipozaliwa kwa maji na
kwa Roho, hawezi kuingia ufalme wa Mungu.” (f.5).
Nikodemu
unahitaji kupokea macho mapya na moyo mpya kabla hujaweza kuuona ufalme
ulioshushwa na Mungu-Binadamu. Unahitaji mwanzo mpya, macho mapya, kabla hujaweza
kuuona utawala wa Mungu unaofunuliwa na Yesu Mgalilaya. Bila mabadiliko hayo utaishia
kuziona kazi zangu kama tu za nabii aliyejaliwa na Mungu (Yoh 3:2) na si za
Mungu aliyefanyika mwili (Yoh 1:14). Utakuwa na utakapopokea moyo safi na
tofauti maana utamwona Mungu ndani yangu (Math 5:8).
Nikodemu
hebu nikuambie,“Lile tulijualo twalinena, na lile tuliloliona twalishuhudia”
(Yoh 3:11). Na ninakushuhudia, “Kilichozaliwa
kwa mwili ni mwili” (f. 6a). Tunashuhudia katika mambo ya kidunia mtoto wa
nyoka ni nyoka na mtoto wa mwili ni mwili. Mtu wa mwilini amezaliwa gizani na hupenda
mama yake giza. “Nuru imekuja ulimwenguni na watu wakapenda giza kuliko
kuipenda nuru kwa sababu matendo yao yalikuwa maovu” (Yoh 3:19). Mtu wa gizani hupenda
kubakia gizani na hukaa mbali na nuru, akiogopa asije akakemewa na nuru akabadilika
(Yoh 3:19-21). Nashuhudia: Kilichozaliwa kwa mwili hupenda kusalia katika
mwili.
Hata
wewe mwenyewe Nikodemu unaelewa jinsi watu wanavyopenda giza na kukataa nuru. Juzi-juzi
nilifukuza wafanyabiasha hekaluni, nikawatoa nje kondoo na ng’ombe wao, nikapindua
meza na kumwaga chini fedha zao. Na unakumbuka jinsi tendo hilo
lilivyowakasirisha wakuu wa hekalu. Nikodemu nakushuhudia: mtu wa mwilini
hapendi mabadiliko ya kiroho; hapendi
kuona ufalme wa roho unatimua ufalme wa mwili. Nimekwambia, “kilichozaliwa kwa mwili ni mwili”.
Wewe
Nikodemu na wenzako kaeni mkijua tatizo lenu la kutokukubaliana na ufalme wangu
ni tatizo la mfumo mzima wa mwili. Tatizo limeanzia moyoni na kuenea mwili
mzima. Ni uovu toka utosini mpaka mguuni. Isaya alitabiri vema juu yenu. Ninyi [m]mekuwa
kama mtu aliye mchafu na matendo ye[nu] ta haki tamekuwa kama nguo iliyotiwa
unajisi” (Isaya 64:6a). Kama nikuanguka katika matope ya dhambi, mmeanguka, mkatenguka,
mkapinda, nakubakia mkiwa mmeinamia uovu. Lakini tumaini lingalipo. Ikiwa kama
wewe na wenzako uliowataja uliposema tunajua—wote
walioangukia Yerusalemu na Alekzandria na Washington na Tanga na Arusha watakuwa
safi tena basi wakaoge upya Yordani (haifai kunawa!) ikiwa watanyooshwa tena
basi wazaliwe upya (mazoezi na nidhamu pekee haifai!) ikiwa mtazaliwa upya
mtakuwa na asili tofauti kabisa; maana, “kilichozaliwa
kwa mwili ni mwili”.
Na kuzaliwa
upya ninakokuzungumzia kunawezekana, kunawezekana. Maana, “kilichozaliwa kwa Roho ni roho” (f. 6b).
Nikodemu, kaa ukijua kwamba ufalme wa Mungu ni wa kiroho (Mungu ni roho) na
wanaouingia ni wa kiroho. Watu wa rohoni hawazaliwi na mama zao wa mwilini isipokuwa
na Mama yao Roho Mtakatifu. Na kama mama yao alivyo ndivyo na wanae walivyo. Ni
kwa uweza wa Roho tu, mtu aweza kuzaliwa katika ufalme wa Mungu.
Nikodemu
funguka: mbele yako ni yeye aliyetajwa na Yohana mbatizaji kuwa angebatiza watu
kwa Roho Mtakatifu(1:33). Nikodemu funguka: mruhusu Yesu akuzae kwa Roho.
Funguka na ugeuke na ulale sawa na njia na utoke upya. Funguka na uzaliwe upya kama
mtu wa rohoni! Na hapo ndipo utakapojua, kilichozaliwa
kwa Roho ni roho.
Unadhani
kuzaliwa kwa roho haiwezekani? Lipi gumu kwa Roho ambaye hapo mwanzo
alitulia juu ya uso wa maji akashiriki kujadili na kutekeleza ajenda ya uumbaji
hapo Mungu aliposema “natufanye mtu kwa
mfano wetu”? (mw 1:26)? Iweje Roho Muumbaji ashindwe kuumba upya watu wa
mwilini kuwa watu wa rohoni? Nikodemu, inawezekana kufanyika upya na kilichozaliwa kwa Roho ni roho.
Mpaka
hapo, Nikodemu amebaki kimya, mdomo wazi! Aseme nini. Akiri ameelewa, ameamini?
Sidhani kama yupo tayari kwa sasa. Na anamwongezea dozi kumwelezea mchakato wa
uzalishwaji wa Roho.
Nikodemu
Roho (kigiriki, Pneuma) anafanya kazi kama Upepo (ambao pia huitwa Pneuma). Pneuma (Upepo) ukivuma utauhisi machoni
unapokugusa, lakini hutauona. Pneuma ukipitia miti utaona matawi yakicheza,
lakini hutaona nyayo zake. Na vivyo hivyo Pneuma (Roho) akimzaa mtu huona Roho
anafanya-fanyaje, lakini utaona matokeo ya kazi zake. Utaona mtu amebadilika na
kuwa na nuru mpya ya Roho, mtazamo mpya
wa kiroho na mwelekeo mpya wa kiroho. (2:7-8). Na ndipo utaona nilichokuambia, kilichozaliwa kwa Roho ni roho.
Neno
hilo linaweza kutimia kwako Nikodemu. Roho akikuzaa upya: wewe mtu wa mwilini
utakuwa mtu wa rohoni; wewe mwoga wa macho ya watu utakuwa mwoga wa macho ya
Mungu; wewe shabiki wa dini utakuwa mwongofu wa imani; wewe mpenda ushabiki
utakuwa mpenda Neno; wewe mpenda ishara utakuwa mpenda Kristo. Ukimulikwa
hutajitetea ili ubakie gizani isipokuwa utajisalimisha ili uachane na giza. Amini
amini nakuambia Roho akikushukia Nikodemu utaona kwamba kilichozaliwa
kwa Roho ni roho na kilichozaliwa na mwili ni mwili.
Nikodemu amgeukia Yesu: Sehemu ya III; Inawezekanaje (fungu 9)
Hata
baada ya nuru hiyo badala ya kuukubali ukweli, cha ajabu, Nikodemu anatafuta tena
kujikinga kwa hoja nyingine ili nuru inayochoma isimuumize moyo. Msikie
anavyouliza, “Yawezaje kuwa mambo haya?”
(f. 9).
Yesu amgeukia Nikodemu: Sehemu ya III; Hufahamu kuwa hiyo ni kazi ya Roho? (fungu 10)
Hapo
hapo bila kumchelewesha Yesu anamuuliza, “Je!,
Wewe u mwalimu katika Israeli, na mambo haya huyafahamu!” (f. 10).
Safi!
Ni vizuri Yesu ampashe mvivu wa kufikiri kwa swali-motomoto. Kwa vyovyote
Nikodemu anafahamu kuzaliwa kwa Roho kunawezekanaje, ameambiwa tayari; iweje
aulize “Yawezaje kuwa mambo haya”.
Hilo ni swali la mchovu anayesinzia. Ni sawa aamshwe, apashwa, na afunguliwe
macho kwa ukweli unaowasha.
Yesu
anamtupia swali Nikodemu: Iweje mwalimu katika Israeli kama wewe usifahamu somo la msingi kwa mwanafunzi wa
awali wa imani (darasa la ubatizo)—somo la kuzaliwa upya? Kwa vyovyote
unafahamu mambo haya:
ü Ninajua Nikodemu umesoma
manabii kama Isaya (32:15-20) na Ezekieli (36:25-27) na Yoeli (2:28) waliotabiri
juu ya kipindi cha ukombozi. Umesoma habari za kipindi ambapo Roho wa Mungu anayebadilisha atamwagwa
kwa Israeli kama gharika juu ya ardhi kavu. Nikodemu
unafahamu mambo haya.
ü Nijuavyo Nikodemu unajua kuwa
Roho ambaye atakayemwagwa atafanya upya mioyo ya Waisraeli. Umekwisha soma aya
ya nabii Ezekieli isemayo, ”Nami nitawanyunyizia maji safi, nanyi mtakuwa safi;...nami nitawapa ninyi moyo mpya, nami nitatia roho mpya ndani yenu" Ezekieli (36:25-27). Nikodemu unafahamu mambo haya.
ü Nikodemu unajua kuwa ninapozungumzia
kuzaliwa kwa maji na kwa roho ninaashiria kipindi hicho cha mvua ya Roho kwa
taifa kavu, kipindi cha ukombozi na mabadiliko na uamusho—kipindi kilichoanza
kutimia tangu siku za Yohana Mbatizaji.
Kipindi cha ubatizo wa maji kama ishara ya kumgeukia Mungu na kufanywa upya.
Kipindi kinachokamilishwa na ujio wa masihi anayebatiza kwa Roho na moto. Nikodemu unafahamu mambo haya.
ü Nikodemu unajua kuwa ninapokwambia
unapaswa uzaliwe upya unaambiwa kipindi cha masihi ajaye kimefika; kwamba
ubatizo wa Roho na moto unapatikana; na kwamba mbele yako anasimama Mkombozi
aliyekuja kutekeleza hayo (Yoh 1:33). Nikodemu
unafahamu mambo haya.
Nikodemu
umefumbia macho ukweli na huhitaji ufafanuzi wa mambo haya. Funguka Nikodemu. Shida
yako Nikodemu ni shida ya wenzako wa Yerusalemu: hamwukubali ushuhuda wetu.
Sisi tuna hakika na tunachokishuhudia lakini ninyi mnatilia mashaka ushuhuda
wetu (3:11,12). Shida yenu ni kuona mashaka na kutoamini.

Giza au nuru: Chagua
Nikodemu
anaaga akiwa na moyo mzito. Anaondoka kimwili lakini akili yake iko kwenye
mahojiano yaliyoisha. Anajua hakuna mtu
anayenena kama Yesu. Aidha Yesu ni Mwalimu aliyeshuka au ni mwalimu
anayejinyanyua. Swali analobaki ni hili: afanyeje na madai ya Yesu Mgalilaya.
Amefika nyumbani na mzigo huo. Sijui amweleze
mkewe au afe nao kiume. Vyovyote, lakini Nikodemu anapaswa atue mzigo, na
kufanya maamuzi magumu. Ni juu yake kubakia amejifunika usiku unaomsitiri mpaka
sasa; au atupilie mbali blankenti leusi, anyanyuke na atembee akiifuata nuru
inayomwangazia? Nikodemu amenasa katikati
ya giza linalomhifadhi na nuru inayomchungulia. Nikodemu amebanwa. Mwombee Nikodemos-Mshindi
ashinde kiburi na woga, afanye uamuzi sahii.
Nikodemu na changamoto ya uamuzi kati ya nuru na giza
Rafiki,
tunapo muombea Nikodemu ni vizuri tutambue uzito wa utata ulioko mbele yake. Injili
ya Yesu inatofautiana kabisa na dini aliyoipokea toka kwa wazee wake. Kumbuka amefundishwa
dini ni kushika amri za Mungu. Anaelewa ushikaji amri ni mlango wa kumuingiza
mtu katika ufalme wa Mungu. Kama farisayo ameamini hilo kwa moyo wote, ametafuta
kulitekeleza kwa nguvu zote, na
kufundisha wengine kwa akili zote. Na kwa mafanikio hayo ya kidini Nikodemu
anajijua yeye ni myahudi kweli kweli, na ana tiketi ya kuingia katika ufalme wa
Mungu. Iweje Yesu amwambie ukitaka uingie katika ufalme uzaliwa upya, uniamini
mimi kama mkombozi aliyeshuka na utakuwa umeingia katika ufalme? Vipi mafanikio
yake kushika amri hayana mchango wowote kumuingiza katika ufalme? Kazi yake
yote ni bure? Aanze upya? Nikodemu ana uchaguzi mgumu wa kufanya: abakie na
dini yake au amchague Yesu. Si uamuzi rahisi..Muombee afanye uamuzi sahii.
ü Si rahisi kwa mtu aliyeirithi
imani toka kwa wazazi wake, akiamini dini yake inamfanya kuwa mtoto wa Mungu;
halafu aambiwe wewe si mwana wa ufalme na akubali kirahisi! Muombee.
ü Si rahisi mtu anayejiamini na
kuridhishwa na rekodi ya uaminifu wake kwa Mungu aambiwe rekodi yake ndefu
inamakosa tangia mwanzo, na akubali bila ubishi. Muombee.
ü Si rahisi mtu aliyezoea kutoa
zaka, kwenda kanisani, kukata nywele fupi, kuvaa nguo ndefu, kula mboga na
matunda, kuimba kwaya, kutoa matangazo, kuendesha ibaada, akijua kwa kufanya
hivyo anapata siti kwenye ufalme wa Mungu, halafu aambiwe hata hajakaribia
langoni mwa ufalme na akubali bila mashaka.
Muombee.
Na ukweli
ambao Nikodemu anapaswa aukubali ndio huu: Hakuna dini kama dini inayoweza
kumpaisha mtu mpaka mbingu ya tatu mpaka kwenye ufalme wa Mungu isipokuwa
Kristo pekee. Amini-usiamini, anayetafuta kupaa na kumfikia Mungu kwa kushika
dini au sheria kama farisayo Nikodemu wenzake walivyoamini (Gal 2:16; 3:10),
anajichosha bure. Akipaa sana ataishia kwenye usawa wa kimo chake-hapo uwezo
wake unapokomea. Hawezi kufika mbali. Kama mbingu zilivyo mbali na dunia ndivyo
atakavyoendelea kubakia chini mbali na ufalme.
Ni
Kristo pekee aliyeshuka ndiye anayeweza kumpandisha mtu mbingu. Yeye ndiye
ngazi ya Yakobo, hakuna nyingine. Ni Yesu-Mkombozi tu hakuna zidio au punguzo. Ni
kristo pekee na chochote kile kisitajwe. Kristo ndiye njia na uzima na ufalme. Kristo
atosha. Nikodemu amini Yesu atosha; na aseme Yesu atosha; na kila mmoja aseme
sasa: Yesu atosha!
Muumini na furaha ya Uchaguzi wa Nuru
kwa
habari ya Nikodemu hatujui (na bado tunaendelea kumuombea), lakini sisi
wanafunzi wake twasema Yesu atosha. Bwana asifiwe, tumemwona Yesu, tumeiona
nuru!
ü Tumeona wazi kuwa dini ya
kweli sio mwanadamu aliye chini kutaka kumfikia Mungu aliye juu; isipokuwa,
Mungu aliye juu kumfikia mwanadamu aliye chini kupitia Kristo pekee. Bwana
ashukuriwe, tumeiona nuru!
ü Halafu tumeona kumbe mwalimu
wa Galilaya ni mwana pekee atokaye kwa Baba Mungu amejaa neema na kweli, Yeye
ndiye ya mfalme na ufalme wenyewe (Yoh 1:14). Aliye na Mwana ana uzima na
ufalme! Haleluya, tumeona nuru!
ü Kisha tumeona ufalme wa Mungu
unaonekana popote mwana wake anapodhihirisha misuri yake ya kifalme kwa kuwahubiria
maskini habari njema, kufungua macho ya vipofu, kuwaachia huru wanaoonewa, na
kutangaza mwaka wa Bwana wa kufunguliwa-Jubilii (Luk 4:18; 7:22 linganisha na Yoh
2:23). Bwana ainuliwe, tumeiona nuru!
ü Tena tumeona hakuna dini au
elimu au uzoefu unamuingiza mtu katika ufalme wa Mungu isipokuwa uweza wa Mungu
mwenyewe. Tumeona mtu anapopokea uweza huo kwa imani ndipo anapokuwa mtoto wa
Roho na mwana wa ufalme. Hivyo mfalme wangu anenapo namsikia, akwendako
nakwenda, apendacho nakipenda, achukicho nakichukia. Kwani ninakuwa nimepokea roho mpya na mtizamo mpya na maisha mapya Bwana
ahimidiwe, tumeiona nuru, tumezaliwa upya!
Nasema tena, kwa habari ya Nikodemu hatujui anamwonaje Yesu
Mgalilaya, na hatuwezi kumsemea; lakini sisi waumini wake tunasema Yesu ni
habari njema ya ufalme!
Mwisho
Na
tunapomaliza tafakari ya mahojiano ya Yesu na Nikodemu, hebu tusifu pamoja na mtunga
zaburi (34:1-5):
“Nitamhimidi Bwana kila wakati/ sifa zake zi kinywani mwangu
daima.
Katika Bwana nafsi yangu itasifu,/ Wanyenyekevu wasikie wakafurahi.
Mtukuzeni Bwana pamoja nami/ Na tuliadhimishe jina lake
pamoja...
[Tu]kamwelekea macho [tu]katiwa nuru, wala nyuso [zetu]
hazitaona haya.”
Haleluya!
Hebu walioina nuru na waitikie, amina.
Ombi
Hebu
tuombe: Bwana Yesu, unyanyuliwe juu kwa kuwa wewe u mfalme wetu, na umeruhusu
nuru ya ufalme wako ituangazie. Miguuni pako, tunatupa taji zetu toka vichwani
mwetu. Kwa furaha pokea taji zetu. Ni wewe tu wastahili taji zote. Uzidi kung’aa na
kujulikana.
Lakini
Ikiwa Bwana kuna watu wa taifa lolote au taasisi yoyote au kamati yoyote, au
kwaya yoyote au chama chochote wananasita kukupigia goti wewe kama mfalme wa
wafalme, wahurumie maana wapo gizani. Bwana tunakuomba uwatamkie “iwe nuru” nao
watafunguka.
Na ikiwa,
Bwana, kama yupo hapa mtu anayelingia dini yake, tabia yake, wasifa wake, elimu
yake, mafanikio yake, kazi yake, au talanta yake, amuru sasa iwe nuru na
magamba macho pake yatadondoka, ili asijione bali akuone wewe tu.
Sasa
Bwana nakuomba umwage roho. Zalisha leo kwa Roho wako mwanamke huyu na mwanaume
yule katika ufalme wako. Kwa uweza wako fanikisha sasa kila goti kukunjwa kwa
Yesu, na kila ulimi kukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba. (Filipo 2:10). Amina.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni