Utangulizi
Mwanamke asiye na Upendo wa Kweli
Nimewahi soma hadithi ya mwanamke mmoja ambaye hakufurahia
tena kumpenda mwenziye. Mumewe mama huyu alikuwa mgonjwa; ikabidi ampeleke kwa
daktari. Walipofika, daktari alibaki na
mgonjwa ofisini kwa uchunguzi huku mwanamke akibaki katika ukumbi wa mapokezi
akimsubiria. Daktari alipomaliza uchunguzi, akaja kukutana na mke wa
mgonjwa akiwa na uso wa huzuni.
Mwanamke kumwona daktari hivyo, hakuweza kutulia. Haraka akauliza, “Daktari,
mme wangu atapona?” Daktari akakusanya ujasiri na kumjibu: “ninaona mme wako ni
mgonjwa sana; na asipohudumiwa vya kutosha, hakika atakufa.”
Mwanamke akachoshwa kusikia hivyo! Baada ya kuvuta pumzi
kidogo, akuuliza, “una maana kuna matibabu yanayoweza kuokoa maisha ya mpenzi
wangu”? “Ndio” Daktari alijibu na kumwambia, “mmewe akipata matibabu stahiki na
huduma bora anaweza kuishi miaka mingi zaidi. Zaidi ya dawa atakazopatiwa
itabidi umpatie mwenzako huduma zifuatazo:
- Mrudishe nyumbani mgonjwa na umfanye kama mfalme,
- Mtayarishie chakula ulichopika mwenyewe,
- Mletee chai ya asubuhi kitandani,
- Nawisha mikono yake kabla na baada ya kula,
- Usimruhusu afanye chochote unachoweza kumfanyia,
- Kama anahitaji kitu mpelekee,
- Mminye-minye mgongoni asubuhi na jioni; mkande-mkande mwili mzima na mikono yako uliyoilainisha kwa mafuta,
- Aha..kuna lingine pia: kwa kuwa uwezo wa mgonjwa kukabiliana na magonjwa ni mdogo, hakikisha nyumba yako ni safi muda wote.
Baada ya maelezo hayo, mganga akamuuliza mwanamke kama ana
swali lolote. Mwanamke akatulia, pasipo swali la kuuliza wala neno la kuongeza.
Ndipo daktari akavunja ukimya na kamuuliza, “je, unataka nimwambie mumewe
kinachomsumbua na huduma stahiki anayostahili kuipata au utamwambia mwenyewe”?
Mke akazinduka na kujibu, “usijali, nitakwenda kumwambia mwenyewe.”
Basi daktari akamwacha na mwanamke akaenda kukutana na
mumewe. Lakini alifika chumba alipokuwapo
mgonjwa mwanamke alikuwa angali na uso ulioshuka na mashavu yaliyosinyaa.
Mumewe alipomwona hivyo akahisi mambo yameharibika na kuharakisha kumuuliza,
“vipi mpenzi, hali yangu ni mbaya sana? Kwani ninaumwa nini?” Mkewe hakujibu
haraka. Akingali anaangalia chini na mikono kifuani akajibu na kumwambia,
“Daktari amesema…. utakufa tu?”
Mwanamke hajajifunza kupenda kwa kweli na anashangaza! Hivi,
mgonjwa wake ni wa kufa tu? Lakini
isishangaze sana. Kwani wanaume na wanawake wangapi wanaofanana na mama
huyu, wangapi wanaopenda wakati wa raha
na wakati wa dhiki huishia? Wangapi wanaopenda kwa mahesabu na gharama ikizidi
hukimbia? Wangapi wanaopenda kwa moyo wote?
Petro asiye na upendo wa kweli
Ninapofungua Biblia ninamkuta mwanamume mwingine aliyempenda
Bwana wake lakini si kwa moyo wote. Mwanamume huyo ni Petro, mmoja wa wafuasi
wa Yesu. Petro alimpenda Yesu lakini si mara zote. Kwa mfano, Petro alimpenda
Bwana wake alipomwita amfuate, hata akaacha shughuli yake ya kumuingizia kipato
ili kumfuata Yesu. Aliweza kufuatana na Yesu kutokea Galilaya mpaka Yudea na
mpaka Yerusalemu lakini si mpaka Golgotha. Golgotha ya adha na fedheha na
mateso na kifo ilikuwa mbali mno na moyo wake; msalaba ulikuwa na gharama kubwa
kwa Petro kuuchukua. Kwa nini ataabike kwa ajili ya Yesu? Hata hivyo Bwana wake
atakufa tu.
Hatumsemi Petro namna hii kwa kuwa hayupo hapa kukanusha au
kujitetea. Rekodi takatifu na ya kuaminika inamuonesha mwanamume huyu mara
kadhaa akikataa kutaabika kwa ajili ya Bwana wake. Kwanza kitabu cha Mungu
kinatuonesha Petro akimuonya Yesu asizungumzie habari za kukamatwa na kuteswa
kwake (). Kitabu kinatuonesha pia kwamba
muda mfupi tu wale askari walipokuja Gethsemani wamchukue Yesu akiwa
katika pingu kama jangili korofi achukuliwavyo na polisi, Petro alipinga mpango
huo kwa upanga (). Tena tunasoma kwamba mara Yesu alipokamatwa, Petro alitimua
mbio na kuwashawishi wenzake kukimbia (). Hata alipokimbia, Petro alidai hamjui
Mgalilaya aliyefungwa pingu. Petro
aliona ni bora amkane Bwana wake kuliko kutaabika pamoja naye—hata hivyo atakufa
tu.
Lakini Yesu ni tofauti na mama yule na Petro huyu katika
kupenda. Bwana Yesu ni wa pekee. Yesu hupenda bila kuacha: akiachwa—haachi,
akichokwa—hachoki. Kumbuka, hata baada ya Petro kumuacha Yesu na kukimbilia
ziwani Yesu alimfukuzia mpaka huko (Yoh 21:3). Ziwani palikuwa ni mahali
mwafaka ambapo Petro alidhani angejituliza. Kwa kujishughulisha na uvuvi
alidhani anaweza akajisahaulisha majuto ya kumkana Bwana wake. Alfajiri hii
Yesu anapokutana na Petro, anamkuta Petro amehangaika usiku mzima bila mafanikio,
amechoka; hana wazo la Yesu kichwani wala samaki nyavuni. Yesu aliyeondolewa
duniani alikuwa ametoweka kichwani mwake. Lakini Yesu aliyefichika machoni pa
Petro mkimbizi akaamuru nyavu zilizoshindwa kupata nyavu usiku zishushwe chini
asubuhi hii. Ni samaki gani mjinga atauona mtego wa kumnasa na akaribie
nyavu? Petro alitilia shaka mbinu hiyo
ya uvuvi,akidai weledi na uzoefu wake wa uvuvi haumtumi kufanya hivyo. Pamoja
na mashaka hayo Petro akaona ajaribu kutii agizo, hata hivyo hajui aliyemwamuru
ana nia gani. Alipotii tu, Bwana akambarikia Petro samaki wengi ajabu! Samaki
walipojaa nyavuni, ndipo Yesu akarudi kichwani! Petro akang’amua kuwa kumbe ni
Yesu!
Hakuna
mahali Yesu hayuko
Weusi wa
usiku, nuru yake iko
Sitaenda
mahali Pendo lake haliko
Yupo hapo
tayari kokote niendako
Kabla
sijamuona, macho yake yako kwangu
Kama pumzi
niivutayo, yuko karibu yangu
Zaidi ya
baba, zaidi ya mama, yu rafiki yangu
Mwanzo mpaka
mwisho yu uzima yangu
Niendapo
popote yuko mbele yangu
Na alfajiri hiyo Yesu alitangulia mbele waliomkimbia.
Alijali hata akasimamia moto kuwashwa, ili miili ya
wavuvi iliyolowa na kutetema itiwe joto! Akasimamia uchomaji samaki-nyama choma- ili miili ya wavuvi hawa itiwe nguvu. Asubuhi hii Upendo umefanyika mwili na wavuvi wameuona utukufu wake. Upendo unaonekana ukitangaza na kusema, Petro hutakufa tu!
wavuvi iliyolowa na kutetema itiwe joto! Akasimamia uchomaji samaki-nyama choma- ili miili ya wavuvi hawa itiwe nguvu. Asubuhi hii Upendo umefanyika mwili na wavuvi wameuona utukufu wake. Upendo unaonekana ukitangaza na kusema, Petro hutakufa tu!
Petro katika Shule ya Upendo
Petro anapopigwa butwaa na utukufu wa upendo huu, Yesu
akaanzisha mazungumzo. Mazungumzo baina ya Yesu na Petro yameanza, huku wengine
wakiwa wasikilizaji. Natamani nisogee pembezoni mwa mahojiano yao. Masikio
yangu yanawasha kusikia Yesu anamwambia nini Petro baada ya Petro kumkimbia
Yesu na Yesu kumpata Petro. Sogea pamoja nami tufuatilie mazungumzo yao kama
yanavyopatikana katika Injili kama ilivyoandikwa
na Yohana, sura ya ishirini na moja. Fuatilia nami fungu la kumi na tano mpaka
kumi na saba (Yoh 21:15-17). (Unapofuatilia mazungumzo haya kwenye biblia yako,
linganisha na tafsiri yangu yangu ya moja kwa moja toka katika lugha aliyotumia
Yohana kusimulia kisa hiki, kigiriki. Kwa makusudi nitaacha bila kubadilisha
baadhi ya maneno aliyoyatumia mwandishi). Nami nasoma kama ifuatavyo:
15. walipokwishapata kifungua kinywa, Yesu alimuuliza Simoni Petro, “Simoni
mwana wa Yohana unanipenda kwa kweli [agapas me]? Naye akamjibu, “kweli Bwana wewe
unajua kuwa ninakupenda kama ndugu[filoo se].” Yesu akamwambia, “Tunza
wanakondoo wangu.”
16. Akamuuliza tena mara ya pili,
“Simoni mwana wa Yohana! Unanipenda kwa kweli [agapas me]?” Petro akamjibu,
“Kweli, Bwana; Wewe wajua kwamba ninakupenda kama ndugu [filoo se].” Yesu
akamwambia, “chunga kondoo wangu.”
17. Akamuuliza mara ya tatu,
“Simoni mwana wa Yohana! Je, unanipenda kama ndugu [filoo see]?” Hapo Petro
akasikitika kwa sababu amemuuliza mara ya tatu, “unanipenda kama ndugu [filoo
se]?” Naye akamwambia, “Bwana wewe [na si mwingine] wajua yote, wewe wajua
kwamba ninakupenda kama ndugu [filoo se].”
Natumaini umeyasikia mahojiano haya. Ninapoyatafakari
najiuliza, kwa nini Yesu amsemeshe Petro
namna hii? Je! inawezekana Yesu anatafuta kumsaidia Petro ajifunze kupenda
wengine kwa vitendo kama Yeye Bwana anavyompenda? Kama ndiyo, kwa namna gani
mazungumzo haya yanamsaidia Petro ajifunze kupenda kwa kweli? Niliporudi kwenye
mahojiano hayo na maswali haya kichwani, nikaona kwamba hapa Yesu anamfundisha Petro
ajifunze upya kupenda kwa kweli. Na anafanya hivyo kwa kumpatia masomo
yafuatayo.
Somo la Kwanza: Jua kuwa hujui Kupenda kwa kweli
Somo la kwanza ambalo Yesu alitaka Petro ajifunze kabla
hajajua kupenda kwa kweli ni kwamba hajui kupenda kwa kweli. Somo hilo Yesu
alilitoa alipomwita Petro mara tatu kwa jina, “Simoni mwana wa Yohana”.
Kumbuka, Simoni ni jina alilopewa na wazazi wake alipozaliwa; na Petro ni jina
alilopewa na Yesu alipokubali kumfuata. Kwa nini Yesu amuite Petro kwa jina la
zamani, jina alilokua akitumia kama mvuvi wa samaki na si jina la Petro
alilopewa na Yesu mwenyewe alipokubali kuwa mfuasi wake? Hapa, Yesu anamwita Petro
kwa jina la Simoni kumkumbusha Petro kwamba sasa amerudia jina lake la kale,
kazi yake ya kale, na maisha yake ya kale. Simoni sasa amefuata samaki ziwani
badala ya kufuatana na Yesu msalabani. Ni sawa Yesu amwite Petro kwa jina hilo
maana sasa anapenda kuvua zaidi kuliko kumfuata Yesu. Na kama si kuitwa hivi,
Petro atajuaje hajui kupenda bila kujulishwa kuwa hajui kupenda?
Lakini Yesu alipomwita Petro Simoni mwana wa Yohana –kumwita
hivyo kulimsaidia Petro apate ujumbe huo?
Au Yesu aliongea fumbo ambalo ni wewe na mimi tu, wasomaji wa leo,
tunaoweza kulifumbua? Hapana, ujumbe ulifika, maana Petro haoneshi tena ujuaji
wa Simoni. Simoni katika injili ni mjuaji na mbishi. Muda wote alikuwa akitamba
anampenda Bwana wake lakini si sasa. Kwa mfano, Petro alibisha alipoambiwa,
Simoni, Simoni Shetani anataka kukuingia ili unikane na na unikimbie (Luk 22:31-33). Petro alikataa
akidai labda wengine wangefanya hivyo lakini si yeye. Tofauti na wakati huo
sasa Petro anapoitwa simoni habishi wala hapingi. Nyavu zake alizonazo pembeni
yake ni ushahidi tosha wa kumuaminisha kuwa hajui kupenda—na hilo ni somo la
muhimu ambalo Yesu alitaka Petro ajifunze.
Yesu yupo tayari kuwasaidia wakina-Petro, wale wanaokiri
kuwa wafuasi wa Bwana, kutambua kuwa
hawajui kupenda kwa kweli-wamemkimbia na kurudia maisha yao ya kale. Kama alivyomwita Petro-Simoni vile vile Yesu anawaita wanaume na wanawake wanaokiri kuwa wafuasi wake lakini wanaishi sawa sawa na majina yao ya zamani. Yesu anawaita kwa majina yao akitaja: Ewe Simoni mwana wa kujiamini, Ewe Simoni mwana wa Kujiokoa, Simoni mwana wa kujihurumia, Simoni mwana wa kujipenda. Ewe Simoni…Simoni nakuita! Swala linalobakia ni kama akina Petro wakiitwa Simoni watajitambua? Watatambua kuwa wameyaacha majina yao ya ukristo na kurudia maisha yao ya kale? Watatambua kuwa hawajui kupenda kwa kweli?
hawajui kupenda kwa kweli-wamemkimbia na kurudia maisha yao ya kale. Kama alivyomwita Petro-Simoni vile vile Yesu anawaita wanaume na wanawake wanaokiri kuwa wafuasi wake lakini wanaishi sawa sawa na majina yao ya zamani. Yesu anawaita kwa majina yao akitaja: Ewe Simoni mwana wa kujiamini, Ewe Simoni mwana wa Kujiokoa, Simoni mwana wa kujihurumia, Simoni mwana wa kujipenda. Ewe Simoni…Simoni nakuita! Swala linalobakia ni kama akina Petro wakiitwa Simoni watajitambua? Watatambua kuwa wameyaacha majina yao ya ukristo na kurudia maisha yao ya kale? Watatambua kuwa hawajui kupenda kwa kweli?
Somo la Pili: Kubali kuwa hujui kupenda kwa kweli
Naamini Petro alijifunza somo hilo la awali, kwamba
amemuangusha Bwana wake, hajampenda vya kutosha. Lakini, zaidi ya kujua huku,
Petro anapaswa akubali (zaidi ya kujua akubali)
kuwa hajui kupenda kabla hajajifunza kumpenda Bwana wake zaidi. Hakuna
mwanafunzi anayeweza kuelimikia isipokuwa ameonesha haja ya kuelimishwa. Ndio
maana Yesu anamtaka Petro akubali anahitaji kujifunza kumpenda zaidi kwa kumuuliza,
“unanipenda…unanipenda…unanipenda”
Yesu hana mchezo anapomuuliza Petro “unanipenda.” Swali
limechongwa na lina makali ya kutosha kuchoma moyo wa Petro na kumliza.
Umesikia Yesu akiuliza na Petro akijibu? Katika kiyunani Yesu anauliza kama
Petro anampenda kwa kutumia neno tofauti
na ambalo Petro analotumia kujibu. Mara mbili Yesu anamuuliza Petro,
“unaniagape au unanipenda kwa kweli [agapes me]? na mara zote Petro alikwepa
kujibu anamuagape, ila akajibu,
ninakufiloo, au “nakupenda kama ndugu’ [filoo see]. Yohana na watumiaji
wa kiyunani cha Agano Jipya walielewa tofauti ya upendo wa Agape na Fileo, japo
mara nyingine waliyatumia maneno hayo bila kuyatofautisha. Agape ni upendo wa
kimbingu hasa baina ya Mungu na mtu; na fileo ni upendo wa kibinadamu baina ya
ndugu na ndugu. Mungu aliu-agape ulimwengu hata akamtoa mwanae wa pekee (Yoh
3:16). Hata Yesu alipomuuliza mara ya tatu unanipenda kama ndugu! Petro
alisikitika kwa kuwa swali hili la mwisho linaonesha kushindwa kwa Petro
kummpenda Yesu kwa kweli, kwa moyo wote, na bila kujali gharama, kama Mungu
ampendavyo mwanadamu. Mara hii ya mwisho ni kama Yesu anauliza, Petro!
“Unanipenda kama umpendavyo nduguyo badala ya kama nikupendavyo? Na Petro kwa
uchungu wa toba akajibu, “unajua Bwana, sijafikia kukupenda kwa kweli kama
unipendavyo; ila nakupenda kama ndugu kama nilivyozoea”. Kwa kusema hivi Petro
amekubali ameshindwa kumpenda Yesu kwa upendo wa kweli (agape).
Umeona? Hapa swali la Yesu kwa Petro unanipenda limefanya
kazi iliyokusudiwa moyoni kwa Petro; kwani limemuongoza kukiri amepungua
kupenda. Kwa kinywa chake amekiri kuwa amempenda Bwana wake kimazoea,
kibinadamu, kindugu tu tofauti na matazamio ya Bwana juu yake.
Kwa kuitwa Simoni, Petro alitambua hajaendelea kumpenda
Bwana wake lakini kwa kuulizwa unaniagape amekubali hajui kumpenda kwa moyo
wote. Ni vizuri kukubali makosa; usipokubali utawezaje kujifunza? Na Petro
alipokubali tu, Yesu hakusita kumfundisha mwanafunzi huyu apendeje.
Somo la Tatu: Hudumia wengine ufaidi upendo wa kweli
Katika mazungumzo haya hapo bichi ya Galilaya, Yesu
akaendelea kumfundisha Petro kwamba atapenda kwa kweli anapohudumia wengine kwa
moyo wote. Yesu akampatia somo hilo kwa kutumia kielelezo cha mchungaji na
kondoo wake. Kama mchungaji anavyowapenda kondoo zake kwa kuwatunza, Petro hana
budi kufanya vivyo hivyo. Kwani ulisikia katika mazungumzo yao, Petro alipokuwa
akimjibu Yesu kuwa anampenda kama ndugu, Yesu alimjibu nipende kwa kutunza
kondoo zangu; akimaanisha, nipende kama mchungaji apendavyo kondoo kondoo zake.
Petro atajifunza kupenda kwa kweli kwa kuiga kile mchungaji
anachowafanyia kondoo zake: kutunza. Petro angalia mchungaji anavyojali kondoo
zake. Kondoo wakipatwa na janga gongo la mchungaji na fimbo yake huwalinda;
kondoo wakiwa na njaa mchungaji huwapeleka “katika malisho ya majani mabichi”;
wakiona njaa huwapitisha “kando ya maji matulivu”; wakipotea huwarejesha
zizini. Kondoo wakivamiwa mchungaji hakimbii akisema hata hivyo watakufa tu;
isipokuwa anatetea maisha yao hata kwa gharama ya kupoteza maisha yake mwenyewe
(Yoh 10:11). Petro unanipenda? Iga mchungaji anavyowatunza kondoo wake.
Namna ya kuhudumia wengine kwa upendo
Kwa vipi Petro anaweza kupenda kama mchungaji mwema
anavyojali kondoo zake? Unawezaje pia?
Waone wahudumiwa kama sehemu ya nafsi yako
Ili Petro afikie kujali wengine kama mchungaji wa kondoo, anapaswa
kwanza kuwaona wengine kama sehemu ya
nafsi yake mwenyewe. Utakumbuka Yesu alisema mchungaji mwema huutoa uhai wake
kwa ajili ya kondoo zake (10:11). Na hiyo ina maana kwamba mchungaji
anawatazama kondoo wake kama sehemu ya nafsi yake, anawathamini kama
anavyothamini nafsi yake, hata kuweza kubadilishana nafsi yake kwa uhai wao.
Kwa macho ya mchungaji mwema: wao ni yeye na yeye ni wao. Lakini mchungaji
asiyejali huwaona kondoo kwa macho tofauti kabisa. Anawaona wao kama wao.
Anawatofautisha kondoo na nafsi yake. Hata kondoo wakipatwa na hatari, yeye ni
wa kwanza kuwakimbia. Maslahi yake ni ya muhimu kuliko mahitaji ya kondoo (Yoh
.) Kwa macho ya mchungaji wa mshahara mimi ni mimi na wao ni wao. Wao wakifa
bado mimi ni salama!
Hapana, hapana haipaswi iwe hivyo! Petro hataweza kupenda
kondoo kama atajiona yeye ni yeye na wao ni wao. Hata sisi hatuwezi kupendana
kama tuwaona wao ni wao na sisi ni sisi; sisi ni wanadamu wao ni wanyama tu,
sisi tunahaki ya kuishi wao hawana. Hata Paulo katika Matendo 17 Paulo myahudi
akiongea na wagiriki wa mji wa Atheni alisema, hakutofautisha wayahudi na
wayunani, Yerusalemu na Atheni aliponukuu mshahiri wa kigiriki kusema, “Sisi
wote ni uzao wake” (Mdo 17:28).
Na kama Paulo yuko sahii basi hakuna ukuta wa kututenga sisi
na wao. Nyumbani mwa Baba yetu sisi ni sisi: hakuna weupe kwa weusi, wamakonde
kwa wachaga, wakenya na watanzania, wakristo kwa waislamu, wanawake kwa
wanaume, matajiri kwa maskini, vijana kwa vikongwe, walemavu wa ngozi na wasio
walemavu wanashiriki damu moja. Wenzetu wakipoteza maisha ni damu yetu
imepotea, wakitembea uchi ni jina letu limeaibika, wakikosa chakula, madawa, na
elimu ni sisi tumekosa. Hatuwezi kutojali ndugu zetu wakibaguliwa, wakionewa,
wakisingiziwa uongo, wakiingiliwa kwa nguvu. Sisi ni walinzi wa ndugu zetu
kuwatetea, kuwalinda, na kuwaokoa. Maana wao ni sisi. Wao hawawezi kufa sisi
tukiwaangalia! Na ndivyo mchungaji wa kondoo anavyowatazama kondoo zake—
anawachukulia wao kama yeye.
Lakini kwa vipi tena Petro anaweza kupenda wengine kwa kweli
kama mchungaji mwema apendavyo kondoo zake?
Waone wahudumiwa kama mwili wa Yesu
Zaidi ya kuwaona kondoo kama sehemu ya nafsi yake, Petro
anapaswa kuwaona wengine kama mwili wa Bwana Yesu mwenyewe. Kumbuka, Yesu
alipomuuliza Petro unanipenda Yesu alijibu tunza kondoo zangu. Kwa lugha
nyingine Yesu anasema, Petro unapowatazama kondoo nione mimi mwenye mali. Mimi
sitakuwepo pamoja nawe kimwili kupokea upendo wako, lakini nina kondoo
wenye chapa yangu pamoja nawe. Tambua
sura yangu juu yao na unipende mimi kwa kuwapenda wao. Maana mimi mchungaji na
kondoo zangu tu wale wale.
Rafiki, somo alilopewa Petro latufaa sisi pia. Huwezi kusema
unampenda mzazi lakini si watoto wake, huwezi kumpenda Mungu usiyemuona huku
ukiwachukia viumbe walioumbwa kwa sura yake. Hivyo, utajifunza kumpenda
Mchungaji kwa kuwapenda kondoo wake:
- utajifunza kumtumikia Mungu kwa kutumikia watu wake
- utajifunza kumtetea Mungu kwa kutetea watu wake
- utajifunza kumsikia Mungu kwa kusikiliza watu wake
- utajifunza kumsifia Mungu kwa kupongeza watu wake
- utajifunza kumfurahisha Mungu kwa kufurahisha watu wake
- utajifunza kushirikiana na Mungu kwa kushirikiana na watu wake
Petro, kwa kuwa Mungu na watu ni kitu kimoja, penda Mungu kwa
kupenda watu.
Umuhimu wa kujua kuhudumia wengine kwa Upendo
Na hilo ni somo la msingi na la muhimu kwa wanafunzi wote
makini wanaotaka kufaulu kupenda kwa kweli. Maishani kila mmoja anapimwa upendo
wake na siku ya mwisho ya hukumu, kila mmoja atatahiniwa ufaulu wa somo hilo.
Ukijua utaepuka kuwa siku ya mwisho kwenye kundi la walioshindwa
Hata kabla ya siku hiyo ya hukumu orodha ya watakaofeli
imekwisha bandikwa katika ubao wa matangazo. Katika sura ya ishirini na tano ya
injili ya Mathayo, orodha waliofaulu kumpenda Bwana Yesu kwa kweli inashangaza.
Orodha inapungukiwa na majina yaliyoyatazamiwa na wengi. Wengi wa wahubiri
walioweza kunena kama malaika hawakuwamo, waliokuwa wajuzi wa unabii na siri
zote na maarifa yote hawakuwamo. Wengi wa waliokuwa na imani za kuamisha milima
hawakuwamo, waliotoa mali kulisha maskini hawakuwamo, waliojilipua kama wafia
dini hawakuwamo. Eti hao wote walifeli kwa kuwa walikuwa wakitumikia majina yao
na matumbo yao badala ya kuwatumikia watu wa Mungu! Jifunze kupenda leo usije
ukapatikana katika kundi hili.
Ukijua utaweza kuwepo siku ya mwisho kwenye kundi la walioshinda
Na ajabu majina ya waliofaulu kupenda watu kwa kweli
yanajulikana. Mathayo anawataja washindi hao kama wale waliolisha wenye njaa,
walionywesha wenye kiu, waliowatazama wagonjwa, waliotembelea wafungwa,
waliokaribisha wageni. Eti hao ndio wapenda watu, hao ndiyo wenye dini safi,
isiyo na hitilafu mbele za Mungu (ling. Yak 1:27).
Ukijua utaweza kuwepo leo kwenye kundi la wanaofurahia maisha
Basi nikawa na hamu kujua hawa waliofaulu walikuwa na siri
gani ya ushindi? Mbona wengine kama wao walifanya kazi hizi wazifanyazo lakini
wakafeli? Hivi wanajua watafaulu? Ile siku ya mwisho watajitapa wakisema, “ndio
tulijua tutafaulu, hata rekodi na takwimu ya mema yetu tunayo yanatushuhudia
kuwa sisi ni wa kufaulu tu?” Cha ajabu haikuwa hivyo; wale waliofaulu
walishangaa wamefaulu! Kumbe hawa walikuwa wasahaulifu. Walisahau mema
waliyotenda walipowafadhili wengine. Walipofadhili hawakutafuta mambo yao,
hawakujivuna, hawakujitangaza. Walikuwa wasahaulifu kweli kweli! Hawa walisahau
mabaya waliyotendewa walipowasamehe wengine, wakasahau uchungu wote,
wakavumilia yote, wakastahimili yote. Hata hawakujua walikuwa wanapimwa
walipokuwa wanaitikia mahitaji ya watu. Ndio maana watauliza, Bwana ni lini
tulikufanyia haya? Yesu atawajibu, “kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu
zangu walio wadogo mlinitendea mimi” (Mathayo 25:40). Kadri mlivyojali kondoo
zangu mlinijali mimi. Kumbe siri ya ushindi wao ilikuwa nikujisahau katika
kuwakumbuka wengine.
Bila shaka Petro alilielewa somo hili. Ukisoma barua ya
Petro ya kwanza utamuona Petro aliyejifunza kupenda kwa kutenda. Katika 1 Petro
5 Petro anawasihi wachungaji wenzie walichunge kundi la kondoo, si kwa
kulazimishwa, si kwa kutaka fedha za aibu, bali kwa hiari na moyo wa kutaka
kumfurahisha Mchungaji Mungu. Maana Petro mwenyewe anawaambia, “na mchungaji
mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyonyauka” (fungu 4).
Ni wazi Petro ameelewa somo: upendo wa kweli hautoki moyoni kwa kusukumwa au
kushinikizwa bila hiari na mahitaji ya watu; bali huwamwagikia wengine kutoka katika hazina yake pasipo
kuzuiwa na ubinafsi, hata huduma haiwi tena wajibu bali burudani.
Mwisho
Nimalizie kusema wewe na mimi tuna bahati. Tunabahati
kujifunza kutoka kwa makosa ya mama yule na Petro huyu. Hatuna haja kurudia
kumkana Bwana wala kuwaacha wahitaji wanaotunzunguka wafie mbali, na huku tukidai ni
wafuasi wanaompenda Mungu. Tuna bahati kujifunza toka katika kinywa cha Yesu
akimfundisha Petro namna ya kupenda kwa kweli. Nadharia imepatikana tayari, kilichobaki ni vitendo.
Basi tunapoamua sasa kubadilisha elimu hii kuwa vitendo halisi, tuombe.
Ombi:
Bwana na Mchungaji
wetu mwema, tunakushukuru kuvumiliana nasi katika kutufundisha kupenda. Ninajua
sasa na ninakubali ujazo wa upendo moyoni mwangu umepungua sana. Nihurumie sasa
na unijaze upya. Nipe kuwajali wengine kama unavyonijali mimi, nipe kujisahau
katika kuwakumbuka wengine. Tena unipe kutumika kupenda na usikose kunipa
furaha ya kupenda kutumika. Ahsante Bwana kwa kuwa umenipa nafasi nyingine ya
kupenda watu. Utukuzwe kwa neema yako, na uweza wako, sasa na hata milele.
Ameni.
Na Bwana akubariki sana sana unapopenda watu. Hata wakati
mwingine, kwa heri.