H
|
akuna heshima
ya juu ambayo Mungu anaweza kukupatia kama wakati unapofunga ndoa na mpenzi
wako. Na hiyo ndiyo heshima ambayo Mungu aliwapatia wazazi wetu wa kwanza. Adamu na Hawa walipokea heshima ya ndoa walipokuwa
bado wanaheshimika kama watoto wapya wa Mungu, waliotoka tu mikononi mwa
Muumbaji wao. Tunajifunza kutoka katika sura ya kwanza na ya pili ya kitabu cha
Mwanzo kwamba Mungu alimweka Adamu bustanini Edeni. Mungu alimpatia Adamu hadhi
ya mtawala/mfalme chini yake. Na kama mfalme wa sayari dunia Mungu akampitishia
wanyama wa aina zote ili awapatie majina. Pamoja na kazi ya heshima aliyopewa,
Adamu alipomaliza kuifanya alijihisi kama mtawala mpweke (umewahi kujikuta
umezingirwa na vitu na watu lakini bado mpweke?). Kwa Adamu, ilikuwa dhahiri
kwamba hakukuwa na kiumbe yeyote ambaye angemfaa kama “msaidizi wa kufanana naye”(Mw 2:18,20). Mpaka hapo, mbele ya
wengine Adamu alikuwa mfalme aliyetukuka kwa kupewa milki kubwa isiyopungukiwa
na aina za viumbe; lakini mbele ya macho yake, Adamu anajiona mwenyewe akiwa amepungukiwa.
Na ni ndoa pekee ndio ingeweza kuziba pengo
lililojitokeza pembezoni mwa Adamu mfalme.
Lakini inakuwaje kazi ya Mungu ya kwanza ipatikane na mapengo? Adamu alipunguaje wakati ndio tu ametoka kuumbwa? Mwandishi wa kitabu cha Mwanzo anapotoa angalizo kuwa Adamu hakuona ambaye angemfaa kama msaidizi wa kulandana nayei, je huku sio kutoa makosa kazi ya Mungu kwamba alipomuumba Adamu aliachia kazi njiani? Kwa kusema Adamu alimuhitaji msaidizi, lugha hiyo inamuumbua mfalme kama muhitaji na mwenye mapungufu. Lakini ni mapungufu gani, mbona ni kimtazama Adamu ninamuona ana miguu na tumbo na moyo na ubongo? Utasemaje hajakamilika? Adamu alilijuaje hilo? Na Mungu alimkamilishaje?
Adamu Mhitaji
Kweli
inasumbua kuelewa mfalme aliyepewa kutawala viumbe vyote apatikane na utupu wa kujazwa. Pamoja na kwamba Adamu alikuwa ndio
ametoka mikononi mwa Muumba asiye na kasoro wala doa (akiwa bado kwenye
karatasi za kiwandani), kusema ukweli, bado alikuwa hajakamilika. Adamu
mwenyewe alitambua hajakamilika alipoendelea na kazi ya kuwapa majina wanyama
walipokuwa wanaopita mbele yake. Ninapenda kutazama mawazoni mwangu Adamu
akiendelea na kibarua kazi yake ya kwanza ofisini:
ü Mnyama wa kwanza anapita mbele zake,
Adamu anaona mnyama huyo anaweza kumsaidia kulima anamwita Ng’ombe ( na
namsikia Adamu akisema, “aha kumbe ninaweza kusaidiwa kulima”).
ü Adamu anamwona mnyama mwingine wa
miguu minne akipita mbele zake, naye anamchunguza anaona anaweza kubeba mizigo
na anamwita punda (msikie tena Adamu akisema, “kumbe ninaweza kusaidiwa kubeba
mizigo”).
ü Na tena mnyama mwingine anapita
mbele Adamu akikimbia, Adamu anaona huyu anaweza kuchukua haraka atakako kwenda
na akamwita farasi (Adamu anasema, “aa kumbe ninaweza kusaidiwa kwenda haraka
nitakako kwenda”).
Na kwa
utaratibu huo huo wanyama wote wanapita mbele ya macho ya Adamu naye anawapatia
majina kulingana na tabia zao na namana wanavyoweza kumfaa. Lakini haraka sana
Adamu ameweza kuona wanyama na ndege hao wangemfaa kama wasaidizi chini yake na
si wasaidizi sawa naye. Biblia inasema, “hakukuonekana wa kumsaidia Adamu
aliteyefanana naye” (mw 2:20b).
Adamu
alitamani msaidizi ambaye atafanana naye. Bila shaka hapa Adamu alihitaji
mshirika mwenye hadhi sawa naye,
mwenye akili sawa naye, mwenye utashi sawa naye: kwa kifupi Adamu
alihitaji msaidizi anayelandana
naye. Kwa kupewa msaidizi-mshirika wa aina hiyo Adamu hakuwa na haja ya heshima
nyingine zaidi ya hiyo. Kama mshirika katika uhusiano wa karibu sana naye kama
wa mapenzi msaidizi msaidizi pembeni yake angefanana zaidi na yeye kuliko na
ng’ombe na punda na farasi na kasuku. Na ni mwenzi wa aina hiyo tu ndiye
angeweza kumpatia heshima ya kiwango sawa naye.
Huwezi
kuheshimika mbele ya macho yako kama anayesimama pembeni yako anakiwango cha
chini au hauendani naye. Unahitaji msaidizi mnayeweza kuabudu pamoja, mwenye
maadili ya juu kama yako, mwenye elimu ya kupelekana, na uzoefu wa maisha ya
kufanana. Haikupasi kutofautiana sana na mwenzio kama utapenda kutunza hadhi na
furaha uliyopewa na Mungu.
Mungu na Hitaji la Adamu
Kama Mungu
angeendelea kumwacha Adamu hivyo hivyo pasipo kumpatia mwenzi wa ndoa tungeona
kuwa hitaji la Adamu la ndoa ni la kufikirika tu na si la halisia. Na hapo
tungeona Mungu anamchukulia Adamu kama wanyama wengine waliomzunguka. Lakini
bahati nzuri haikuwa hivyo. Mungu akatafuta kuumba kiumbe kinachoweza kusimama kandokando
mwa Adamu kama mwenzie. Kiumbe hicho ni sharti kisiwe na hadhi ya chini kama ya
wanyama hata Adamu ahisi yeye naye ni wa hadhi ya chini kama mwenziye pembeni
yake. Na hapo hapo kiumbe hicho kisiwe cha hadhi ya juu kama malaika hata Adamu
ahisi ni mtu “bwana mdogo’ kando ya Goliati. Kiumbe huyo atapatikanaje? Mungu
akampulizia Adamu dawa ya usingizi. Adamu akalala. Operesheni ikaanza. Na Mungu
akachukua ubavu wake mmoja, na kumuumba mwanamke wa kwanza, Hawa. Na Adamu
akasema, “sasa huyu ni mfupakatika mifupa yangu, na nyama katika nyama
yangu...kwa kuwa ametwaliwa katika mwanamume” (Mw 2:23). Kwa kumpatia mwenziye
toka mbavuni mwake, Mungu anahakikisha Adamu anampata mwenziye wa kutembea
ubavuni mwake na si miguuni mwake wala kichwani mwake. Sasa Adamu anaweza
kutembea kifua mbele kama mwanamume kamili.
Adama
aliyeheshimika kwa kupata mke hakuwa na haja ya kuhofia kuumbuka kwa sababu ya
mapungufu yake:
ü Kwa kuwa wanalandana na msaidizi
wake, Adamu hawezi kuona haya kupanga mipango pamoja na msaidizi wake (na sio
kupasua kichwa mwenyewe),
ü Adamu anaweza kufanya kazi pamoja na
msaidizi wake bega kwa bega (na sio kupindisha mgongo mwenyewe),
ü Adamu anaweza kutembea pamoja na
msaidizi wake mkono kwa mkono (na sio kubaki mwenyewe), Adamu na mkewe wanaweza
kuzaa na kulea watoto pamoja, wanaweza kufutana machozi pamoja, wanaweza lala
pamoja, amka pamoja, abudu pamoja, ishi pamoja. Adamu alihitaji hakuhitaji
mwingine yeyote isipokuwa mwenzi.
Huwezi
kufuata nyanyo za Adamu na hawa katika kushirikiana na mwenzio, ukijazia
upungufu wa mwenzako, na bado ujisikie mpweke na duni pachoni pako na mbele ya
watu.
Mungu na Hitaji la Ndoa kwa Wote
Mwishoni,
mwandishi wa kitabu cha Mwanzo akatangaza nia ya Mungu ya mwanamume na mwanamke
kuishi kama wamoja katika uhusiano wa ndopo aliposema, “Kwa hiyo mwanamume
atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili
mmoja: (fungu, 24). Kwa kuwa ndoa ni kusudi la Mungu kwa wanadamu lililowekwa
wazi kiasi hiki, basi imepaswa kuheshimiwa na watu wote. Usitegemee ndugu zako,
wazazi wako, serikali yako wakuheshimu kama wewe mwenyewe huhiheshimu ndoa
yako. Wewe ni mwenye kuheshimiwe kama mwanandoa; iheshimu ndoa yako uheshimike.