- Kwa macho ya mwingine kanisa ni kama “kimbilio la wanyonge” huku kwa mwingine ni kama “nyumba iliyohamwa siku nyingi” (uzuri wa kitu upo katika macho ya mwonaji).
- Kwa mwingine kanisa ni mgodi wa hazina ya milele huku wengine kanisa ni shimo lililojaa mapokeo ya zamani (uzuri wa kitu upo katika macho ya mwonaji).
- Kwa mwingine kanisa la Lutherani ndio kanisa na huku kwa mwingine Katoliki ndio kanisa (uzuri wa kitu upo katika macho ya mwonaji).
- Tena kwa mwingine kanisa ni Wapentekoste na kwa mwingine ni Wa Sabato (uzuri wa kitu upo katika macho ya mwonaji).
Lakini macho
yetu sio kiongozi amini. Leo yananionesha mwanamke yule kuwa anapendeza. Kesho
yananionesha mwingine na kunifanya nipoteze hamu na wa jana. Hata kanisa nililoliona
jana limejaa ngano leo naliona limejaa magugu tupu. Macho yetu si kiongozi wa
kuaminika, hayatulii.
Na hapo nakusikia unauliza, hivi Mungu analitazamaje kanisa? Mungu anawachukuliaje watu wake? Swali zuri namna gani! Japo swali hili laulizwa leo, bahati nzuri jibu lake ni la zamani na uhakika kama injili ya Mathayo.
Kabla
Yesu hajawaambia wanafunzi wake mtazamo wake juu ya kanisa alijaribu kuwauliza
wao wanamtazamaje. “Watu hunena Mwana wa
Adamu kuwa nani?” (Mathayo 16:13).
Na Yesu akapewa majibu. Majibu
tofauti-tofauti kutoka mitazamo yao tofauti-tofauti. Kulikuwa na hao waliosema
Yesu ni Yohana Mbatizaji; wengine walisema Yesu ni Eliya; Yesu ni Yeremia; Yesu
ni mmojawapo wa manabii. Bila shaka Yesu alihuzunishwa na majibu yao. Kwa
sababu Yesu alikuwa zaidi ya Yohana Mbatizaji, Eliya, Yeremia, au nabii.
Baadaye, Petro akamtuliza Yesu kwa jibu sahii: “Wewe
ndiwe Kristo (Masihi-Mkombozi aliyetumwa na Mungu), Mwana wa Mungu aliye hai?”
Haleluya! Hapo, hapo Yesu akampongeza akimwambia, una bahati, huo sio mtazamo
wa kibinadamu, “mwili na damu havikufunulia hili, bali baba yangu aliye
mbinguni”(fungu la 18). Kwa lugha nyingine, Petro kwa
kuwa unanitazama kwa macho ya imani kama mwana wa Mungu na mkombozi, subiri
nitakueleza watu wenye imani kama yako ninavyowatazama. Kaa chini basi
nilitambulisha kanisa langu kwako kama ninavyolitazama. Umesikia Yesu anavyolitambulishaje
kanisa lake?
1. Kanisa ni Kama Jengo lililosimama Mwambani
Kwanza
kabisa ninamsikia Yesu akilitambulisha kanisa kama Jengo lililosimama Mwambani
(angalia nami fungu la 18a) “Nami
nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu”.
Tuanze na
Petro. Yesu anapompongeza Petro kwa kumtambua hamwiti Petro, isipokuwa anamwita
Simoni Baryona, hilo ndilo jina lake alilopewa na wazazi wake. Petro ni jina la
kupewa-“jina la ubatizo” (Yoh 1:42). Petro
lina maana katika kiyunani kama mwamba. Na katika kiaramaki (lugha mama
ya Yesu na Petro) mwamba huitwa kefa. Kwa kuwa Yesu alikuwa anaongea na Petro
kwa kiaramaki bila shaka Yesu aliongea hivi: “Wewe ndiwe Kefa (mwamba) na juu
ya kefa (mwamba) hili nitalijenga kanisa langu”
Simon
Baryona anaitwa Kefa na juu yake Kanisa litajengwa? Kweli Yesu, Simon Baryona
ni mwamba? Mbona baadaye Simon Baryona ulimwita shetani alipotaka kukuzuia
usiongelee habari ya msalaba? Simon Baryona ni mwamba? Mbona baadaye ulimwambia
“Shetani anataka kukupeta, lakini nimekuombea imani yako isitindike” Simoni
Baryona ni mwamba? Mbona baadaye alikukimbia dhoruba ya mateso ilipoanguka? Ni
mwamba gani unaoweza kusogea? Simon Baryona ni mwamba? Kanisa linawezaje kuwa
imara kama litajengwa juu ya “kefa” hili? Bwana unamwona sawa sawa Petro? Hapana,
hapana, Petro kama Petro anaitwa Mwamba
lakini tunamfahamu kama kijiwe, hawezi kuhimili uzito wa Jengo la kanisa na
kanisa haliwezi kuwa salama likisimama juu ya Petro tunayemjua.
Tulia, tulia….Ni
kweli Simoni mwana wa Yona ni sawa na wanadamu wengine. Lakini hapa Simon ameonesha
ukefa, upetro, umbwamba. Na ninyi ni mashahidi, wengi wamechagua kuyumbishwa na
upepo wa maoni ya watu kunihusu mimi. Wengi wameniona kama Yohana Mbatizaji,
Eliya, Yeremia, na kama nabii tuu. Lakini hapa Simon amejibu kama Petro (jiwe); amekataa kusogezwa na
maoni ya wengi, kama mwamba usivyosukumwa na upepo. Petro ni muumini wa kwanza kunikiri mimi kama Mwana wa Mungu.
Imani ya Petro kwangu kama Masihi na Mwana wa Mungu ni mwamba imara na salama
ambao juu yake nitalijenga kanisa langu. Kama unasita uliza historia.
Na hapo labda unataka kujua, Je! Yesu alijenga kanisa lake juu ya imani ya Petro? Ni kweli kanisa leo linasimama juu ya imani ya mtume Petro:
- Katika mathayo 16:16 Petro ni wa kwanza kumkiri Yesu kama Mwana wa Mungu.
- Katika Matendo sura ya 2 Petro ndio wa kwanza kumtangaza Yesu kama Masihi na Mwana wa Mungu kwa Wayahudi
- Na katika Matendo sura ya 10 tunamkuta Petro tena kama mhubri wa kwanza wa Yesu kama Masihi na Mwana wa Mungu kwa Wamataifa.
Kwa kifupi wayahudi kwa wamataifa wanaikiri imaini ile ile ya Petro kwa Yesu. Kama Petro wakristo leo:
- Tunaamini Yesu ni Masihi na Mwana wa Mungu hata kama wengine hawaamini hivyo.
- Leo hii tunaamini Yesu ni Masihi aliyetumwa na Mungu kutukomboa hata kama wengine hawamuoni hivyo.
- Tunamwona Yesu kama Mungu mwenye nguvu hata kama wengine wanamwona ni mwana wa Mariam tu.
Na ni imani hii ndio inayotufanya tusalie salama
kama jengo lililosimama mwambani. Imani hii na mtazamo huu ndio mwamba. Msingi
wa maoni ya wengi kuhusu Yesu kama nabii tu, mwalimu tu hautufai kusimamisha
imani yetu juu yake. Misingi hiyo haitulii kama mchanga wa mwambao. Leo ipo
kesho imechukuliwa na maji. Tunaposongwa na mitazamo tofauti tofauti juu ya
Yesu ni muhimu kutoyumbishwa kama Petro. Na tukisimamia katika imani ya Petro
tuko salama.
Hivyo, mbele ya macho ya Yesu kanisa la
Mungu ni Jengo linalosimama juu ya mwamba wa imani. Ndivyo linavyosimama mbele
ya macho ya Yesu.
2. Kanisa ni kama Jeshi lililoko uwanja wa vita
Lakini kanisa linashindana na nani? Linashindana na milango ya kuzimu. Na hapa kuzimu haiwakilishi kitu kingine
isipokuwa mauti na kifo (uf 1:18). Kutoka kwa dhambi ya Adamu na wengine tunajua dhambi huzaa
mauti (Yak 1:15). Na kama dhambi huzaa mauti, basi kanisa linapambana na dhambi na mauti--baba na mtoto. Adui wa kanisa sio wewe sio mimi na wala si wao; adui wa kanisa
sio waislamu wala wapagani, adui wa kanisa sio viongozi wake wala
washiriki wake; adui wa mtu sio baba yake, sio mme wake na wala sio watoto wake;
labda tu kama wamegeuka kuwa mawakala wa kifo na mauti.
Kanisa halijatulia na haliwezi
kutulia, mpaka limeondolewa uwanjani mwa vita, na dhambi na kifo vimetupwa Jehanamu. Wale
wanaolilia utulivu na amani watusubiri malangoni mwa Yerusalemu. Huko ndiko
hakuna maombolezo wala kilio wala maumivu (ufu 21:4). Wale wanalalamikia magugu
yamezidi kutubanaa, uovu umetusonga zaidi, watusubirie siku ya hukumu ambapo
wema na wabaya watatenganishwa milele. Kanisa ni Jeshi lililoko vitani, hivyo
ndivyo Yesu anavyoliona.
Wewe na mimi
tuko vitani. Inawezekana tumemkimbia Yesu, tumemkana hadharani,…. Hilo
halitukatishi tamaa, tunajua tuko vitani. Tunaweza kutetereka na kujeruhiwa. Si
neno, lakini hatutaitupilia mbali imani yetu. Mapambano yanaweza kuwa makari na
majeraha yetu yakatupunguzia damu nyingi na kutuliza usiku kucha, lakini hatutatupilia
mbali silaha yetu na imani yetu. Vidole vya wanao tushtumu na kutushtaki
vinaweza kuelekezwa mioyoni mwetu na kutukumbusha tulivyomkana Yesu, hatutakata
tamaa kutumaini wema wa Yesu. Kama tutabakia uwanja wa vita, hakika tutashinda.
Maana Yesu anasema, “milango ya kuzimu”hayatamshinda muumini anayemtumainia
Yesu kama Petro. Kama jiwe lililowekwa mlangoni mwa kaburi la Yesu halikuweza
kumzuia Yesu siku ya Jumapili ile, kadhalika hata sisi “milango ya kuzimu
haitatushinda” tunaposhikiria imani yetu.
Kujua kuwa
kanisa liko vitani kunanifanya nisilikatie tamaa ninapolitazama. Hata mimi
kujua niko vitani kunanifanya nisijikatie tamaa katika mapambano ya maisha na
imani. Kanisa ni la wapiganaji.
Mbele ya Yesu Kanisa ni zaidi ya jengo lilosimama mwambani, isipokuwa ni Jeshi linaloshindana vitani. Hivyo ndivyo Yesu anataka kila mmoja alitambua kanisa lake hivyo. Na zaidi ya hapo Yesu analitambua kanisa kama mlinzi wa malango ya ufalme wa mbinguni
3. Kanisa kama mlinzi wa malango ya ufalme wa mbinguni
Katika aya
hii ya Mathayo 16 Yesu anamalizia kulitambulisha kanisa kama Mlinzi wa malango ya ufalme
(angalia nami fungu la 19): “Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni”. Kwa maneno mengine Yesu anasema, "Kefa
nitakupa wewe funguo [wewe kefa ambaye
hukuteteleka kunikiri mimi kama Masihi na Mwana wa Mungu]. Wewe ni mshika
funguo, mlinzi katika malango ya ufalme.” Unaweza kufunga na kufungua, kuruhusu
na kuzuia, wewe ni mlinzi.
Lakini Kefa au waumini wanaokiri imani ya Kefa ni walinzi wa namna gani mlangoni pa ufalme?
Na kwa Petro na waumini wote, ujuzi na maarifa ya ufalme umetolewa.
Petro na
waumini tumefunuliwa na Baba wa mbinguni kumwona Yesu kama Masihi na Mwana wa
Mungu. Ufunuo huo ni ufunguo langoni mwa ufalme. Injili ya Yesu yaweza
kuwafungulia malango ya ufalme wote wanaoipokea na kuwafungia malango hayo hayo
wanapoikataa. Petro na sisi wakristo tumepewa funguo nyeti.
Lakini mwenzetu Petro alizitumiaje funguo
zake? Historia takatifu imerekodi kwa ufasaha jinsi mtume Petro alivyotumia maarifa ya kumjua Yesu masihi, kwa mfano:
- Petro alizitumia funguo hizo siku ya Pentekoste alipowaonesha wayahudi kuwa Yesu ni Masihi na Mwana wa Mungu aliye hai. Akawaambia, “Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi” (Mdo 2:38). Na siku ile wengi kwa kumsikia Petro na kukubali ujumbe wake walifunguliwa malango ya ufalme—tunaambiwa maelfu.
- Mara nyingine Petro alimfungulia malango ya ufalme Kornelio na nyumba yake na wote wakaingia (Mdo 10)
- Mara nyingine Petro akiwa na Yohana alimfungulia kiwete langoni mwa hekalu naye akapokea uponyaji
- Mara nyingine Petro na Yohana wakawafungulia wasamaria nao wakapokea Roho Mtakatifu
- Lakini mara nyingine Petro alimfungia Anania na Safira na hawakuingia katika ufalme
Funguo
alizopewa Petro ndizo tulizopewa. Tumepewa kuwafungulia watu wamjue Yesu kama
Mkombozi nao wafunguliwe. Na kama kila mmoja wetu aliyepewafunguo hizi
atazitumia wangapi wangepokea msamaha wa dhambi, wangapi wangefunguliwa na
utumwa wa dhambi, wangapi wangepokea uponyaji. Yesu analitambulisha Kanisa kama
walinzi katika malango ya ufalme. Ni bahati kuu kiasi gani lakini ni wajibu
mzito namna gani kumiliki funguo za lango kuu la uzima?