30/05/2013

Mwanamume Huyu ni Nani? (Yoh 9)

Kabla ya Yote

Kati ya watu wote walioingia na kutoka katika jukwaa la historia, nani aliyegawa walimwengu kama mwanamume huyu? Alipotua tu juu ya uso wa sayari dunia, ripoti zinaonesha namna watu walitofautiana namna kumpokea. Mwandishi mmoja anasema wageni walisafiri umbali mrefu ili kumsujudia mtoto huyu wa kiume, huku wenyeji wakifanya mikutano mirefu ili kumuua. Mwingine anaandika kuwa alipokuwa angali mvulana mdogo, walimu wa dini waliinamisha masikio yao kumsikiliza, huku wazazi wake wakimnyoshe vidole kumgombeza. Na tena mwingine akaongeza kuwa alipotoa hotuba yake ya kwanza katika hadhara ya watu waliomfahamu tangu utoto wake, wasikilizaji walimsikia kwa furaha lakini muda mfupi baadaye waliziba masikio yao na kutaka kumfungia kufuli mdomo wake. Lakini ripoti inaendelea kuonesha mwanamume huyu aliendelea kuhutubia mikusanyiko midogo na mikubwa. Siku moja katika hotuba yake mwanamume alidai kuwa Yeye ni mkate ulioshuka toka mbinguni na wasikilizaji wake wanapaswa kumpokea nafsini kama chanzo pekee cha uhai.  Wachache waliweza kuyakubali madai hayo, lakini wafuasi wake wengi hawakuweza kumwelewa na walimwacha (Yoh 6:66). Viongozi wa dini na jamii waliposikia madai ya mwanaume huyu wakajaribu kutumia nyadhifa na nyenzo walizokuwa nazo kumdhibit mhubiri huyu asije akaligawa zaidi taifa. Viongozi wakatuma vyombo vya usalama kumkamata, laikini askari waliotumwa wakarudi na pingu tupu wakisema hatujawahi kusikia mwanamume anayenena kama mwanamume huyu  (7:32). Katika historia iliyoandikwa sijui mwanamume mwingine aliyewahi kuamsha hisia mchanganyiko kiasi hiki kama mwanamume huyu? Mtu huyo huyo akubaliwe na akataliwe, aheshimiwe na adharauliwe, apendwe na achukiwe?

Mwanamume huyo si mwingine ila Yesu wa Nazareti. Natamani kujua undani wa Yesu ili kubaini kwa nini watu watofautiane kumpokea kwa hisia zilizopishana kiasi hiki. Nitajaribu kurudi kwenye kurasa za historia na kufuatana naye anapopita katika barabara za vumbi za Palestina. Nitafuatana naye ili nisikie anasema nini na nimtazame anafanya nini huku nikifuatilia miitikio ya waliomshuhudia. Na ninaanza kukutana na Yesu kwenye injili ya Yohana sura ya tisa. Katika sura hii Yesu anafanya mambo ambayo hayajawahi kuonekana na anasema mambo ambayo hakuna mtu aliyewahi yasema.Mwanamume huyu nin nani?

Tukio A: “Nani katenda dhambi?”

Yesu anapita, anamwona kipofu. Wapo vipofu wengi hapa mjini Yerusalemu. Wengi wao ni upofu wanaupata ukubwani kwa sababu za uchafu, maji yenyewe hayawekwi dawa. Hapa kuna kipofu aliyezaliwa hivyo. Yesu anamwona kwa macho ya huruma. Lakini wanafunzi wanamwona kipofu huyu kwa macho ya udadisi. Wanafunzi wakimtazama kipofu huyu wakaona huo ndio wakati mwafaka wa kukata rufaa kwa Yesu kwa malumbano yaliyokuwa yakiendelea miongoni mwa wayahudi kuhusiana na uhusiano wa dhambi na ugonjwa. Wapo walioamini mtu anaweza kuumwa kwa sababu ametenda dhambi (wayahudi kwa ujumla wao waliamini afya ni baraka toka kwa Mungu na ugonjwa ni laana). Lakini kulikuwa na nadharia nyingine. Walimu wengine wa kiyahudi walifundisha hata kama mtu hajatenda dhambi maishani kabla ya kuumwa inawezekana alitenda kabla hajazaliwa (japo ilikuwa ngumu kuthibitisha hilo). Wapo wayahudi wengine walioamni mtu anaweza kuumwa kwa sababu wazazi wake walitenda dhambi (wakielewa yale maneno ya Torati kwamba Mungu huwapatiliza adhabu kwa maovu ya baba zao hata kizazi cha tatu na cha nne cha wamchukiao).  Sasa kichwani mwa wanafunzi , swali halikuwa, je dhambi inaleta magonjwa, isipokuwa je, mdhambi yupi kaleta upofu huu? Sikiliza swali lao kwa maneno yao, “Rabi ni yupi aliyetenda dhambi, mtu huyu au wazazi wake, hata azaliwe kipofu”?(fungu, 2).

Yesu anajibuje swali la wanafunzi? Kwanza, Yesu anakanusha nadharia zote zilizotolewa kwamba mgojwa mwenyewe au wazazi wake walitenda dhambi ndio maana akazaliwa kipofu. Magonjwa mengine hayasababishwi na dhambi tuliyotenda bali ni maumbili dhaifu tuliyorithi. Kuna wagonjwa wa ukimwi waliozaliwa nao au kuambukizwa na wenzi wao wa ndoa. Kuna magonjwa ya kurithi au kuletewa. Usimtazame kipofu wa kuzaliwa au ukoo wake kama wadhambi. Hilo Yesu aliliweka wazi kabisa.
Lakini utata unajitokeza katika maelezo ya Yesu yanayofuata ufafanuzi huo. Ni kama Yesu anasema,  amekuwa kipofu ili Mungu ajidhihirishe! Sawa Yesu, kweli Mungu ni Mwenye enzi yote na anastahili kujidhirisha kwa wote wenye mwili, wenye afya na wasio na afya. Lakini Bwana wa dunia yote hapaswi kuwa Mungu wa haki? Je, Mwenyezi Mungu ana haki ya kumfanya mtu kipofu ili aoneshe uwezo wake wa kuponya? Bwana hivi hapa hautuchanganyi? Kama Mungu ana haki kuharibu ili atengeneze, mbona sauti ya haki ndani yangu inabisha na mimi nimeumbwa kwa mfano wake? Lakini hivi Yesu aliwaambia wanafunzi Mungu amemfanya mtu huyo kipofu iliajioneshe? Au kwa kusema hivyo tunamuwekea Yesu maneno mdomoni? 

Inawezekana shida haipo kwa kauli ya Yesu yenyewe ila kwa kauli ya Yesu kama ilivyotafsiriwa. Tukisoma kauli ya Yesu kama Yohana alivyoandika katika kiyunani tunaona kauli ya Yesu inaweza kufasiriwa tofauti na ilivyo sasa na kutusababishia tumfikirie Mungu vibaya. Tuanze na mstari wa tatu wa sura hii ya tisa. Yesu asema, “Huyu hakutenda dhambi, wala wazazi wake” (weka nukta[.] hapa badala ya semi koloni[;]). Sehemu ya pili ya fungu la tatu inapaswa ianze na maneno, “Ili kwamba (neno la kigiriki hina ambalo linaweza kufasiriwa pia bali kama ilivyo kwenye tafsiri ya Union Version) kazi za Mungu zidhihirishwe ndani yake, imetupasa kuzifanya kazi zake yeye aliyenipeleka maadamu ni mchana, usiku waja asipoweza mtu kufanya kazi” (fungu 4). Hapa Yesu hakutoa tungo tata.

Kwa hiyo ni kama namsikia Yesu anawaambia wanafunzi wake; swala hapa sio nani katenda dhambi. Mimi ninapomtazama mgonjwa huyu ninaona fursa ya kazi. Nikitazama majeraha ya mtu simtazami kama polisi kutaka kujua ni nani aliyemsababishia nimtie nguvu. Mimi nikitazama udhaifu wako ninaona nimepata fursa ya kukuganga! Nimetumwa kama “Nuru ya Ulimwengu” (9: 5) Na ninakwenda kumtia nuru kipofu huyu. Ninajua kazi yangu itanitambulisha mimi ni nani japo utambulisho wangu unagawa watu. Ninajua sina muda, kama jua nimepewa masaa 12 tu kuangazia vipofu wapate kuona tena. Imenipasa kufanya kazi hii bila kujali matokeo. Ni lazima wajue mimi ni "Nuru ya Ulimwengu" (8:12).

Tukio B: Yesu akutana na kipofu mara ya kwanza

Alipokwisha kusema hayo Yesu akaendelea mbele na kazi yake. Kwa ujasiri mwingi na huruma tele akatema mate chini kutengeneza tope, akampaka kipofu mate usoni. Neno aliyekuwepo mwanzo wa uumbaji (Yoh 1:1-3) aliyetengeneza tope na kumuuba mtu wa kwanza (mwanzo 2:7), siye huyu amefanyika mwili na sasa anaumba tena? Wanafunzi wanaona hilo?  Yesu kwa kutema mate na kutengeneza tope ni kama anamkumbusha kila mtu kisa cha uumbaji na kuwaashiria kuwa yeye ni muumbaji na anaumba upya macho haya. Nani atamuona Yesu hivyo? Yesu akaendelea mbele kumtuma kipofu aende kunawa katika bwawa la Siloamu (maana yake, Aliyetumwa). Kipofu akakubali kufanya alichotumwa kukifanya, japo haikuwa rahisi kufanya hivyo. Kwanza mpaka hapo kipofu hajaahiwa kusikia vipofu wakinawa Siloamu wanapona. Pili vipi aibu ya kutembea na tope usoni? Tatu, kwa nini aende umbali huo mpak kisimani wakati angeyapata maji njiani kabla ya kufika huko? Mwanamume huyu anaagiza watu wafanye mambo ambayo hayaingii akilini. Lakini kipofu aliamini Yesu anaweza kuwa anania nzuri kwa kumpatia maagizo aina hiyo. Aliyaamini, aliyatii kwa kuende kunawa Siloamu. Na aliponawa, kipofu akarudi nyumbani anaona! Mara nyingi, maana ya maagizo ya Mwanamume huyu haionekani haraka akilini, lakini matokeo yake ni ya wazi machoni.

Tukio C: Majirani na Kipofu anayeona

Kipofu anayeona akarudi nyumbani na kuzua mshangao katika mitaa ya Yerusalemu—mitaa iliyojaa nyumba zilizobanana na majirani wanaofahamiana. Kundi la watu mtaani waliokuwa wakimfahamu kipofu kama omba-omba na kumsaidia njiani, walishtushwa kumuona  na kushindwa kukubaliana na ukweli uliokutana na macho yao. Wengine wakasema, “ndiye”; wengine, “siye ila anafananaye tu”! Kipofu mwenyewe akiingilia kati na kuzima malumbano kwa kusema, “ni mimi, ni mimi.” Watazamaji wakataka kujua alipataje kuona. Bila kumungunya maneno kipofu akajibu jinsi alivyoponywa: aliniwekea tope la mate machoni, akaniamuru niende kisimani kunawa, nikanawa na kurudi ninaona. Tangia hapo, hawakua na shaka kuwa ni yeye na aliponaje, lakini kilichowatatiza ni nani aliyeweza kufanya kitu hiki. Ni nani huyu aliyeweza kumponya kipofu tangu kuzaliwa? Ana mamlaka gani ya kuponya mlemavu wa aina hii, na amepata kibali cha nani kuponya siku ya Sabato, siku ya mapumziko, ambapo kazi yoyote ile hata ya uponyaji imepigwa marufu na viongozi wa dini?

Maswali hayo yalikuwa magumu mno kutatuliwa na wenyeji waliomfahamu kipofu huyu. Hivyo wakakata rufaa kuomba msaada kwa viongozi wa dini. Ninatamani kufuatilia viongozi wataamuaje kesi hii. Je, mtu aliyefanya uponyaji huu atakubalika kwa kazi nzuri aliyoifanya au atapingwa bila kujali kazi nzuri aliyoifanya?

Tukio D: Mafarisayo na Kipofu anayeona

Viongozi wa dini waliopelekewa kesi walijulikana kama mafarisayo, viongozi walioheshimika mbele ya jamii kwa uadilifu wao kwa katiba na sheria ya Israeli. Mafarisayo walimchukua aliyekuwa kipofu kwa mahujiano maalumu, kwanza wanataka kuhakiki kama ni kweli alitendewa muujiza:

Mafarisayo: Ulipataje kupona?
Aliyekuwa kipofu: Alinitia tope juu ya macho, nami nikanawa, na sasa naona.
Mpaka hapo mafarisayo wakaona shida katika maelezo ya kipofu aliyepokea uponyaji. Hawakuguswa kwamba kipofu omba-omba sasa ni mzima, ila walitatizwa na mamlaka ya mtu aliyefanya kitendo hiki. Wengine wakasema Yesu hakufanya uponyaji kwa ridhaa ya Mungu, maana haishiki Sabato. Wakadai Yesu si chochote isipokuwa mvunja-sheria. Lakini wengine wakakataa na kusema mtu hawezi kuwa mvunja-sheria na hapo hapo Mungu amwezeshe kufanya muujiza huu. Basi baraza likagawanyika pasipo maamuzi kuchukuliwa: Yesu ni nani? Ndipo mafarisayo wakamgeukia kipofu kutaka kujua maoni yake.
Mafarisayo: Unamaoni gani juu ya mtu huyo. Wewe unahusika zaidi kujibu swali hili, maana ni macho yako aliyoyafungua.
Kipofu: Ni nabii. Kichwani Kipofu haoni tofauti ya Yesu na nabii Elisha eliyefanya miujiza mingi kwa idhini ya Mungu?, Jibu lake: Yesu ni nabii

Mpaka hapo mafarisayo hawakuridhika. Hawakudhani kuwa Yesu anaweza kuwa kama manabii wa kale waliofanya miujiza ya kweli; maana kulikuwepo na wazushi enzi hizo, watenda miujiza bandia.

Tukio E: Mafarisayo na Wazazi wa Kipofu anayeona

Basi wakataka ushahidi wa kutoka kwa chanzo sahii cha habari—wazazi wa kipofu. Wazazi watasemaje? Sikia mahojiano yao:

Mafarisayo: Mnamtambua mtu huyu, ni mtoto wenu? Mnakubali alizaliwa kipofu? Kama ndio, alipataje kuona?
Wazazi wa Kipofu: Tunajua ni mwana wetu, kweli alizaliwa kipofu, lakini kwa habari ya alipataje kupona hatujui. Muulizeni mwenyewe, atajisemea mwenyewe maana ni mtu mzima.

Wazazi walijua hatari ya kutoa ushahidi utakaothibitisha mamlaka ya Yesu juu ya magonjwa na mapokeo yao ya utunzaji Sabato. Waliambiwa yeyote atakayemkiri Yesu kama masihi atatupwa nje ya jamii ya Wayahudi. Nani anapenda kufutwa ushirika?

Tukio F: Mafarisayo na Kipofu anayeona

Mafarisayo wakamgeukia kipofu, na kutaka kumbana amkiri akili mamlaka ya Yesu ili wapate kumuadhibu.

Mafarisayo: mpe Mung utukufu. Tunajua huyo si nabii kama ulivyosema, ila mwenye dhambi
Kipofu: ni mwenye dhambi mimi sijui. Najua neno moja tu, nalikuwa kipofu na sasa naona
Mafarisayo: Alikutendea nini mpaka ukapata kuona?
Kipofu: Niliwaambia hamkunisikia na sasa mnaniuliza tena? Mnataka kuwa wanafunzi wake?
(Kauli hii toka kwa aliyekuwa kipofu, asiye msomi ilikuwa ni kama matusi kwa mafarisayo wasomi. Wakakasirika)
Mafarisayo: Labda wewe ndiwe mwanafunzi wake, sisi ni wanafunzi wa Musa mtoa Sheria. Huyu jamaa yako hata hatujui alikotoka (wenzetu enzi hizo umashuhuru wa mtu unauhusiano na alikotoka)
Kipofu: Hii ni ajabu mtu mashuhuri aliyeweza kunifungua macho hamjui alikotoka? Tunajua Mungu hutumia watu wema kufanya mema. Haijawahi kusika mtu amemfumbua macho kipofu wa tangu kuzaliwa.  Kama huyu mtu asingelitoka kwa Mungu mwema, asingeweza kufanya wema huo?
Mafarisayo: Ama wewe mtoto wa laana! Ulizaliwa katika dhambi tupu na unajaribu kutufundisha sisi?
(Wakamtupa nje)

Tukio G: Yesu na Kipofu aliyeponywa

Yesu kusikia wamemtoa nje akamfuata na kuanza kuhojiana naye.

Yesu: Unamwamini mwana wa mwanadamu, mjumbe wa Mungu?
Aliyekuwa Kipofu:Ni nani nipate kumwamini?
Yesu: Umekwisha muona, na ndiye anayesema nawe sasa
Aliyekuwa Kipofu: Naamini Bwana. Akaanguka chini kumsujudia
Yesu: Nimekuja ulimwenguni kuhukumu; na hukumu yangu ndio hii: wasioona waone, wanaoona wasione.
Mafarsayo: Unamaana umetuhukumu sisi kuwa wasioona?
Yesu: Kama mngekuwa hamuoni nisingewahukumu mnaona, lakini sasa mnasema mnaona huku hamuoni hamuna hudhuru na hukumu yenu ipo pale pale.

Mwanamume Huyu ni Nani? Majibu Mbalimbali

Katika injili ya Yohana miujiza ya Yesu inajulikana kama ishara. Na muujiza wa kuponywa kipofu ulikusudiwa kuamuashiria Yesu ni nani? Lakini makundi mbalimbali yaliyokutana na Yesu katika yaliitikia utambulisho wake tofauti tofaut kulingana na sababu zao mbalimbali.

Majirani wa Kipofu: Hawana Hamu Kujua Yesu ni Nani

Kundi la kwanza la watu walioshuhudia kazi ya Yesu ya kuwatia nuru watu ni majirani na waliomfahamu kipofu hapo mtaani. Hawa walishuhudia mtu waliyekuwa wakimuona mtaani kwao na kila mara wakimsaidia kama omba-omba eti sasa anaona! Walishangaa sana wakiulizana ni kweli? Walipojua kuwa ni kweli, wakakimbia kuwapasha habari viongozi wao. Hawa wapenda-umbeya hawana kazi nyingine isiipokuwa kusimulia kipya walichokiona. Hawana muda wa kutafakari walichokiona. Wanawashwa kusikia muujiza mpya, hotuba mpya, muziki mpya, lakini hawana muda wa kutafakari walichosikia kinamfunuaje Yesu kwao. Watu wa namna hii kwa kwa kukosa hamu kumjua Yesu, wanabakia katika upofu wao. Hapana sisi si watu wa aina hiyo. Sisi huwa tunaimba huku tukiomba, “nataka nimjue Yesu na nizidi kumfahamu, nijue Pendo lake kuu wokovu wake kamili. Zaidi, zaidi zaidi...."

Mafarisayo na Viongozi wa Dini: Hawataki Kujua Yesu ni Nani

Kundi la pili la watu waliokutana na ushahidi wa Yesu kama Nuru ya ulimwengu ni mafarisayo na viongozi wa dini. Hawa hawakutaka kujua Yesu ni nani. Na wanasababu zao.

Kwanza kama viongozi, hawataki kujua wasije wakaonekana hawajui. Walijiona kama viongozi wasomi, wakijiita wanafunzi wa Musa. Na kama wasomi walidhani wanajua sana kiasi cha kutotegemea kufundishwa na mtu yeyote. Waliamini viongozi waliosoma vitabu  kama wao hawezi kufundishwa na mtu ambaye hakwenda shule. Eti usomi ni kutojifunza tena! Na hata kipofu alipowaambia mtu  aliyenifungua macho si mwingine isipokuwa nabii, mtu aliyetoka kwa Mungu, walimtusi yeye na wazazi wake kwa kebei na dharau! Hivyo walimu wa hawa wa dini wakakataa kufundishwa na mwanafunzi wao na wakabakia katika upumbavu wao, bila ya wao kutambua Yesu ni nani hasa.

Wafuasi wa Yesu sio kama mafarisayo na hawapaswi kuwa kama wao. Tofauti na mafarisayo wakristo tunajua Yesu ni nuru ya ulimwengu. Ulimwengu wote unaangazwa na jua hili moja. Tofauti na mafarisayo walioamini Musa ni wa Waisraeli, na hasa wao walioisoma sheria yake, sisi wakristo tunafahamu Yesu wetu ni nuru inayomtia nuru kila mtu, wanaoona na wasioona, viongozi kwa wafuasi, wasomi kwa wasio wasomi. Tofauti na mafarisayo, sisi tunaamini kila mtu ameumbwa katika sura ya Mungu na kila mtu anaangaziwa na utukufu wa Kristo.

Na siku inakuja, nayo imefika ambapo wakristo hawatatafuta kuwa walimu zaidi kuliko wanafunzi na waumini hawatakuwa wepesi kusema kuliko kusikia. Siku hiyo wanaoona watafunguliwa macho na wasioona, wasomi wataelimishwa na wasio na elimu, viongozi watawasikiliza wafuasi wao. Na siku hiyo wakristo kwa waislamu, wakaloliki kwa waprotestanti, watunza jumapili kwa watunza jumamosi watafurahia kuutazama utukufu wa Mungu unaoonekana katika kipaji cha uso cha mwenzake, kila mtu atafaidika na uzoefu wa imani ya mtu mwingine. Na siku hiyo Kristo atajulikana kweli kama nuru ya kila mtu.
Ninajua siku hiyo inakuja maana sisi sio mafarisayo ambao walikataa kumtambua Yesu ni nani wakidhani wanajua kila kitu na hakuna wa kuwaambia kitu.

Lakini kuna sababu nyingine iliyowafanya mafarisayo kutotaka kumtambua Yesu. Madai ya Yesu kama mkombozi aliyesubiriwa yalitofautiana kabisa na elimu yao. Walijua mkombozi ajaye atakuwa mtu mashuhuri, na watu mashuhuri walijulikana kwa sehemu mashuhuri walikotoka. Sasa Yesu hawezi kuwa mashuhuri kama mkombozi maana hata hajulikani ametokea wapi. Wakahitimisha, Yesu hawezi kuwa masihi. Kadhalika wayahudi walijua mkombozi ajaye atakuwa kama Musa wa pili, iweje huyu Yesu aponye mtu katika siku ya mapumziko na hivyo kufanya kazi tofauti na Torati ya Musa tunavyoifundisha? Yesu-mvunja sheria hawezi kuwa Musa wa pili wala mkombozi wa Israeli. Mpaka hapo utaona Mafarisayo hawakuwa tayari habari yoyote mpya inayotofautiana mtizamo wao wa kidini.

Wazazi wa Kipofu: Hawana ujasiri kueleza Yesu ni Nani

Kundi la tatu lililoshuhudia jinsi uponyaji wa kipofu ulivyomtangaza Yesu ni wazazi wenyewe wa kipofu. Wao walijua lakini hawakuwa na ujasiri wa kueleza walichojua. Walijua mtoto wao aliyezaliwa kipofu ndiye anayesimama mbele yao anaona. Walijua aliyeweza kufanya hivyo ni mkombozi kutoka kwa Mungu. Miujiza ya namna hii ndio walisikia manabii wa kale wakiifanya, na manabii walitabiri masihi ajaye angefungua macho ya vipofu. Walijua Yesu aliyefanya hivi si mwingine ila masihi. Lakini walipoulizwa kushuhudia kwa maneno imani yao kwa aliyemponya mtoto wao, walikwepa kwa hofu ya kutengwa na kunyanyaswa na vyombo vya dola.

Mpaka injili ya Yohana inafungwa, hatujasikia wazazi wa kipofu wakiwa wanafunzi wa Yesu. Huwezi kumtambua Yesu ni nani bila kumtangaza na bado ukawa mfuasi wa Yesu. Imani isiyokugharimu haina thamani, ikikugharimu utaithamini. Kama unajua Yesu ni nani usiogope kumtangaza kwa gharama yoyote na utaufurahia uhusiano wako naye.

Kipofu Anayeona: Hana woga kukiri Yesu ni Nani

Kati ya makundi yote yaliyoshuhudia uponyaji alioufanya Yesu ni kipofu pekee aliyefunguliwa macho ndiye aliyepata kumtambua Yesu ni nani. Maneno ya Yesu yalidhirika ukweli wake: “mimi nimekuja ulimwenguni humu kwa hukumu, ili wao wasioona waone, na wanaoona wawe vipofu” (39). Nuru ya Yesu iliyomfungua kipofu haikumuangukia kwa ghafla na kwa wingi usoni hata kumpofusha asiuone utukufu wa Yesu. Yesu alijifunua kwake taratibu taratibu na kipofu hakusita kuifuata nuru iliyokuwa ikimuangazia hatu kwa hatua. Mwanzoni alipoulizwa majirani zake nani aliyekuponya, alijibu, “mtu yule aitwaye Yesu” (11), baada alipoulizwa na mafarisayo anamwonaje Yesu, alijibu bila woga, “nabii” (17) na baadaye kidogo akaongeza kusema Yesu ni mtenda miujiza aliyetoka kwa Mungu (30-33). Baadaye Yesu alipojitambulisha kwake hekaluni, akaanguka chini kumsujudia akimuita, “Bwana.”

Kipofu anayeoona ni mfano wa kuigwa wa namna sahii ya kumuitikia Yesu kama Nuru ya ulimwengu. Nuru inapokuangazia usiipuuze kuifuatilia kama majirani walivyoipuuza wakabakia gizani, usiiogope kuikuikubali hadharani kama wazazi wa kipofu walivyokwepa kuikiri wakabakia gizani, na wala usipingane nayo kwa nguvu kama mafarisayo ukabakia gizani. Kubali hivi leo kutembea nuruni

Yesu ni Nuru ya Ulimwengu

Siulizi tena kwa nini mwanamume huyu agawe watu. Kwa kauli na matendo Yesu alijitambulisha kama Nuru ya Ulimwengu na hasa katika sura ya tisa ya Yohana. Hakumungunya maneno aliponena na hakuficha matendo alipoyatenda. Alikuwa wazi kama nuru. Lakini kama ilivyo asili ya nuru Yesu huangaza na kutia giza. Kwa wanaomkubali Yeye ni taa iongozayo wanaomkata ni giza la kujikwaa. Nuru ni ile ile, lakini humtia nuru macho huyu na humtia giza mwinginge. Wasioona wanaona na wanaoona wasione. Uamuzi ni wa mpokeaji. Amua leo pamoja nami kumkubali mwanamume huyu ili upokee nuru na uzima na furaha!




14/05/2013

Uponyaji Bethzatha: “Je, Wataka Kupona?” (Yoh 5:1-14)


Utangulizi

 Kama unatamani maisha bora zaidi ya uliyonayo sasa, usiondoke hapa; maana, unaweza kupata maisha mapya sasa. Lakini kabla ya yote unahitajika  kujibu swali rahisi lakini la muhimu. Swali ni hili, “Je, Wataka Kupona? Huwezi kukwepa kujibu swali hili kama unahitaji kupona. Mganga pekee anayeweza kukuponya haanzi kukutibu kabla hajakusikia utamjibuje. Na ndivyo Yesu Mkombozi alivyomuuliza mgonjwa mmoja swali hilo la msingi tunaposoma katika Injili ya Yohana 5:1-14:

1 Baada ya hayo kulikuwa na sikukuu ya Wayahudi, naye Yesu akaenda Yerusalemu.
 2 Huko Yerusalemu, karibu na mlango uitwao Mlango wa Kondoo, kulikuwa na bwawa la maji liitwalo kwa Kiebrania Bethzatha, ambalo lilikuwa nabaraza tano zenye matao.
 3 Humo barazani mlikuwa na wagonjwa wengi wamekaa: vipofu, viwete na waliopooza.*fa*
 4 missing 4maana mara kwa mara malaika alishuka majini nyakati fulani na kuyatibua. Mtu yeyote aliyekuwa wa kwanza kuingia majini baada yamaji kutibuliwa, alipona ugonjwa wowote aliokuwa nao.
 5 Basi, hapo palikuwa na mtu mmoja aliyekuwa mgonjwa kwa muda wa miaka thelathini na minane.
 6 Naye alipomwona huyo mtu amelala hapo, akatambua kwamba alikuwa amekaa hapo kwa muda mrefu, akamwuliza, "Je, wataka kupona?"
 7 Naye akajibu, "Mheshimiwa, mimi sina mtu wa kunipeleka majini wakati yanapotibuliwa. Kila nikijaribu kuingia, mtu mwingine hunitangulia."
 8 Yesu akamwambia, "Inuka, chukua mkeka wako utembee."
 9 Mara huyo mtu akapona, akachukua mkeka wake, akatembea. Jambo hili lilifanyika siku ya Sabato.
 10 Kwa hiyo baadhi ya Wayahudi wakamwambia huyo mtu aliyeponywa, "Leo ni Sabato, si halali kubeba mkeka wako."
 11 Lakini yeye akawaambia, "Yule mtu aliyeniponya ndiye aliyeniambia: `Chukua mkeka wako, tembea."`
 12 Nao wakamwuliza, "Huyo mtu aliyekwambia: `Chukua mkeka wako, tembea,` ni nani?"
 13 Lakini yeye hakumjua huyo mtu aliyemponya, maana Yesu alikuwa amekwisha ondoka mahali hapo, kwani palikuwa na umati mkubwa wa watu.
14 Basi, baadaye Yesu alimkuta huyo aliyeponywa Hekaluni, akamwambia, "Sasa umepona; usitende dhambi tena, usije ukapatwa na jambo bayazaidi."

Bethzatha



Swali “Je, Wataka Kupona? Limeulizwa katika kisa hiki. Kabla hatujaelewa swali hili, nakualika tutembelee eneo la tukio, na kufuatilia kwa karibu yaliyotokea katika hadithi hii. Kisa chenyewe kimetokea kandokando ya bwawa lililoitwa Bethzatha. Bethzatha ni jina lilitoholewa na Yohana kutoka kiebrania kwenda kwa kigiriki na limebakia hivyo hivyo katika biblia zetu za kiswahili—Bethzatha. Yohana  kama mwanahistoria makini hakumuacha msomaji wake akisie mwonekano wa bwawa lenyewe. Anatuambia kuwa bwawa lilikuwa limezungukwa na matao (mabaraza) matano. Kwa muda mrefu wasomi wasioamini walidhani hadithi hii ni ya kutunga, wakisema eti hakuna mahali kihistoria palipojulikana kama Bethzatha. Mpaka mwaka 1940 wafukuaji wa mambo ya kale (wajulikanao kama wana akiolojia)  walipofanikiwa kupata jiwe la kale lenye jina Bethzatha. Hivyo, hii si hadithi tu yenye fundisho. Hadithi ni ya hakika kama Bethzatha yenyewe ilivyo mahali halisia.

Yohana akitusimulia kisa kwa nia ya kutuminisha zaidi uhakika wa kihistoria wa hadithi yake anaendelea kutuambia Yesu alipitia lango gani akiingia Yerusalemu. Anasema Yesu aliingia Bethzatha kupitia lango lililojulikana kama “Lango la Kondoo” (leo watalii wanaozuru mji wa Yerusalemu ya zamani wanaambiwa panaitwa “Lango la mtakatifu Stefano.”).  Hili ni lango lililotumika kupitishia kondoo ndani ya mji wa Yerusalemu tayari kwa mauzo kwa mahujaji. Yesu kama hujaji aliingia mjini kwa kupitia lango hili, kaskazini-mashariki mwa mji. Karibu na soko hili Yesu akakutana na Bethzatha yenyewe. Ukubwa wa Bethzatha ni futi 150 kwa 300; kubwa la kutosha kupokea watu kwa mamia. Wenyeji wa Yerusalemu wanapaita mahali hapa Bethzatha, huenda wakimaanisha "Nyumba ya Neema." Nyumba hii ni bwawa la maji yanayoaminiwa kuponya maradhi. Na utaonai eneo limefurika wagonjwa waliotafuta neema ya kufunguliwa (kumbuka watu walivyojaza kwa babu). Anapokuja hapa Yesu anakutana na hospitali isiyo na kuta, kliniki ya iliyojaa vipofu, na viwete, na walioopoza wakiwa wamejazana! (Fikiria harufu ya kondoo upande huu na ya wagojwa upande huu, jiulize kwa nini Yesu aingie Yerusalemu kupitia lango hili!)

Inaonekana hakuna anayefahamu mpaka sasa nani aliyeingia hapa katika “Nyumba ya Neema.” Wagonjwa wa Bethzatha hawajui kuwa mahujaji aliyetokea Galilaya ni Bingwa wa magojwa! Yesu anawatazama kwa huruma.  Apande juu ya dari na atangaze kuwa saa ya neema imefika? Apaze sauti yake kuwaambia amefika awasaidie? Kwamba sasa anakwenda kuifunga hospitali hii na kuwarudisha wote nyumbani? Hapana. Huo sio mpango-kazi wa Yesu. Huwa Yesu hatangazi kazi zake, ila kazi zake zinamtangaza. Yesu akiwatazama wagonjwa, macho yake yakawa yakikimbia-kimbia kumpata mgonjwa aliyechoka kupita wote.

Katika wagonjwa wote, Yesu akaamua kumkaribia mgonjwa mmoja tu. Mgonjwa hajamwita Yesu na wala hamfahamu, lakini huyu ndiye anayetaka kumponya. Mgonjwa hajawahi kuita ama kuimba “usinipite
Mwokozi, unapodhulu wengine” lakini huyu ndiye Yesu anataka kumfikia. Kweli Bwana humrehemu amurehemuye na kumbariki ambarikiye, bila kujali imani ya mpokeaji. Mgonjwa huyu hana imani atapona tena. Mwanzoni aliamini atapona, lakini si sasa. Mwanzoni ndugu na jamaa zake waliamini, hata wakasaidia kumleta yalipo maji ya uzima. Lakini sasa hawaamini tena atapona, ndio maana wamemwacha mwenyewe. Kwa miaka 38 ameteseka na sasa yupo hapa mwenyewe pembezoni mwa maji ya uponyaji akisubiria uponyaji. Hana shamba, hana nyumba. Mali yake ni mkeka wake anaoulalia. Mikono yake imekakamaa kwa kutembea chini akijibuluta kama omba-omba. Ugonjwa wa kupooza miguu umewasababishia baadhi ya wagonjwa kujikojolea bila wao kuwa na habari. Inawezekana Yesu anapomkaribia mgonjwa ana harufu ya mkojo, mgonjwa amechoka!

Yesu anapomfikia, anainama kuanza kuongea naye. Hapo nyuma ni Nikodemu kiongozi wa Kiyahudi na afisa mwingine wa kirumi ndio walioanza kumsemesha Yesu. Lakini alipoongea na mwanamke msamaria aliyetengwa na sasa mgonjwa mchovu ni Yesu ndiye anayeanza kuongea. Yesu anajali masikini zaidi ya watu wote! Yes akamuuliza mgonjwa,"Je, Wataka Kupona?" Utadhani mgeni huyu anayesimama mbele ya mgonjwa haoneshi kumjali mgonjwa; atamuulizaje mgonjwa, "Je, Wataka Kupona?" Kwani yeye hajui mgonjwa yupo Bethzatha?

Je, Wataka Kupona?

Je, Uko Tayari Kukaribiana na Changamoto za Mtu Mwenye Afya?

Kwa haraka haraka utadhani kumuuliza mgonjwa kama anataka kupona ni kufanyia mzaha zahama yake, lakini ukilitazama swali lenyewe kwa ukaribu haionekani hivyo. Mara nyingine wagonjwa hawataki kupona. Mgonjwa anapopona anakuwa amemaliza seti moja ya matatizo lakini na kuibua mengine. Kuna changamoto za maisha zinazowafikia walio na afya tu! Kwa upande wa mgonjwa huyu, kwa miaka 38 hajawahi kugombana na viongozi wa dini, lakini leo atakapotoka miguuni pa Yesu atakabiliana na changamoto ya kutofautiana na viongozi wake wa dini. Atakapoponywa na kuamuliwa kujitwika mkeka wake na aende atakuwa anakwenda kinyume na walimu wake wa dini walivyomfundisha. Kumbuka kuwa kati ya mambo 39 wayahudi waliyokatazwa kutoyafanya siku ya sabato kwa kuwa kwa kuyafanya ni kutenda kazi mojawapo ni kubeba kitanda siku ya sabato. Mgonjwa yupo tayari kukutana na changamoto ya kutofautiana na viongozi wake? Atakuwa tayari kuwajibika kwa matendo yake kama mtu mzima, au ataishia kusema, “msinilaumu mimi, si kosa langu. Muulizeni aliyeniponya”? 

Cha ajabu ndicho mzee huyu alichokifanya (fungu 10). Alipotakiwa kuwajibika kwa matendo yake inawezekana akafika mahali akasema moyoni mwake, kuliko vita hii maisha yalikuwa bora pale kwenye mkeka wangu. Yesu akatafuta kumwokoa mgonjwa huyu na majuto ya kuingia kwenye maisha ya kujitegemea. Kwa lugha nyingine alikuwa anamuuliza, uko tayari kulipa gharama ya kuwa mtu mzima? Unahiari kukabiliana na changamoto za Mtu mwenye afya?

Je, Uko Tayari Kupoteza Fursa za Kubakia “Kwenye Mkeka”?

Lakini Yesu ana nia nyingine anapouliza mgonjwa wa Bethzatha swali hili. Kabla hajamponya, Yesu anamtaka ajihoji kama yupo tayari kupoteza fursa alizokuwa akizifaidi kama mgonjwa. Kumbuka wagonjwa kama huyu katika Yerusalemu ya karne ya kwanza walikuwa omba-omba. Omba-omba walijikimu maisha kwa fadhila za mahujaji waliokuja kuabudu Yerusalemu. Na mahujaji waliamini watapata thawabu kubwa
kwa kuwasaidia masikini wanapotembelea mji mtakatifu. Mgonjwa alifaidi fursa zote hizi akiwa kwenye mkeka wake. Rafiki, Kuna fursa za kubakia kwenye mkeka, na kabla ya kuponywa unahitajika kuhihari kupoteza faida hizo:
  • Ukiwa kitandani, shida ya kuamuka asubuhi kwenda shule haipo tena, Tuition huendi tena, homework hutakiwi kufanya tena; isipokuwa, unaletewa juisi, chips zinakaangwa, kuku wanapoteza maisha kwa ajili yako, unakaa ukiangalia TV muda wote. Lakini ukipona fursa zote hizi umezikosa. Je, wataka kupona?
  • Ukiwa mlevi, unajisikia kuchangamka, aibu hupotea, huna mawazo ya kukusumbua: hufikirii Mungu amenikataza nini, hukifikirii nitailisha nini familia yangu. Lakini ukipona fursa zote hizi umezikosa. Je, wataka kupona?
  • Ukiwa tapeli na fisadi, unajisikia mwerevu, unakula bila jasho, una muda wa kutosha kwa starehe zako. Lakini ukipona fursa zote hizi umezikosa. Je, wataka kupona?
  • Ukiwa kwenye ndoa haramu, bado kuna heshima unayopata (nimeoa, nimeolewa) na  matunzo unayofaidi. Lakini ukipona, fursa zote hizi umezikosa. Je, wataka kupona?
  • Ukiwa mwenye hasira, umezoea kumkasirikia mwenzi wako wa zamani, wazazi wako au Mungu wako, kuna utamu fulani unausikia unapokasirika. Lakini ukipona utamu umeukosa. Je, wataka kupona?
  • Yesu anapouliza, Je, unataka kupona? Kweli anahitaji kujua kama uko tayari kupoteza fursa zote unazozifaidi sasa uwapo kwenye mkeka wako.

Yesu amesimama pale pale na swali lile lile. Je unataka kupona? Utamjibuje? Utajibu: “labda baadaye?”, “Ndiyo”, au “Hapana”?

"Ninataka kupona" 

Bahati nzuri mgonjwa wa Bethzatha alitaka kupona. Japo hakutoa jibu la moja kwa moja lakini alionesha anataka kupona. Akaanza kumsimulia Yesu jinsi alivyohangaika kupata uponyaji bila mafanikio. Aliamini kama kila mmoja mitaani alivyoamini kwamba maji katika bwawa hili yakitibuliwa wa kwanza kuingia anapona. Imani yake ndiyo iliyomleta hapo, japo imani hiyo bado haijazaa matunda. Anamweleza kuwa amekosa mtu wa kumudumbukiza haraka maji yatibuliwapo. Utadhani anajaribu kumshawishi Yesu amsaidie kumtumbukiza siku maji yakivurugwa eti na malaika.Shida yake alikosa njia sahii ya uponyaji. Yesu akamsikiliza akimuhurumia. Bila kutafuta kumsahihisha kuwa imani yake kwa maji haya ni potovu na yeye hana muda na hadithi za mitaani, Yesu akaamua sasa kumponya.

"Simama, jitwike mkeka wako, uende" 

Yesu akitambua mgonjwa hamtambui yeye ni nani, akaamua kutoa amri ya kimamlaka: “Simama, jitwike mkeka wako, uende.”

“Simama, jitwike mkeka wako”

Ukinukuu maneno haya moja kwa moja toka kigiriki, lugha aliyoitumia Yohana utaona maana iliyokusudiwa: Simama (kitendo cha mara moja[aorist imperative]), jitwike mkeka wako (kitendo cha mara moja[aorist imperative]). Yesu anatamka kwa kishindo na anataka kitendo cha mara moja. Mara moja aamuke na aachane na mazingira ya ugonjwa wake. Hilo ni tendo la mara moja na upesi. Yesu hamwachii mgonjwa asema, “asante sasa nimeweza kusimama, ila kkilago changu nitakiacha hapa, ikitokea shida tena niikute nafasi yangu pembezoni mwa maji ya uponyaji.” Hapana, Yesu anamtaka mgonjwa aachane na maisha yake ya kale,. Aachane na aliyokuwa anayafanya. Anamtaka asimame na kujitwika godolo lake.

Kama mgonjwa wa Bethzatha ukitaka kupona, “simama, jitwike godolo lako uende”:
  • Ukitaka kuachana na ugonjwa uliokulaza miaka yote, nyanyuka tupa shuka na blanketi ondoka kitandani, simama jitwike godolo lako
  • Ukitaka kupona kutoka uvivu na kutojituma, simama jitwike mkeka wako
  • Ukitaka kupona kutoka kulazimika kufanya kazi na Sabato, achana na kazi hiyo, simama jitwike mkeka wako na uende.
  • Ukitaka kupona unywaji, kamwage chupa iliyosalia kabatini, achana na wanywaji wenzako, usizubaye  katika mazingira ya unywaji, simama jitwike godolo lako
  • Ukitaka kupona na hasira dhidi ya mpenzi wako, achana na mawazo yanayoamsha hasira yako, acha kujihurumia, acha kivitazama vidonda au makovu uliyosababishiwa, simama jitwike mkeka wako.
  • Ukitaka kupona kutoka mapenzi haramu, futa namba yake ya simu, usimpigie, usimtembelee, usiongee naye, simama jitwike mkeka wako.

Rafiki usisite kusimama na kujitwika gogoro lako. Kama kwa kusimama na kujitwika mkeka wako unaogopa utapoteza fursa ya kuwa pembezoni mwa bwawa la maji uliyoyaamini, tupilia mbali hofu yako, maana maji uliyoyaamini na kuyasubiria hayaja kukusaidia na ukiendelea kubakia hapo utakufa tu.
Mpendwa, najua mazoea yanatabu. Tunajisikia salama tukibakia kwenye mtindo wa maisha tuliyoyazoea. Lakini ndugu kama mazoea hayo hayatupi usalama, ni bora kuchukua uamuzi mgumu: achana na mazoea hatarishi. Tumeona Yesu akikutana baadaye na mgonjwa aliyepona na kumtahadharisha asirudie mtindo wake wa maisha ya dhambi yasije yakampata makubwa zaidi ya yaliyompata! Kama jicho lako, au mkono wako au miguu yako inakukosesha achanana viungo vyako, vingo’oe na vitupilie mbali, ni bora uingie uzimani ukiwa mpungufu kuliko kuingia Jehanamu ukiwa na viungo na mazoea yako hatarishi

 “...uende”

Tumesema ukiyasoma maneno aliyotumia Yesu katika lugha ya mwandishi utaona maana iliyokusudiwa ikibaki wazi: Simama na Jitwike [aorist imperative] ilikuwa ni amri ya mara kwa kitendo cha mara moja. Lakini sasa tunaposoma agizo la mwisho katika lungha hiyo hiyo ya awali (kiyunani) tunakuta Yesu anamtaka mgonjwa afanye kitendo cha mara kwa mara. Yesu anapomuagiza mgonjwa Uende, Yesu anamwambia mgonjwa adumu kutembea. Mgonjwa asiache kutembea, aendelee kutembea.

Mgonjwa wa kupooza aliyeponywa baada ya kusimama na mkeka kichwani angeweza kusema, “ndio nimesimama na godolo nimebeba, lakini miguu bado inauma, sikuzoea kutembea, hebu nisimame kidogo.” Hilo Yesu hakulitaka mgonjwa alifanye ndio maana akamwabia, “dumu kutembea”. Ushauri ambao Yesu anampatia ni ushauri ambao daktari yeyote wa mifupa angempatia mgonjwa wa Bethzatha. Mgonjwa wa mifupa ni lazima atembee mara kwa mara! Mgonjwa wa Bethzatha ni lazima adumu kutembea. Haitoshi asimame na kilago chake kichwani. Haitoshi apige hatua moja au mbili na kutegemea atabakia mzima. Ndio maana Yesu anamwambia dumu kutembea.  Na alichomwambia mgonjwa yule ndicho anatuambia sote: dumuni kutembea katika maisha mapya!
  • Haitoshi kuacha kulaghai na kutapeli kwa mwaka mzima, lakini ukibanwa sana unaongeza uongo kidogo ili ujikwamue, dumu kutembea katika mazoea mapya
  • Haitoshi kuacha kuvuta au kunywa kilabuni, lakini nyumbani unatumia chupa moja au mbili, dumu kutembea katika mazoea mapya.
  • Haitoshi kuacha kumsalimia mpenzi wako haramu kwa wiki moja, lakini wiki ya pili unasema hebu nimsalimie kidogo, dumu kutembea katika mazoea mapya
  • Haitoshi kuacha kukasirika ukiwa ndani katika nyumba ya sala, lakini tukitoka ibaadani huwezi kumsalimia, tembea sasa katika mazoea mapya.
  • Haitoshi kuanza kwenda katika nyumba ya ibaada kwa wiki mara moja au mbili lakini wiki zingine huuendi, dumu kutembea katika mazoea mapya

Rafiki huo ndio ukweli. Tukidumu kutembea katika uzima mpya tuliopokea, tutabakia uzimani, na hakuna hatari kwamba tutarudi kifoni.

Mwisho

Kwa hiyo swali ambalo Yesu alilomuuliza mgonjwa wa Bethzatha ndilo analomuuliza mtu yeyote anayetaka mabadiliko.  Je, wataka kupona? Hili ni swali linalostahili kujibiwa sasa kama wahitaji kupona sasa. Swali hilo linalenga nini katika maisha yako? Unahitaji kupona kutoka shida gani? Kama Yesu hakuwa na haja ya kukusaidia, unadhani angeuliza, unataka kupona?

Ombi pamoja nami ombi hili:

Bwana Yesu, hapa unasimama karibu yetu. Unajua mahali ulipotukuta. Tupo penye mkeka wetu, wapweke katikati ya watu. Unajua kushindwa kwetu maishani. Kama ni kushindwa kusamehe, kushindwa kupenda, au kushindwa kuachana na mazoea yanayotuharibu, Bwana wewe watujua. Sasa Bwana, umetuuliza leo kama tunataka kupona. Tusaidie tutake kusaidiwa. Tusaidie tuseme “Ndiyo, Bwana, Ndiyo, Bwana”. Hapa hapa Bwana kuna mtu anaomba, “nataka nipone, niko tayari kuponywa”. Bwana sikia maombi yetu. Sema nasi kwa sauti yenye nguvu na ya uponyaji, gusa akili zetu na mioyo yetu, mpaka tusikie maneno yako, “inuka, chukua mkeka wako uende” Tuachanishe Bwana na maisha yetu yaliyopita, na tembea nasi katika upya wa maisha. Ameni